October 3, 2015


Na Saleh Ally
HIVI karibuni Msemaji wa Yanga, Jerry Muro, aliingia kwenye matatizo na wadau wa soka hasa baada ya kujisifia kwamba kikosi cha Taifa Stars kinaundwa na ukuta wa Yanga ambao ni wa kimataifa.


Alichokisema Muro kilikuwa ni sahihi kwa kuwa ukiachana na Shomari Kapombe, kipa hadi namba tano wanatokea Yanga na si kwamba wamependelewa, hakika ni uwezo wao, hilo halina ubishi.

Alichokisema Muro kilikuwa ni ukweli mtupu, lakini hata mimi nilipingana naye kwa kuwa alishindwa kusoma alama za nyakati, akazungumza tu.

Kwamba huu ndiyo wakati Watanzania wanataka kuinua morali ya timu yao ya taifa ambayo ilikufa kabisa kipindi cha yule Mholanzi, Mart Nooij ambaye kwangu niwe wazi tu, kaivuruga kabisa Stars na kuifanya kama sehemu ya kujifurahisha kwake.

 Niliambiwa kuna kiongozi mmoja wa TFF alikuwa akimhakikishia hataondoka. Ndiyo maana alikuwa anafanya anavyotaka, lakini alisahau ile timu ni ya Watanzania na si ya yule kiongozi aliyekuwa anamdanganya. Sasa amekaa kando, kocha ameondolewa angalau matumaini yanaanza kurejea.

 Siasa za Simba na Yanga zina nguvu sana, lakini wakati mwingine bora kupambana nazo ili kutafuta mafanikio ya mpira wetu ambao tunajua, unatambaa tu kila kukicha, haujawahi angalau hata kusimama ili tuanze kuangalia matumaini ya kutembea na baadaye tukimbie.


 Stars sasa ipo chini ya mzalendo, Charles Boniface Mkwasa ambaye ameonyesha njia kwamba tukiendelea kumuunga mkono kuanzia wachezaji, viongozi wa TFF, viongozi wengine na wadau wote wa mchezo wa soka, basi ataweza.

 Lakini inaonekana wazi suala lake lina mkanganyiko na sasa ni muda mrefu tangu tumekuwa tukisikia Mkwasa atapewa mkataba rasmi ili achukue kazi ya kuinoa Stars.

Niliambiwa Yanga na TFF walikuwa katika makubaliano na Mkwasa alikuwa amekubali kuondoka na kufanya kazi ya Taifa Stars. Tunajua hii haitakuwa mara ya kwanza kufanya kazi na TFF.

Alifanikiwa kuipeleka Twiga Stars katika michuano ya Kombe la Mataifa Afrika baada ya kuitwanga Ethiopia nyumbani kwao Addis Ababa kwa mabao 3-1.

 TFF wanamjua vizuri Mkwasa kwamba ni mchapakazi, ana uwezo wa kutoa msaada katika kikosi cha Stars na ameonyesha. Swali linakuja hivi, vipi suala lake la mkataba linakuwa la kuzunguka sana?

Kwa nini TFF wasimpe mkataba huo Mkwasa halafu waitaarifu wizara husika ianze kumpa ule mshahara wake ambao wakija makocha Wazungu wamekuwa wakilipwa?

 Kwa kiasi fulani nimekuwa nikiona hata wizara husika nayo inasuasua kutoa mshahara huo kwa Mkwasa kwa kuwa ni mzalendo! Kama itakuwa ni hivyo, basi litakuwa jambo kubwa baya ambalo hawajawahi kufanya kwa miaka mingi.


Hakuna kitu kibaya kama kujidharau, kujishusha. Huu ndiyo wakati pia wa kuonyesha mzalendo anaweza kufanya kinachoonekana kigumu. Vizuri kabisa apewe mkataba mpya na alipwe stahiki zake kama walivyolipwa makocha kutoka Brazil, Denmark na Uholanzi ambao baadhi walijitahidi na wengine hawakutusaidia lolote na bado walilipwa.

 Pamoja na kumthamini Mkwasa pamoja na msaidizi wake, Hemed Morocco na kumpa moyo zaidi kwamba anaaminiwa na Watanzania wapo pamoja naye, lakini itamuongezea uhuru zaidi wa kazi yake.

Saa hizi mwajiri wake ni Yanga, upande wa Stars ni deiwaka tu. Sasa kati ya hizo wapi utatoa kipaumbele? Jibu ni rahisi kwa kila mtu, hivyo TFF waliangalie hili kwa kuwa asije akaanza kuona kama anatumiwa kwa muda tu.

 Motisha itamfanya Mkwasa aone kweli anapewa thamani. Pia itapunguza maneno mengi.

Kama Mkwasa atakuwa kocha mwenye ajira Stars na wengine wakalaumu, basi hawatakuwa na hoja za msingi. Lakini wakati huu, lawama nyingine zinakuwa na mashiko.

Pia kingine ninachokiona, kocha wa timu ya taifa kuwa kocha msaidizi katika klabu, kiaina fulani haipendezi. Lifanyieni kazi.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic