BODI YA WAKURUGENZI SIMBA YAMPA MASHARTI MAGUMU MBELGJI
BODI ya Wakurugenzi wa Klabu ya Simba ikiongozwa na mwekezaji, Mohammed Dewji ‘Mo’ imempa masharti kocha wake Mbelgiji, Patrick Aussems kuelekea mchezo ujao wa Ligi ya Mabingwa Afrika.
Masharti hayo ni kuhakikisha anashinda katika mchezo dhidi ya JS Saoura, ikiwa ni pamoja na kuepuka kufungwa mabao mengi kama ilivyo katika michezo iliyopita.
Simba inatarajiwa kucheza mchezo wa marudiano dhidi ya Saoura, Machi 9, wakiwa ugenini ambapo katika mchezo wa awali uliochezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar walifanikiwa kuwafunga mabao 3-0.
Katika mechi mbili zilizopita za ugenini mbele ya AS Vita na Al Ahly, Simba walipoteza kwa idadi kubwa ya mabao baada ya kufungwa 5-0, jambo ambalo viongozi hao wanahitaji kuliondoa katika mchezo huo ambao matokeo mazuri yatawapa nafasi ya kutinga robo fainali.
Mtendaji Mkuu wa Simba, Crecentius Magori amesema kuwa, tayari bodi ya klabu hiyo ilishakaa na kocha kuzungumzia suala la kupata matokeo mazuri katika mechi dhidi ya Saoura kwa kuhakikisha wanafikia malengo na si kufungwa mabao mengi kama ilivyotokea katika mechi zilizopita.
“Tumeshakaa na mwalimu Aussems tumeshamueleza kuhusiana na mchezo wetu dhidi ya Saoura na anaendelea kufanyia kazi kile tulichomueleza kuhakikisha makosa yaliyofanywa katika michezo iliyopita ya Vita na Al Ahly hayajirudii, ya kufungwa mabao mengi.
“Kocha ameonekana kutuelewa kuhusiana suala hilo na hakutakuwa na makosa hayo tena.
“Tumejipanga kuhakikisha tunafanikiwa kupata ushindi katika mchezo huo ama kutoka sare ili tuweze kukaa katika mazingira mazuri ya kuingia robo fainali.
“Tunatarajia kuondoka hapa nchini mwanzoni mwa mwezi Machi ili kujiandaa vyema, maandalizi yanaendelea vizuri lengo likiwa ni kusonga mbele,” alisema Magori.
0 COMMENTS:
Post a Comment