November 16, 2015


Matokeo ya sare ya 2-2 kati ya Taifa Stas na Algeria yamewaumiza vibaya wachezaji nyota wa Stars, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu kiasi cha kuhisi kuishiwa nguvu na kuwapa kazi ya ziada baadhi ya watu wa jopo la ufundi la timu hiyo kuwatuliza.

Hayo yalijiri wakati wachezaji hao wakiwa kwenye vyumba vya kubadilishia nguo muda mfupi baada ya kumalizika kwa mchezo huo uliopigwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mara baada ya kutoka uwanjani, wachezaji hao wanaoichezea TP Mazembe ya DR Congo, walionekana kunyong’onyea, kukosa nguvu na hata walipofika vyumbani, waliishia kulala sakafuni, kitu walichokatazwa kukifanya na mmoja wa viongozi wa benchi la ufundi kwa kuwa wanahatarisha afya zao.

Lakini wachezaji hao hawakuonekana kujali, hata walipotaka kuinuliwa, walionekana wazito huku wakiwa hawaongei chochote, baadhi ya memba wa Stars walijaribu kumvua viatu Ulimwengu na kumshawishi asiwaze kilichotokea kwani yanaweza kuwa makubwa lakini hakukuwa na mwitikio wowote.

Baadaye wachezaji wa Stars walilazimika kutoka vyumbani na kwenda kuzungumza na Makamu wa Rais, Samiah Suluhu aliyekuja kushuhudia mchezo huo, lakini bado kina Samatta hawakunyanyuka. Ikabidi itumike nguvu ya ziada kuwashawishi kuwa wasipokwenda inaweza kutafsiriwa vingine, ndipo waliporudiwa na nguvu angalau na kujinyanyua na kutoka vyumbani humo.

Kuhusiana na hilo, Samatta alikiri kujisikia vibaya lakini zaidi akasema hawana uhakika wa kufanya makubwa Algeria kwa kuwa wana mzigo mkubwa ambao unaweza kufuta ndoto zao zote za kusonga mbele.

“Tumetoa sare katika hali ya mchezo, siwezi kusema mengi lakini mchezo wa marudiano ni mgumu sana, si rahisi kwa kweli, tuna kazi kubwa na kila mmoja anawafahamu Waarabu, sijui, tusubiri marudiano,” alisema Samatta ambaye alifunga bao la pili katika mechi hiyo, la kwanza likifungwa na Elias Maguli wa Stand United.

Stars pamoja na mashabiki waliojitokeza kushuhudia mchezo huo, walikuwa na matumaini makubwa ya kuifunga Algeria kutokana na mpira mwingi uliopigwa uwanjani hapo lakini pia mabao mawili ya kuongoza yaliwatia jeuri Watanzania kabla ya matokeo kubadilika baadaye.


Huo ulikuwa ni mchezo wa raundi ya pili wa kufuzu kushiriki Kombe la Dunia 2018 nchini Urusi. Marudiano ni kesho Jumanne nchini Algeria.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic