November 16, 2015


SARE ya Taifa Stars dhidi ya Algeria iligeuka kitu kisichotarajiwa kwa njia tofauti ambayo pia haikutarajiwa.


Imekuwa ni mambo ya kisichotarajiwa kwa kuwa kabla ya mechi hiyo, wengi sana walisema Taifa Stars haina nafasi hata kidogo kwa Algeria na lazima itafungwa hapa nyumbani.

Kitendo cha kukosa mabao kadhaa na kuongoza hadi mapumziko, wengi wakageuka na kuanza kuamini Taifa Stars sasa ilikuwa na nafasi ya kushinda hata mabao manne. Safari hii wengi wakawa wamesahau kabisa kwamba waliamini Stars haina lolote dhidi ya Waalgeria hao ambao kwa ubora wa viwango vya Fifa, inashika nafasi ya pili barani Afrika.

Baada ya mechi kuisha, matokeo yakiwa ni 2-2, Algeria wakisawazisha mabao yote mawili, watu wengi wakaingia kwenye ule mtindo wetu kwamba ni lazima tulaumu tu kila linapotokea jambo lolote la mpira, iwe ni sare au kushinda.

Lawama zinamwangukia Kocha Charles Boniface Mkwasa ambaye aliamua kufanya mabadiliko katika dakika ya 63 baada ya kuwatoa wachezaji, Elias Maguri na Mudathir Yahya na kuwaingiza Mrisho Ngassa na Said Ndemla.

Hakika wakati mabadiliko hayo yakifanyika, niliingia hofu kidogo. Nikaona kulikuwa na dakika 27 ambazo zilikuwa nyingi sana kwa kutoa wenye uwezo mkubwa wa kukaba na kuingiza wengine kwa ajili ya kushambulia.

Kwa waliokuwa wameingizwa, ingekuwa Stars iko katika hali ngumu na inahitaji bao kwa namna yoyote, basi Mkwasa angefanya hivyo. Badala yake niliona ingekuwa sahihi kumuingiza Jonas Mkude ambaye ana nguvu na uwezo wa kukaba na sasa angekuwa bado na pumzi ya kutosha tofauti na Mudathir aliyekuwa amechoka.

Hii maana yake, Stars ingeweza kulinda mabao yake. Halafu ingewezekana kuingiza mtu mwingine wa kushambulia kama ilivyo kwa Ngassa kwa ajili ya kujaribu kupata bao la tatu ili kujihakikishia nafasi nzuri katika mechi ya pili.

Pili, niliona Mkwasa alifanya mabadiliko hayo haraka sana. Angalau kuanzia dakika ya 75 au kama ni mapema zaidi, mkabaji alihitajika zaidi ya mchezeshaji.

Pamoja na yote hayo, sioni kama kuna sababu ya kugeuza suala la mabadiliko hayo ndiyo gumzo kubwa na kuanza kulaumu kupitiliza.

Sare na Algeria bado ni jambo zuri na funzo kubwa kwetu. Pia jambo la kuwakumbusha wengi ambao waliamini Taifa Stars itafungwa hata mabao matano nyumbani kabla ya kufungwa tena wakienda Algeria.

Bado nashangazwa na watu wengi ambao hakuna hata mmoja anakumbuka kumpongeza Mkwasa kuhusiana na uamuzi wake wa kuanza na Maguri ambaye ni ‘Top Striker’ hapa Tanzania kwa sasa na kweli akafunga. Jiulize kama asingefunga, huenda wengine wangelia sana kwamba alikosea kumuanzisha ndiyo maana amechemka, bora angemuanzisha Ngassa!

Katika soka pia lazima tukubali, kocha anaweza kuwa na mipango, ikafanya kazi au kugoma. Hivyo lazima twende na mafunzo ya kila kinachofanyika.

Tumekuwa na makocha wa kigeni au Wazungu kama Mart Nooij, huyu anatokea Uholanzi. Stars imefungwa mabao hadi matatu na timu dhaifu kama Swaziland na Lesotho.

Lakini Watanzania leo wanalia au kukasirishwa na sare dhidi ya Algeria. Jambo ambalo kwangu nalichukulia kama hatua kubwa ya kimaendeleo ya soka nchini na hatupaswi kujilaumu na kama tunaona alichokifanya Mkwasa ni kosa. Kwake litakuwa funzo kama aliona hivyo, nasi tulitumie kama mafunzo badala ya kupoteza muda mwingi tukilalamika.

Kwamba tumeweza kutangulia kwa mabao mawili, halafu tumeruhusu yote yarejeshwe. Hongereni Watanzania mliojitokeza kwa wingi kuiunga mkono timu yetu, tuendelee kuiunga mkono kwa kuwa inacheza ugenini Algeria na bado ina nafasi na mambo hakika yanawezekana.

SOURCE: CHAMPIONI




2 COMMENTS:

  1. Watanzania ni mabingwa wa kulaumu, lazima tukubali kuwa Mkwasa alifanya kazi kubwa!! Hakuna aliyejua kuwa angeanza na Maguri lakini hilo bado hatulioni, asingefanya mabadiliko na tukafungwa watu bado wangelaumu kwa kutofanya mabadiliko ama kuchelewa kufanya mabadiliko!! Mpira una maajabu yake na lazima tujifunze kukubali matokeo, sio kila kitu siasa!!

    ReplyDelete
  2. Salehe umesema sawasawa kabisa kama ulikua kwenye kichwa changu, maana sisi watanzania tunajua kulaumu bana we acha tu...kama Ndemla na Ngasa wangefunga basi Mkwasa angekua Special one

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic