September 29, 2020










Na Saleh Ally 
MAMA mzazi wa Luis Suarez aitwaye Sandra alikuwa ni mfagizi katika moja ya kituo cha mabasi katika kitongoji cha Tres Cruzes Jiji la Montevideo nchini Uruguay na hakuwahi kukata tamaa kuhusiana na mwanaye kwamba atakuja kuwa mtu mkubwa na maarufu siku moja duniani. 

Katika kitabu chake cha Luis Suarez, Crossing The Line, Suarez ameelezea namna Sandra alivyokuwa akihangaika na watoto wengi aliokuwa akiishi nao licha ya umasikini wake na kufanya asiwe na muda wa kumuuliza kuhusiana na shule hasa maendeleo yake. 


Pamoja na hivyo, ameeleza namna mama yake alivyoendelea kumpa moyo na kumuasa kuendelea kupambana kwa kile anachokiamini kwa kuwa hakupenda kumpangia. Baba yake mzazi, Rodolfo Suarez alikuwa ni mwanajeshi, baadaye akaamua kuondoka jeshini na maisha yakawa magumu zaidi hadi kufikia kuanza kujitafutia riziki kwa kufanya kazi katika kiwanda cha biskuti na baadaye kuamua kujihusisha na ujenzi. Kuna wakati Rodolfo hakuwa hata na fedha ya kujilipia kodi ya pango tu na kulazimika kulala katika eneo walilokuwa wakifanya ujenzi ili kujisitiri. 


Suarez anazungumzia namna umasikini ulivyowafanya wazazi wake washindwe kwenda kumuunga mkono wakati akienda mazoezini katika klabu ya watoto ya Nacional, moja ya klabu maarufu nchini Uruguay. Pamoja na hivyo, Suarez ameeleza anavyoendelea kuwashukuru wazazi wake kwani licha ya kutomuunga mkono kwa vitendo walikuwa wakimpa maneno ambayo yalimfanya aendelee kupambana bila ya kuchoka na mwisho anamtaja mkewe Sofi Balbi kuwa ndiye shujaa wake. Suarez na Sofi sasa wana watoto watatu, binti Delfina (alizaliwa 2010) na wavulana wawili, Benjamin (alizaliwa 2013) na Lauti, aliyezaliwa 2018. Walianza kuwa wapenzi Suarez akiwa na umri wa miaka 15 na Sofi akiwa na 13. 

Mshambuliaji huyo mtukutu sasa ana umri wa miaka 13 na chanzo cha mafanikio yake ya mpira ni Sofi na ndiyo maana anamuona ni shujaa wake lakini mji ulio katika historia ya maisha yake ni Barcelona. 

Huenda hapa inakuwa ni nafasi nzuri ya kujua kisa cha yeye kufikia kumwaga chozi wakati anaondoka katika klabu hiyo na kwenda kujiunga na Atletico Madrid ambao ni moja ya wapinzani wakubwa wa Barcelona kutoka katika Jiji la Madrid. Baada ya kocha mpya wa Barcelona, Ronald Koeman kuonekana hana mpango wa kumtumia au hana mpango naye, ikaelezwa atajiunga na Juventus ya Italia na kuungana na Cristiano Ronaldo. Akiwa katika hatua za mwisho, ikabainika kuwa alifanya udanganyifu wakati akitafuta uraia wa Italia ambao anao. Hivyo ikawa ni kesi ambayo mwisho ilionekana anastahili kubaki nao lakini kukawa na ugumu tena kujiunga na Juve. Ofa ya Atletico, mwisho imefanikiwa kama mchezaji huru lakini mwisho aliangua kilio kama mtoto akijua anaondoka Barcelona. 


Wengi wanaweza kudhani ni mapenzi pekee na klabu hiyo ambayo wana kauli mbiu yao “Zaidi ya Klabu”. Suarez lazima atakuwa anakumbuka maisha ya Barcelona ambayo alijiunga nao mwaka 2014 akitokea Liverpool na kufanikiwa kuichezea mechi 191 na kufunga mabao 147, hivyo kuandika rekodi ya kuwa mmoja wa washambulizi hatari zaidi waliowahi kuichezea Barcelona. 

Lazima ndani ya Barcelona kuna umoja, ukaribu na urafiki. Lakini aina ya mashabiki ambao Suarez atawakumbuka na mazoea kama mwanadamu wa kawaida, hivyo ni lazima kumwaga chozi. Yote sawa, lakini kama utabahatika kusoma kitabu chake hicho utagundua mapenzi yake na Barcelona hayakuanza wakati anakwenda kujiunga nayo lakini Barcelona imo ndani ya maisha yake kupitia Sofi. 


Suarez hakupenda shule, ukizingatia familia yake ilikuwa ni ya kimasikini sana, hawakuwa na muda wa kuifuatilia sana mienendo yake shuleni. Lakini Sofi alipinga mara zote na kumhimiza kusoma. Muda mwingi, Suarez alilazimika kuazima nauli asafiri zaidi ya kilomita 30 kwenda kumtembelea Sofi nyumbani kwao. Baadaye familia ya Sofi ilihamia Ulaya, ilihamia jijini Barcelona mwaka 2003 na huu ndio ulikuwa mwanzo wa Suarez kutamani kwenda kucheza barani Ulaya kwa kuwa alitaka tena kuungana na Sofi ambaye alimuona ndiye tegemeo katika kila kitu kwake. Mara moja, alialikwa Ulaya na Sofi na bado anavyokumbuka walivyoibia kwenda kupiga picha ndani ya Uwanja wa Camp Nou kwa kuwa hawakuwa na fedha za kulipia zoezi la kutembelea uwanja huo. Unaona namna maisha yalivyokuwa na baada ya kurejea Uruguay, aliamua kufanya juhudi kuu, akapambana hadi alipofanikiwa kusajiliwa na klabu ndogo ya Groningen ya nchini Uholanzi, hii ilikuwa ni mwaka 2006. 


 Suarez aliongeza juhudi akijua alistahili maisha bora kwa kuwa Ulaya ni mapambano zaidi na mara nyingi alitaka kumridhisha Sofi kwa kuwa alijua alivyompigania na yeye hakuwa na elimu wala hakuwahi kufaulu, hivyo alipambana akijua mkombozi ni mpira. Alifanikiwa kujiunga na Ajax mwaka 2007, mwaka 2011 akatua Liverpool na 2014 ikawa ni Barcelona lakini kumbuka mwaka 2013 alitaka kujiunga na Arsenal lakini Steven Gerrard wakati huo akiwa nahodha wa Liverpool, alimzuia na kumueleza acheze msimu mmoja akiwa Anfield na huenda akajiunga na Real Madrid, Bayern Munich au FC Barcelona na si Arsenal tena, na kweli msimu uliofuata, hilo likatokea. 


Unaona kiasi gani Mji wa Barcelona ulivyokuwa sehemu ya kumvuta Suarez kwenda Ulaya, kwa kuwa ulikuwa mji wake wa kwanza kukanyaga akiwa Ulaya lakini mapenzi yake na Barcelona, yalimfanya asichoke sababu alitamani siku moja ataichezea. Bila shaka ilikuwa ni klabu yake pendwa ambayo alifanikiwa kuifikia. Sofi, anabaki kuwa shujaa wake kwa kuwa unaona alivyoshiriki katika maisha yake wakiwa watoto kutoka katika familia zenye aina tofauti kabisa. Kwani baba mzazi wa Sofi alikuwa bosi wa benki na walihama baada ya benki kufungwa kutokana na anguko la kiuchumi mwanzoni mwa miaka ya 2000. 


Chozi la Suarez si kuondoka tu FC Barcelona, linajumuisha mengi na “undugu” wa historia ya maisha yake na Jiji la Barcelona, unamfanya akumbuke mengi aliyopitia akijua sasa anahamia katika jiji pinzani la jiji lake kipenzi, timu yake kipenzi lakini maisha, hayakupi nafasi ya kuchagua kila unachokitaka kama leo Suarez ni tajiri, maisha yake ni ya kifahari kwa kuwa mshahara wake kwa mwaka utakuwa zaidi ya pauni milioni 6 (zaidi ya Sh bilioni 17), lakini hana ujanja, lazima aondoke Barcelona kwa maana ya klabu na jiji pia.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic