February 3, 2020




INAWEZEKANA kabisa kama mshambuliaji wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Mbwana Samatta angekuwa hana uvumilivu na nidhamu ya hali ya juu pengine leo hii ndoto yake ya kwenda Ulaya ingekuwa ishaota mbawa.

Inahitaji uvumilivu na kuamini zaidi katika ndoto zako ili kuweza kukifanya kile ambacho Samatta ameweza kukifanya hadi kutua England na kujiunga na Klabu ya Aston Villa ambayo inashiriki Premier League.

Samatta ameweka rekodi ya kuwa Mtanzania wa kwanza kucheza Premier, ligi kubwa yenye umaarufu kemkem, hakuna asiyependa kucheza hapo. Tanzania tunajivunia yeye.

Lakini yote tisa kumi, nidhamu, kijana alikuwa na nidhamu ya hali ya juu tangu yuko Simba kisha akaenda TP Mazembe hapo akapanda ndege tena kwenda kujiunga na KRC Genk ambayo inashiriki Ligi Kuu ya Ubelgiji.

Sasa hivi yuko sehemu yenye baridi, England katika mji wa Birmingham, kwa sasa kuna baridi kali sana. Barafu limetanda juu ya nyumba za watu. Hapana shida Samatta anaweza kuvumilia maana akiangalia alikotoKa hasira za kusonga mbele zaidi zinamjia.

Sasa hiki ndicho kitu ambacho wachezaji wengine wengi wa Bongo wanakikosa. Uvumilivu hawana. Imewahi kutokea kuna mchezaji fulani aliwahi kwenda kufanya majaribio nje ya nchi na akafanya vyema tu akiwa kwenye hatua za kujadiliana masuala ya mkataba fasta akarudishwa nyumbani ili acheze mechi ya watani.

Inasikitisha sana. Samatta sasa kaonyesha njia. Kubalini kuifuata licha ya kuwa ina mabonde, milima na vikwazo vingine mbalimbali. Ninyi vijana mnaochipukia hakikisheni mnafuata nyayo za Samagoal hakika mtafanikiwa.

Samatta amekuwa ni mfano wa kuigwa kwa wachezaji wa Tanzania kutokana na uvumilivu na nidhamu ya hali ya juu ndani na nje ya uwanja jambo ambalo kimsingi limemjenga na kumfikisha hapo alipo sasa.

Safari ya kuelekea mafanikio kama aliyonayo Samatta inahitaji moyo wa uvumilivu, nidhamu na kutokubali kurudi nyuma hata kama safari hiyo ina vigingi na miba ndani yake.

Wengi wameenda kama alivyoondoka Samatta lakini mwisho wa siku tumekuwa tukishuhudia wakirudi kimyakimya na visingizio rundo, ambavyo asilimia kubwa vimekuwa havina mbele wala nyuma.

Waliobahatika kwenda Ulaya hawakudumu kwa kisingizio cha baridi kali au chakula kibaya! Walirudi nchini kwa sababu zisizoeleweka kutokana na kushindwa kuvumilia maisha ya ughaibuni.

Ule uhuru ambao walikuwa wameuzoea wa kwenda katika vijiwe vya Sinza, Temeke, Ilala au wale mabinti ambao wamezoea kila baada ya kutoka mazoezi au mechi ‘kujivinjari’ nao huko Ulaya hawapatikani kwa urahisi.

Sasa kwa kuwa Samatta katangulia Ulaya basi awe kama somo kwenu, msomeni, msimiss mihogo na chips za Sinza kwani zipo miaka yote, ninyi pambaneni kwanza na maisha na kuitangaza nchi yetu kimataifa.

Sasa mbele ya runinga tunamuangalia Samagoal akicheza mechi kwenye Premier League na mechi yake ya kwanza mbele ya Bournemouth pale Uwanja wa Dean Court, alitupia ikifikia mwakani basi tuwe tunakaa kuangalia mechi za Watanzania wengine wakicheza La Liga, Bundesliga, Serie A au hata Ligue 1.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic