June 15, 2015


UKIWA katika mitaa mbalimbali ya jiji la Mwanza, wadau wengi wa soka wanaonyesha hofu ya wazi kuhusiana na suala la klabu kongwe ya Toto African.


Wengi wa wadau hao wanaonyesha waziwazi kuhusiana na suala la kama kweli timu hiyo inaweza kuhimili vishindo na kubaki Ligi Kuu Bara msimu ujao.

Tatizo kubwa ni nguvu ya wanachama ambao wanaweza wakasema lolote bila ya kuhofia chochote kwa kuwa wao “ndiyo wenye timu.”

Wanachama wengi wa Toto African hawana tofauti kubwa na wale wa Yanga na Simba. Ambao hujiita wenye mapenzi makubwa, lakini kikubwa kinakuwa ni kuendeleza maslahi yao binafsi.

Mara kadhaa, nimekuwa nikiingia kwenye migogoro na wanachama wa Yanga na Simba, hasa wale wanaojiita Makomandoo. Kwa kuwa wanachofanya wao ni kuangalia watapata nini kwa kivuli kuwa wanaipenda timu yao.

Lundo la mashabiki wa Toto African wanaidai kuipigania timu yao si wanachama hai. Hawana mpango endelevu zaidi ya kukimbilia kulaumu tu.
KIKOSI CHA TOTO NA KOCHA WAO, JOHN TEGETE.

Wako walioshindwa katika uongozi kiutendaji na timu ikaporomoka daraja. Wako ambao hawakushiriki hata kidogo katika harakati za timu kurejea Ligi Kuu Bara baada ya kuwa imeporomoka. Kwa kuwa sasa imerejea, kila mmoja ana sauti.

Wako walioanza kuamini viongozi walio madarakani sasa ndiyo wakati wa neema kwa kuwa kuna fedha za udhaminiza Vodacom, Azam TV na huenda timu hiyo ikawapata wengine. Huo ni ulaji na sasa lazima wauchangamkie!

Toto African inasema haiwezi kukwepa historia, inataka iendelee kuwa chini ya Yanga. Kitu ambacho kimekuwa tatizo kubwa kwa kuwa mashabiki wa Simba wa jiji la Mwanza wanaamini timu hiyo si yao, jambo ambalo ni kosa kubwa.

Kwa sasa ndani ya Toto African kuna mgogoro mkubwa kati ya viongozi na wale wanaojulikana kama Toto African Ukawa. Ambao nao wana yao wanayotaka wasikilizwe, huenda ni sawa au si sawa, kwangu naona si vibaya wakisilizwa.

Wasikilizwe uli kutatua mgogoro huo, pia wakati wanasikilizwa, nao wanapaswa kukubaliana katika kuhakikisha suala hilo linakwisha. Kikubwa kiangaliwe ni maslahi ya klabu. Badala ya watu binafsi.

Lazima tukubaliane na kila mtu aitazame nafsi yake kwamba miongoni mwenu, wako mnaofuata maslahi na wale si mapenzi yenu na klabu. Mnaangalie kama kuna wengine watafaidika, nanyi mnataka. Mko mnaopiga kelele sababu ya njaa tu, mnajidai wakorofi lakini hamlengi maendeleo ya klabu.

Lakini wako mlio madarakani huenda mmetanguliza dharau, mkiamini nyie ndiye kila kitu na lazima muwepo ili katika klabu mambo yaende, jambo ambalo si sahihi pia.

Kikubwa hapa ni pande zote mbili kukutana zikiwa na lengo moja, maslahi ya klabu. Nilielezwa jana kuliratajiwa kuwa na mkutano wa wanachama kwa lengo la kumaliza tofauti hizo.

Kama utafanyika na kuwakutanisha pande hizo mbili, zikafikia mwafaka, basi utakuwa wakati mwingine wa kuonyesha upevu katika suala la maendeleo ya soka katika mkoa wa Mwanza.
Itakuwa aibu kuu mwakani Toto African ikiporomoka tena kwa ule mtindo wake wa “maji kupwaa…”.

Kuna haja ya Wanatoto African kuunganisha nguvu ya pamoja ili kuhakikisha nguvu ya klabu na pia kikosi kitakachokuwa kinapambana uwanjani.

Baada ya hapo Wanatoto African waunganishe nguvu na Wanamwanza wengine kwa kuwa Toto African ndiyo timu pekee inayoshiriki Ligi kuu Bara. Ndiyo itakayowasaidia kuziona timu zote zikicheza pale CCM Kirumba.

Hivyo kwa kipindi hiki, bado sapoti ya Toto African inaweza kuwa ya Kimkoa. Lazima muungane ili kufanya mambo makubwa. Kama mnataka kutengana na kufanikiwa, basi maisha ya klabu yenu na nyie wenyewe katika michezo yatakuwa ya kubahatisha tu!.






0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic