May 12, 2017



Huku harakati za Simba kuusaka ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu zikiendelea, mwenyekiti wa kamati ya usajili wa klabu hiyo, Zacharia Hans Poppe, ameionya Yanga.

Hans Poppe amewaambia Yanga wasijiamini na kuona kuwa tayari wameshauchukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara msimu huu, kwa sababu tu bado wana mechi nyingi mkononi, tofauti na Simba.

Yanga ipo kileleni ikiwa na pointi 62, sawa na Simba lakini ikiwa na uwiano mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa, huku ikiwa na mchezo mmoja mkononi.  

Hans Poppe amesema kuwa mchezo wa soka haupo hivyo kama wanavyofikiria kwani lolote linaweza kutokea mbele yao.
Alisema kutokana na hali hiyo, wamejipanga vilivyo kuhakikisha Simba inashinda mechi zake zote zilizobakia ili iweze kujitengenezea mazingira mazuri ya kunyakua kombe hilo.
 “Waache tu waendelee kushangilia lakini maajabu yanaweza kutokea na kuwaacha midomo wazi, kwa sababu mchezo wa soka una maajabu yake.

“Kwa upande wetu sisi tutaendelea kupambana kwa uwezo wetu wote ili kuhakikisha tunashinda michezo yote iliyobakia kwani kwa jinsi ligi ilivyo na ushindani mkubwa, Yanga bado hana uhakika wa kunyakua ubingwa huo licha ya kuwa na mechi nyingi ambazo hawajacheza tofauti na sisi.

“Mpaka aweze kupata uhakika huo, atatakiwa kushinda mechi zote zilizobakia jambo ambalo bado ni mtihani mkubwa kwake, hivyo mpaka sasa bado hawana uhakika wa kuwa mabingwa na hapaswi kuanza kushangilia kwa sasa,” alisema Poppe.


Mpaka sasa Yanga imecheza mechi 27 na imebakiza tatu ili kuhitimisha kivumbi cha ligi kuu msimu huu wakati Simba yenyewe mpaka sasa imecheza 28 na imebakiza mechi mbili.

SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic