July 24, 2015


Kiungo mshambuliaji wa Yanga, Godfrey Mwashiuya kweli anatisha, wakati Wabongo wakimsifia kuwa anaweza kuwa staa wa baadaye wa timu hiyo, hilo limeonekana kuwa njiani kutimia, ndiyo maana mabeki wa timu ya Télécom ya Djibouti waliamua kutumia nguvu ya ziada kumzuia.


Mwashiuya ambaye alifunga bao moja katika mechi dhidi ya wapinzani hao katika Kombe la Kagame, juzi Jumatano, alijikuta akiwa katika wakati mgumu kutokana na mabeki wa Telecom kumchezea kibabe muda mwingi wa mchezo huo ambao alifunga bao kali.

Katika mchezo huo ambao Mwashiuya aliingia kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Simon Msuva, alikabwa kibabe na nahodha wa Telecom, Mohamed Wais Ali kiasi cha kumsababishia maumivu makali shingoni ambayo yangeweza kusababisha apoteze maisha kwa kushindwa kupumua.

Picha hapo juu ilibaini ubabe huo aliokuwa akichezewa Mwashiuya hata kama hakuwa na mpira dhidi ya nahodha huyo ambaye alionekana wazi kufanya hivyo ili kumtoa mchezoni Mwashiuya.

Yawezekana kutokana na ugeni wa mechi ngumu au za kimataifa, licha ya kubanwa kibabe na kuchezewa rafu mara kadhaa bado Mwashiuya alishindwa kuonyesha kujibu mapigo mbele ya beki huyo zaidi ya yeye kumtesa kila alipokuwa akipata mpira.

Kamera yetu ilimnasa Mwashiuya akikabwa koo kwa nguvu na Wais Ali ambaye wazi hakuonekana kuwa na huruma hata kidogo.

Wais Ali alitumia nguvu kubwa kumbana kooni kiungo huyo kiasi cha kusababisha akose pumzi na kuanguka chini lakini mwamuzi hakutoa kadi yoyote.

Alipoulizwa juu ya suala hilo na mchezo huo kwa jumla, Mwashiuya alisema: “Nimekatazwa kuzungumza lolote na vyombo vya habari.”

Daktari wa Yanga, Juma Sufian akizungumzia kuhusu kilichotokea kwa Mwashiuya alisema:

“Alipatwa na maumivu ya koo baada ya kukabwa, tulilazimika tumpe huduma ya kwanza mara tatu hivi, ilikuwa ni kumtuliza maumivu aliyokuwa nayo, baada ya mechi tulimuangalia alikuwa na alama za kucha kidogo chini ya kidevu na uvimbe kwenye sehemu za koo.

“Unajua aliumia na kupata maumivu makali kwa sababu kuna wakati alikabwa mpaka akavutwa koromeo, ndiyo maana ana maumivu mpaka leo asubuhi (jana), hata mazoezini alikuwa na uvimbe kidogo.”

Kuhusu madhara ya tukio hilo, anafafanua: “Kama angemuumiza zaidi athari zake ni kwamba angeweza kuvimba kwenye koo ndani au nje na inaweza kusababisha kushindwa kumeza na kupata maumivu zaidi ya hapo. Ikifikia hatua hiyo basi angeweza kuugua zaidi.”


SOURCE: GAZETI LA CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic