May 11, 2015


Simba SC jana ilikutana na kocha wake aliyemaliza mkataba kwa sasa, Mserbia, Goran Kopunovic na kufanya naye mazungumzo ya kuendelea kukinoa kikosi hicho kwa msimu ujao lakini mambo hayakwenda sawa katika makubaliano na kuifanya ishu kuwa ngumu.


Kopunovic alitua kuinoa timu hiyo katikati ya msimu huu kwa mkataba wa miezi sita na kuifanikisha kumaliza kwenye nafasi ya tatu baada ya kuikuta inapumulia ‘mashine’ kwenye nafasi ya 12.

Simba imeonekana kuvutiwa na kazi ya kocha huyo anayeonekana kulipenda soka la vijana na jana ikalazimika kumuita na kuzungumza naye juu ya mustakabali wake ambapo inaelezwa kuwa kikao hicho kilichohudhuriwa na baadhi ya wajumbe wa kamati ya utendaji kilichukua takriban saa mbili bila ya majibu ya uhakika ya kocha huyo kuendelea na kazi.

Mmoja wa watu wa ndani wa Simba ameliambia Championi Jumatatu kuwa kikwazo kikubwa kuhusiana na kusaini mkataba mpya kwa kocha huyo ni kutokana na dau kubwa la usajili wake alilolitaja ambalo ni dola 50,000 za Kimarekani ambazo ni sawa na Sh milioni 100.

Chanzo hicho kiliongeza kuwa Kopunovic alitaka ada hiyo kwa mkataba wa miezi tisa mpaka 12 ambapo uongozi wa Simba kwa upande wao umepinga muda huo na kupendekeza wampe miaka miwili.

“Ishu inaonekana kuwa ngumu kwa sababu kocha amekazia ada yake ya usajili dola 50,000, fedha ambazo uongozi unaona ni nyingi na kingine ada hiyo anataka iwe kwa miezi tisa au 12 lakini uongozi unataka apewe miaka miwili, hapo ndipo kwenye mvutano mpaka sasa na mpaka wanatoka kwenye kikao hakukuwa na muafaka,” alisema mtoa taarifa huyo.

Baada alitafutwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe kuzungumzia suala hilo lakini hakupatikana baada ya simu yake ya mkononi kuita muda mrefu bila ya majibu.

Haikuishia hapo, alipotafutwa makamu mwenyekiti wa kamati hiyo, Kassim Dewji alisisitiza bado hawajashindwana na kocha huyo na kwamba mazungumzo bado yanaendelea.

“Si kweli kwamba tumeshindwana na kocha, isipokuwa bado tupo kwenye mazungumzo ya kuafikiana, leo (jana) tulikuwa kwenye kikao na tumekiahirisha mpaka siku nyingine ila mazungumzo yetu yakifika mwisho au kuafikiana chochote basi rais (Evans Aveva) atatoa tamko rasmi kuhusiana na hilo,” alisema Dewji.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic