November 4, 2015


Na Saleh Ally
TAIFA Stars ni timu ya taifa ya soka ya kila Mtanzania. Hakuna anayeweza kujiita Mtanzania halafu akajigamba timu yake ya taifa ya soka ni nyingine zaidi ya hiyo.


 Kufanya vizuri au vibaya kwa Taifa Stars kutakuwa maumivu kwa kila ambaye angetamani kitu au jambo kutoka ndani ya taifa lake la Tanzania hasa kuona kikosi hicho kinafanya jambo lenye sifa njema au ya kujivunia kwake na Watanzania wengine.
 Taifa Stars Novemba 14, itakuwa uwanjani kuivaa Algeria kuwania kupata nafasi ya makundi kuwania kucheza Kombe la Dunia 2018. Kumbuka Algeria ni timu ambayo kama utazungumzia ubora wa viwango vya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa), ndiyo inaongoza barani Afrika.

 Algeria ina wachezaji bora na wanaotamba Afrika na Ulaya. Tunakubali ndiyo timu bora kwa maana hiyo. Je, tuitoe Taifa Stars kwenye mapambano?

 Kama jibu ni hapana, basi Taifa Stars lazima iungwe mkono nayo ipambane kwa juhudi hiyo Novemba 14 ambayo ni muhimu zaidi kwani itatoa majibu ya Taifa Stars ina mwelekeo gani kabla ya mechi ya marudiano ya Novemba 17 ugenini.
Wapo ambao wameonyesha kuingia uoga, mapema wamekuwa wakisema haitawezekana Taifa Stars kuifunga Algeria na kupata nafasi ya kuingia kucheza katika hatua makundi.

 Lakini wengine wametoa maoni yao kwamba badala ya Taifa Stars bora kuanza kuziangalia timu za vijana kwanza.

Kila Mtanzania ana haki ya kutoa maoni, lakini unaweza kugundua watoa maoni wanatazama mbali kiasi gani kulingana na hali halisi lakini kikubwa kwa kila Mtanzania kuhakikisha anaweka mkono wake kuisaidia Taifa Stars kwa maana ya kuipa nguvu pale uwanjani.

 Kuiacha Taifa Stars leo litakuwa ni jambo la kuchekesha sana, eti zianze kufanyika juhudi ya kukuza vijana. Nafikiri hilo limekuwa likifanywa na TFF na wameshaeleza malengo yao lakini msisitizo, vijana wanakuzwa na klabu zao kupitia vikosi vya watoto na vijana na si shirikisho la soka.

 Wakati huu ni kipindi sahihi cha kuwa pamoja na kuonyesha uchungu wetu kwa taifa letu. Katika soka mengi yanawezekana kuliko kuweka hisia hasi ambazo haziwezi kuwa na msaada.
 Mtanzania usikubali kushawishika kuwa Taifa Stars ni timu ya TFF, wao wamepewa jukumu hilo na wewe, mimi na Watanzania wengine kuisimamia timu hiyo na kuhakikisha inafanya vizuri.
 Huu ndiyo wakati wa kuonyesha kwamba, Watanzania wanaweza kuungana pamoja na kufanya jambo fulani kwa ajili ya utaifa. Kama kweli kutaonekana kuna matatizo, basi baada ya hapo tunaweza kukosoana kutokana na tulichokiona ila itakuwa ni baada ya kuonyesha uzalendo wa vitendo.

 Lakini kama tukifanikiwa, bado tutakuwa tumejifunza na tutajipongeza huku mafunzo tuliyoyapata tukiyafanyia kazi.

 Kama wakati huu hauungani na Watanzania wengine kuisaidia Taifa Stars kwa kwenda uwanjani na kushangilia kwa nguvu. Vipi utaweza kukosoa baadaye eti kikosi hakikufanya jambo fulani.
 Atakayekosea kwa kuwa alikuwa uwanjani, akaonyesha upendo wake, atakuwa na haki au ukosoaji wake utakuwa na tija kuliko aliyekaa nyumbani ambaye sasa anapiga kelele nyingi bila sababu za msingi.

 Algeria wanaweza kuwa wagumu sana, lakini ili Taifa Stars ivuke au kuleta kitu kipya au kuingia hatua nyingine, lazima ivuke na kuzing’oa timu bora kwanza.

Algeria kuifunga Tanzania halitakuwa jambo kubwa, lakini Taifa Stars ikawadondosha Waarabu hao wa Kaskazini, basi litakuwa ni gumzo kubwa na hiki ndicho ambacho Watanzania wanapaswa kukipigania kwa kuwa katika soka, mengi yanawezekana kuliko yanavyotarajiwa na ndiyo maana mchezo huo umekuwa na mashabiki wengi zaidi duniani kuliko mingine kwa kuwa si wenye majibu yenye uhakika kwa asilimia 100.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic