August 21, 2015


Na Saleh Ally
VIKOSI vya Yanga, Simba na Azam FC ndivyo vilivyosajili wachezaji wengi zaidi wa kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kujiimarisha.


Ninaamini hakuna timu hata moja iliyomsajili mchezaji wa nje kwa ajili ya kupata ujiko kwamba ina wachezaji wengi wa kigeni na inaweza kuwa na kikosi imara.

Lakini kila upande utakuwa umefanya hivyo kwa ajili ya kujiimarisha, lengo ni kujiweka sawa kwa ajili ya mafanikio.
Mafanikio ya Ligi Kuu Bara ni mambo mawili tu, moja ni kusaidia kupatikana kwa ubingwa au nafasi ya pili. Nafasi hizo mbili ndiyo zinatoa wawakilishi wa Tanzania kimataifa.

Klabu zinasajili wachezaji wa kigeni katika vikosi vya timu zao, lengo ni kufanikisha nilichokieleza hapo juu, lakini kwa wachezaji wazawa wa timu hizo yaani Simba, Yanga na Azam wanaweza kufaidika zaidi.

Hali halisi ilivyo, wageni wanalipwa zaidi kuliko wenyeji. Hali hii imekuwa ikiwapoteza baadhi ya wachezaji wazawa kutokana na kutojitambua na kisingizio ni hao wageni.

Wamekuwa na hoja za msingi kwamba hao wageni wanalipwa kuliko wao, wapo wanaopewa nyumba na wakati mwingine usafiri, mambo ambayo wao hawafanyiwi hata nusu yake.

Ukisikiliza wanachokisema wachezaji wazawa kwa kweli kina hoja na klabu zinapaswa kuyafanyia kazi malalamiko yao badala ya kuwaona sawa na wasaliti au watu wanaolalamika bila ya kuwa na hoja.

 Katika kikosi, suala la usawa ni bora lakini wachezaji nao wanapaswa kujua usawa wa kila kitu haiwezekani kwa kuwa kila mmoja anakuwa na aina yake ya uchezaji, mchango katika timu na tofauti hizo ndiyo maana ya timu.

Ninacholenga kuwaeleza wachezaji ni kwamba badala ya kuwa walalamikaji, kuna kila sababu ya kuhakikisha wanatumia makosa ya viongozi wao kuwajali zaidi kama changamoto.

Wana kila sababu ya kujiuliza maradufu kwa nini wageni wanaonekana wako bora zaidi kuliko wao? Baada ya hapo wajifue zaidi, wajifunze na ikiwezekana wawe na ndoto ya kupambana na kuhakikisha wanawazidi.

Lazima tukubaliane kwamba si kweli wachezaji wa nje ya Tanzania wanajua kila kitu kuliko wenzao wa hapa nyumbani. Lakini kuna mambo mengi yanamsaidia mchezaji kuwa bora zaidi.

Hata mchezaji awe na kipaji cha aina gani, lakini kama atakuwa si mwenye juhudi na anayejitambua, basi atakwama tu. Wachezaji wa hapa nyumbani wanapaswa kujipima kama kweli wanafanya hayo mambo.

Wajiulize, ubora walionao katika kipindi husika ndiyo mwisho wa safari na hawawezi kwenda zaidi ya hapo?

Lakini msisitizo wangu mwingine ni hivi, anayeshindwa ni lazima ajiulize maradufu kwamba wapi aliposhindwa na baada ya hapo apandishe kiwango chake.

Ninajua, ninaamini suala la majungu ndani ya timu za soka kupitia wachezaji linapewa nafasi kubwa sana. Wachezaji hamuwezi kukubali, lakini majungu katika sehemu yoyote yenye watu wengi hayakosekani.

Wavivu wanatumia mdomo kwa mambo yao mengi hasa unapotakiwa utendaji. Lazima wachezaji wajue ushindani ni sehemu ya chachu ya kupandisha ubora. Sasa hawawezi kufanikiwa kushinda kwenye ushindani kwa maneno mengi hasa kuulaumu uongozi.

Badala yake wanapaswa kuwatumia wageni hao kama sehemu ya ushindani wa dhati na kujiimarisha. Wakiona hawana kiwango, wanaweza kujifunza kwingine au kwa Watanzania wenzao. Katika soka kila siku mtu anajiuliza, wapi ametoka, alipo, pia wapi anakwenda.

Kuendelea kukaa bila ya kujituma halafu maneno ndiyo yanakuwa chachu ni kufeli tena na tena na mwisho ni kuishia kulaumu milele bila ya mafanikio.


Mimi ninaamini vipaji au ubora wa wachezaji wengi tu walio hapa nyumbani Tanzania. Lazima waukubali ushindani, waingie na kupambana nao kwa njia sahihi ambazo ni kuibua na kuboresha ubora wao ili wawe washindi. Majungu, hayajawahi kumsaidia yeyote kuwa mshindi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic