August 28, 2017




LIGI Kuu ya Ujerumani (Bundesliga) ambayo kwa mashabiki wa Tanzania inaonyeshwa kwenye king’amuzi cha StarTimes wikiendi iliyopita iliendelea kwa kasi ya hali ya juu.

Mashabiki wa soka walikuwa wanasubiri kuona nini kinaweza kutokea kwenye michezo hiyo ya wikiendi, katika ligi hiyo ambayo huwa na kasi ya hali ya juu.

Staa wa Bayern Munich, Robert Lewandowski aliendelea kuibeba timu hiyo baada ya kuiongoza kwenye ushindi wa pili mfululizo walipoichapa Werder Bremen mabao 2-0.

Bremen ambao kwa Bayern Munich wamekuwa hawafui dafu, mara yao ya mwisho kuibuka na ushindi dhidi ya mabingwa hao watetezi wa Bundesliga ni mwaka 2006, ndiyo maana hata juzi Jumamosi walikuwa hawapewi nafasi kubwa ya kuwika.

Hata hivyo, mashabiki wengi walianza kupata hofu kwa kuwa Bayern walitakiwa kusubiri hadi dakika ya 72 kupata bao lao la kwanza ambalo liliwekwa kimiani na Lewandowski.

Staa huyo raia wa Poland, alifunga bao hilo baada ya kuiwahi krosi iliyopigwa na Kingsley Coman, hata hivyo, dakika ya 75 aliifungia timu yake bao la pili baada ya uzembe wa mabeki wa Bremen.

Lakini pia mashabiki wote walioshuhudia mechi hiyo, walifanikiwa kuona soka safi likitandazwa huku Bayern wakionekana kutafuta mabao mengi zaidi kwenye michezo hii ya mwanzoni.

Hata hivyo, pamoja na yote, Bayern wanatakiwa kumshukuru kipa wao Manuel Neuer, ambaye aliichezea timu hiyo mchezo wake wa kwanza msimu huu akitokea kwenye majeraha.

Wakati Bayern wakifanya hivyo, staa wa BorusSia Dortmund, Pierre-Emerick Aubameyang, naye alifanya kweli baada ya kuifungia timu yake ilipopata ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Hertha Berlin.

Kitendo cha Aubameyang kufunga na kufikisha mabao mawili, kinaonyesha kuwa sasa anaendeleza vita ya kuwania ufungaji bora kwenye Bundesliga na Lewandowski ambaye ana mabao matatu.

Aubameyang alifunga katika dakika ya 15 tu ya mchezo akiwahi krosi iliyopigwa na Nuri Sahin, hata hivyo, Sahin aliifungia timu hiyo bao la pili muda mfupi baadaye.
                         
Sasa staa huyo raia wa Gabon ameweka rekodi ya kufunga bao kwenye michezo nane mfululizo iliyopita ambayo ameshiriki.

Ushindi walioupata Dortmund, umewaweka kileleni mwa ligi hiyo kwa tofauti ya mabao ya kufunga dhidi ya Bayern Munich.


Matokeo mengine yaliwashuhudia Hamburg nao wakiendelea kushinda michezo yao miwili baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Cologne Ijumaa.

Wolfsburg walifurahia ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Eintracht Frankfurt kwa bao safi lililofungwa na Daniel Didavi kipindi cha kwanza.

Baada ya kuondolewa kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na Liverpool timu ya Hoffenheim ilitoka nyuma na kupata ushindi wa mabao 2-2 dhidi ya Bayer Leverkusen.

Mashabiki wa soka wanaotumia king’amuzi cha StarTimes waliwashuhudia pia Borussia Moenchengladbach wakiruhusu bao katika sekunde ya 35, kwenye sare ya mabao 2-2 dhidi ya Augsburg.

VfB Stuttgart walipata faida ya beki wao raia wa Ujerumani Holger Badstuber, aliyewafungia bao kwenye ushindi wa bao 1-0 nyumbani dhidi ya Mainz.


Msimu huu unaonekana kuwa mkali zaidi kwenye ligi hiyo kwani hata timu ambazo zilikuwa hazipewi nafasi kubwa ya kuonyesha kiwango cha juu uwanjani zimekuwa zikipambana na kupata ushindi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic