September 11, 2017


JUZI Jumamosi kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam, tulishuhudia mchezo wa Ligi Kuu Bara uliozikutanisha wenyeji Azam dhidi ya Simba. 

Matokeo ya mchezo huo yalikuwa suluhu. Awali kabla ya mchezo huo, hofu ilikuwa kubwa kwa mashabiki juu ya usalama wao, lakini Jeshi la Polisi Tanzania likawahakikisha kutakuwa na usalama huku likitoa angalizo kwa mashabiki kwamba wawe wastaarabu. 

Mashabiki walitahadharishwa mapema kwamba wanatakiwa kufuata utaratibu uliowekwa, lakini pia kwa wale watakaofika uwanjani na kukuta uwanja umejaa, basi warudi nyumbani na kushuhudia mechi kupitia luninga. Kikubwa ambacho naweza kuwapongeza mashabiki, walifuata kile ambacho walitahadharishwa mapema, lakini pia jeshi la polisi lilikuwa limejipanga tayari kuweka ulinzi wa kutosha kuhakikisha hakuna uvunjifu wa amani. 

Mwanzo mpaka mwisho wa mchezo, hakukuwa na vurugu zile ambazo wengi walikuwa na hofu nazo jambo ambalo linadhihirisha kwamba mashabiki wa soka hapa nyumbani wamestaarabika na kuondoa ile dhana inayoonyesha kwamba mchezo wa soka ni wa wahuni. Kumekuwa na dhana hiyo kutokana na kwamba, mara kadhaa kumekuwa na vurugu viwanjani ambazo chanzo chake ni mashabiki, lakini kilichotokea juzi pale Azam Complex, imeondoa dhana hiyo mbaya. Rai yangu ni kwamba, amani kama hiyo iendelee kutokea viwanjani kote ili kuepusha uharibifu wa mali viwanjani kama ilivyotokea Uwanja wa Taifa katika mechi kadhaa kama ile ya Yanga dhidi ya TP Mazembe na ya msimu uliopita iliyowakutanisha Simba na Yanga ambayo ilisababisha uwanja huo kufungwa kutokana na mashabiki kung’oa viti. Kutokana na vurugu kutawala sana viwanjani, siku za nyuma Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), lilishindwa kutoa ruhusa kwa Azam FC kuutumia uwanja wao huo kwa mechi za nyumbani dhidi ya Simba na Yanga. 

TFF ilikuwa haina imani na usalama wa uwanja huo kwa jinsi ulivyo, kwanza unaingiza idadi ndogo ya mashabiki ambayo ni 7000 tofauti na Uhuru unaoingia zaidi ya mashabiki 23,000 na ule wa Taifa unaochukua watazamaji 60,000. Mashabiki wa Simba na Yanga wanapocheza na Azam wanakuwa wengi, hivyo TFF ilikuwa ikihofia kuzuka kwa vurugu kama itatokea mashabiki watakuwa wengi tofauti na uwezo wa uwanja huo. Lakini baada ya jeshi la polisi kujiridhisha juu ya kujipanga kwao kulinda usalama na kuwadhibiti mashabiki, tukaona TFF ikiruhusu kwa mara ya kwanza kutumika na mpaka dakika tisini zinamalizika, Azam ikashindwa kufungana na Simba.

 Baada ya mchezo huo kumalizika kwa amani, tunatarajia kuona tena Yanga wakienda hapo na mambo yakiwa sawa katika suala zima la usalama kama ilivyo kwa wenzao wa Simba. Mwisho kabisa niwaambie Ruvu Shooting, Mtibwa Sugar na Mwadui FC ambao nao walikuwa wanataka kuona mechi zao dhidi ya Simba na Yanga zinachezwa kwenye viwanja vyao, kuvifanyia marekebisho ili kuipata haki yao. Kwa mujibu wa Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Kidao Wilfred, viwanja vya timu hizo ambavyo ni Mabatini, Manungu Complex na Mwadui Complex havina hadhi ya kuchezewa mechi hizo kutokana na kutokuwa na majukwaa ya kutosha. 

Kama kweli viwanja hivyo vinataka kupata haki kama waliyoipata Azam FC, hawana budi kufuata kile TFF inavyotaka kwani tayari wameambiwa juu ya kuweka majukwaa kwenye viwanja vyao ili hata zile mechi zingine wanazocheza hapo ziweze kuchezwa kwani wasipofanya hivyo, kuna hatari ya kufungiwa viwanja vyao.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic