August 17, 2015


Na Saleh Ally
UNAIJUA tofauti ya ushabiki wa soka hapa nchini? Huenda ukawa ndiyo tofauti kuliko ushabiki wa aina nyingine yoyote duniani kwa kuwa watu ili waonekane wanapenda soka, lazima wawe wanazishabikia Yanga au Simba!


Lakini ukiwa England, kuna mtu humuelezi kuhusu Newcastle, Southampton, Leeds, Stoke City hata kama zitateremka daraja, kamwe, shabiki atakufa na timu yake.

Ukiangalia chimbuko, utaelezwa anatokea eneo ilipo Leeds United au Everton na si kuangalia timu kubwa tu yenye mafanikio kama ilivyo hapa, wote tunashindana kuwa Yanga na Simba.

Ilitakiwa anayetokea Shinyanga, leo mapenzi yake yawe kwa Mwadui au Stand United. Mwanza ni Toto African, Pamba au nyingine za mji huo. Mbeya waendelee na Mbeya City yao, Iringa wafe na Lipuli kama ambavyo Tanga wanavyoweza kugawana Coastal Union, African Sports au Mgambo.

Bado kunaweza kukawa na mapenzi ya wachezaji ambayo yanakuwa ya dhati kweli. Hii ni sehemu ya kuonyesha furaha ya moyo kwa mtu fulani kutokana na kile alichojaaliwa na Mwenyezi Mungu.

Bado tuna ugonjwa unaweza usiwe kwenye soka pekee, huu uko hata katika maisha ya kawaida kwamba hatuna tabia ya kukubali ubora walionao wenzetu. Badala yake tutashindana nao hata kama hatuna uwezo au kipaji kama chao.

Louis Diamond ni Mwingereza mwenye miaka mitano tu, sasa tayari ni mtu maarufu sana duniani hata kuliko Simon Msuva wa Yanga au Mussa Hassan Mgosi wa Simba.


Umaarufu wa Diamond umetokana na machozi yake ya dakika tano akilia kwa uchungu kutokana na kuumizwa na taarifa kuwa mshambuliaji Robin van Persie anauzwa na Manchester kwa kitita cha pauni milioni 23 kwenda Fernabahce ya Uturuki.

Mama yake alimrekodi mwanaye huyo akilia, akionyesha uchungu wa juu kwa kuwa van Persie anahama. Siku chache baadaye, idadi kubwa ikaiangalia video hiyo, Diamond akawa maarufu sana.


Klabu ya Fernabahce iliamua kutoa ofa kumsafirisha Diamond, wazazi wake na wadogo zake wawili kwenda Istanbul, Uturuki ambako waliishi kwa siku tano katika hoteli ya kisasa kabisa.
Wakapata nafasi ya kutembelea klabu hiyo, sehemu mbalimbali za mji huo ikiwa ni pamoja na kumuona van Persie, kupiga naye picha kabla ya kushuhudia akiichezea timu yake, mechi ambayo Fernabahce waliibuka na ushindi.

Theo Walcott alikuwa mwokota mipira, alivutiwa zaidi na Michael Owen wa Liverpool iliyokuwa timu yake ya kwanza kuishabikia. Wayne Rooney pia alifanya kazi hiyo na shujaa wake alikuwa Dancun Ferguson wa Everton, timu ambayo aliichezea zamani na wote hawa mapenzi yao hayakuwa ya kupikwa na walipenda timu zilizokuwa karibu na maeneo waliyotokea au kuvutiwa na mchezaji fulani.


Jiulize kwa nini unaipenda Yanga au Simba? Sababu za msingi ni zipi hasa na kweli mapenzi yako ni ya dhati kutoka moyoni au kwa kuwa Simba na Yanga zinaweza kukuletea mlo?

Mapenzi ya Diamond unaweza ukayachukua kama kipimo sahihi cha kuona namna kutokuwa wakweli ndani ya mioyo yetu kunakuwa chanzo cha kuuangusha mpira wetu.

Huenda mapenzi ya wengi kwa Yanga na Simba, hayana sababu za msingi. Ndiyo maana wanashindwa kuwa msaada na klabu hizo zinaendelea kubabaisha miaka nenda rudi!


Wengi hawaamini unaweza kuwa shabiki wa Mbeya City au Stand United au Ndanda FC pekee. Ndiyo maana Pamba, Lipuli, Kahama United, Kariakoo ya Lindi na nyingine zimebaki hadithi tu leo.

Lazima tujipime, lazima tukubali, mapenzi ya dhati tena yenye sababu ni hadithi njema ya mabadiliko sahihi ya kitu.

Usishangae siku ukisikia Diamond ni nyota wa Manchester United au Fenabahce kutokana na kilichotokea na atakuwa na kila sababu ya kufanya vizuri kwa kuwa ana sababu za msingi na za dhati kutoka moyoni mwake.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic