February 1, 2020



SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) mnastahili pongezi kwa kuwekeza nguvu kubwa kwenye mpira wa Wanawake jambo ambalo matunda yake yanaonekana.

Tunaona kwamba kwa sasa timu ya Wanawake chini ya miaka 17 inazidi kusonga mbele ikiwa inasaka tiketi ya kufuzu Kombe la dunia kwa Wanawake ambalo linatarajiwa kufanyika mwezi Julai mwaka huu wamefika hatua nzuri wanastahili pongezi.

Ushindi wa jumla ya mabao 6-1 ambao wameupata mbele ya wapinzani wao wakubwa Burundi sio wa kubeza kwani inaonyesha namna gani wanajiamini na kutambua kazi ambayo wamepewa na Taifa.

Tuliona kwenye mchezo wa kwanza walianza kwa kushinda mabao 5-1 wakiwa kwenye Uwanja wa nyumbani wa Taifa jambo ambalo liliwaongezea kasi.

Tumeona kwamba wakiwa ugenini wameweza kufanya kazi kubwa kwa kushinda bao 1-0 hili sio jambo la kubeza kwani tunajua ugumu uliopo kwenye kusaka matokeo ugenini ila mwisho wa siku wameweza kufanya kile ambacho wengi hawakutarajia.

Yote kwa yote ni hatua nzuri ambayo watanzania tunapaswa tujivunie na kufurahia kuona timu zetu zinafanya vizuri uwanjani hasa kwa kupata ushindi hakuna jambo jingine ambalo tunalihitaji.

Kwa hatua ambayo mtafika Wanawake basi msisahau kwamba jukumu lenu uwanjani ni moja tu kutafuta matokeo mazuri na sio masuala mengine hayo yaacheni kwanza ambayo yanawasumbua nje ya Uwanja ndani chezeni soka la kitabuni.

Itakuwa ni fursa kwenu kujiweka sokoni na kufanya makubwa ambayo Taifa litakuja kupata faida hapo baadaye ninapenda kuona mkifanya vizuri hata Kocha Mkuu, Bakari Shime anaonyesha tabasamu la kweli pale mnapofanya vizuri.

Si kwa ajili yenu tu bali ni Taifa kiujumla linafurahi ila Shime anaiwakilisha ile jamii ambayo inawazunguka kwa kuwa anawatambua vema watanzania wanahitaji nini kutokana na uzoefu alionao na maisha yake ya soka anatambua walikuwa wanahitaji nini.

Mashabiki pia msikate tamaa pale ambapo timu inashindwa kupata matokeo ambayo mnayatarajia kwani kuna mengi ndani ya Uwanja yanatokea na ukizingatia hawa ni Wanawake wanapambana kutafuta furaha ya Taifa wanapaswa wapewe sapoti bila kuchoka.

Mechi zao tusiwaache peke yao ama zikawa ni za watu fulani hapana mashabiki hii ni timu yetu sote tunapaswa kujitokeza kwa wingi uwanjani kuzipa sapoti timu zetu zote zinapocheza bila upendeleo.

Kuna mambo ya msingi ambayo yakifanywa na TFF  ninaona kwamba mpira wa Wanawake utasonga mbele na kuvuka mipaka zaidi ya hapa ambapo ipo kutokana na mwanzo ambao tumeanza nao.

Kwanza timu za wanawake ziboreshewe mazingira yao hasa kwa namna ambavyo zinacheza mechi zao pamoja na mazingira ambayo yanawazunguka kwa sasa.

Ukweli ni kwamba timu nyingi hapa Bongo maisha yao ni ya kishkaji watu wa mtaani wanasema hivyo kutokana na kutokuwa na uhakika wa kupata mahitaji ya msingi kwa wachezaji.

Hili ni tatizo ambalo linazikumba timu nyingi na kuna wakati zipo timu ambazo hata kusafiri ni shinda kufika sehemu ambayo wanatakiwa kucheza hii ni mbaya.

Ule mtindo wa kuchangishana fedha na kupigiana simu kwa wadau ndio mchezo mkubwa ambao upo nyuma ya timu nyingi za Wanawake hali hii sio shwari inachelewesha mafanikio ya soka letu.

Timu zao zinapenda kupata matokeo chanya ila zinakutana na vikwazo vingi kuyafikia hayo mafaniko jambo ambalo linapaswa litafutiwe dawa mapema ili kuboresha kwanza timu.

Imani yangu ni kwamba timu zikiwa zinatoka kwenye mazingira bora ushindani utakuwa mara dufu zaidi ya sasa na wachezaji watakaopatikana kuunda timu ya Taifa watakuwa ni bora kwa ushindani.

Wachezaji waboreshewe pia hata aina za viwanja ambavyo wanatumia hapa wanapata taabu sana ukizingatia maumbile yao yalivyo na namna ambavyo wanacheza kwenye mazingira magumu hii pia inakatisha tamaa.

Viwanja vyao vinapaswa viwe rafiki. Kila iitwapo leo wanapata majeraha ambayo sababu kubwa inatokana na tatizo la kutokuwa na viwanja bora katika hili TFF msifumbe macho litazameni kwa ukaribu.

Vyanzo vya fedha pia ni tatizo lingine hawa wakipewa nguvu na njia ya kupata sehemu ya kipato itapunguza ule ukali wa maisha ya soka ukizingatia kwamba kila mchezaji ana ndoto zake.

Wadau na wadhamini hapa wanahitajika ili kufungua milango na kuwapa fedha hawa wamiliki wa hizi timu ili waboreshe mazingira ya wachezaji wetu.

Pia kwenye kambi zao mazingira yao yanapaswa yawe ni bora na vifaa vyote vya michezo viwe vinapatikana isiwe llimradi kambi tu hiyo sio sawa.

Vipaji vipo hapa Tanzania tena vingi ila namna ambavyo vinatunzwa pia bila kujali inapoteza ule morali na kuwaua wale wenye uwezo kutokana na kutokuwa na misingi imara.

Kipaji  ili kikue kinahitaji matunzo na kuwa na mtu sahihi ambaye anawasimamia endapo tutachukulia haya masuala katika hali ya ukawaida basi tusitarajie kupata matokeo mazuri.

Ugumu wa kazi unatokana na kutokuwa na vifaa pamoja na miundombinu kutokuwa rafiki ni wakati wa kuona namna gani tutaondoa haya matatizo yaliyopo kwenye soka la Wanawake.

Uwezo upo kwa vipaji hasa ukizingatia kwamba kwenye ligi ya Wanawake ambayo ipo na inaleta matunda wengi wamekuwa wakionyesha vile ambavyo wamebarikiwa na Mungu vipaji.

Namna ya kuwaboreshea vipaji ndiyo njia sahihi ya kuzidi kuboresha sekta ya mpira wao na kwa wale wadau na wadhamini ni muda wa kujitokeza kuwekeza huku ili kuzidi kuwaongezea nguvu.

Timu zote duniani zinaanza kunyanyuka kwenye ligi ya Wanawake hivyo tunyanyuke nazo pamoja tusiziache mpaka zinatupoteza kwenye ubora ndipo tunashtuka muda ni sasa wa kuendelea kuzipa sapoti.

Endapo kasi yetu itaongezeka ni rahisi kufikia malengo ambayo tumejiwekea hasa kwa kuvuka na kufika mbali tusisahau ushindani kila mahali ni mkubwa.

Huku ni tofauti na upande wa wanaume ambapo tayari tulikuwa nyuma wakati tunaanza kupambana hii inatokana na ukweli kwamba tulichelewa kustuka kwa wanaume ndio maana kwa sasa tunaannza kupata mwanga kidogo.

Hapo tulipo tuna kazi ya kuendeleza makali yetu kwa Wanawake ambao ndio wote wanaanza kunyanyuka kusonga mbele kuyafuta mafanikio nasi pia tusikae nyuma katika hili.

Tunachotakiwa ni kuendeleza pale ambapo tumeishia kwa kukazana kutafuta mafanikio kwa juhudi isiyo ya kawaida na mwisho wa siku nasi tutakuwa sehemu ya mafanikio.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic