November 6, 2015


Na Saleh Ally
JOHN Joseph Pombe Magufuli kaapishwa, ndiye Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Huu ni uthibitisho kipindi cha kampeni kimepita na tayari rais wa nchi amepatikana, hivyo heshima ichukue mkondo wake.
Niwe kati ya watu wa mwanzo kabisa kuungana na wengine watakaofuatia kumkaribisha Rais Magufuli.
Najua aliahidi ataishughulikia michezo, alisema atashughulika na masuala ya wasanii na mambo mengine mengi.
 Hakika Rais Magufuli ana mambo mengi sana ya kufanya na suala la kumpa muda halikwepeki kwa kuwa mengi atakayokuwa akiyafanya, pia yatahitaji muda.
Wakati akianza utekelezaji wa ahadi zake, tafadhali namkumbusha katika michezo nchini na kama akianza, basi katika mchezo wa soka kuna mengi ya kufanya pia.
Soka ndiyo mchezo unaopendwa zaidi nchini, namhakikishia Magufuli kwamba una uwezo wa kuwanufaisha watu wengi zaidi kuliko mambo yanavyokwenda kwa sasa.
 Mchezo wa soka kweli ni furaha na wakati mwingine maumivu ya watu. Lakini ni ajira, ndiyo maana unaona vijana wengi kama ingekuwa ni suala la kuomba kuajiriwa benki, mahakamani au kwingineko basi wasingefikia vigezo, leo wapo katika soka na wanalipwa mishahara mikubwa kuliko hao wa ofisini.
Vijana hao wanafaidi matunda ya vipaji vyao, lakini wana bahati mbaya bado hawajapata viongozi sahihi wa kuwaongoza na kuwatengenezea njia inayoweza kupitika.
Kweli Rais Magufuli atakuwa na kazi nyingi, ndiyo maana ninataka kumkumbusha asiisahau michezo na ikiwezekana iwe na wizara yake inayojitegemea kabisa ili iweze kuwa na mwendo sahihi.
Kuna kila sababu pia ya kuweka utaratibu wa kupambana na viongozi wababaishaji walio katika michezo ikiwemo soka.
 Simba na Yanga zina viongozi wengi wasio wakweli, wengi walio ndani ya klabu hizo ni kwa ajili ya maslahi yao na si Watanzania wengine. Klabu zao hazina hata viwanja vya mazoezi, TFF ilibahatika kupata wa msaada!
Ndani ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), nao kuna watu wasio wakweli, walio kwa ajili ya maslahi yao ambao hawaangalii nchi hii inataka nini, badala yake wao wanataka nini.
Wapo ambao wanatetea maovu kwa kuwa wanataka kufaidika wao. Wapo wanaotetea maovu ya rafiki zao angalau tu wawafurahishe na si kwa ajili ya mpira wa Tanzania.
Wapo rundo la watu wanaoimaliza michezo ya Tanzania na wana nafasi ya kuwa jeuri kwa kuwa tu wana hiyo nafasi na utaratibu unaonyesha hakuna lolote la kuwafanya. 
Kipindi chako, tafadhali iangalie michezo kama sehemu hasa ya mipango ya maendeleo ya taifa letu. Usiiangalie kama unaisaidia tu, usiiangalie kama ni sehemu ya ziada, michezo ina msaada mkubwa katika maendeleo.
Watanzania wamechoka na kudanganywa tangu enzi za Chama cha Soka Tanzania (Fat). TFF bado inaonyesha haina mabadiliko makubwa kwa kuwa ndani yake kuna chembe za uzembe ambazo hazijaisha pia.
Lakini vyama vya mikoa, navyo vinarithi na katika soka ndiyo kunaonekana kuna majungu makubwa badala ya maendeleo makubwa.
 Unaweza kushangaa, kwamba unawezaje kuingia huko. Lakini serikali yako inaweza kama itajikita na kutupa macho ya kutosha katika michezo, hasa soka. Tatua suala la viwanja kwanza, maisha ya soka yawe uwanjani zaidi ya kwenye makabrasha na majungu.
Serikali izipiganie timu zetu zinazoshiriki michuano ya kimataifa. Rwanda wanaweza vipi sisi tushindwe?
Mafanikio zaidi kupitia uwanjani, taratibu kutaanza kuwakimbiza viongozi wavivu wanaozidisha majungu badala ya kazi tu.
 Viwanja kwa ajili ya kukuza na kuendeleza vipaji, maeneo ya wazi yaliyoibiwa yarudishwe na ikiwezekana uwe unakemea viongozi wanaotuangusha maana wengine wanajidai wameziba masikio, lakini ukizungumza wewe, watayafungua tu hata bila ya kupigiwa hodi.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic