April 11, 2021

 


Na Saleh Ally

NANI aliye nyuma ya wanaotaka kuandamana eti kwa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Yanga, Frederick Mwakalebela amefungiwa miaka mitano baada ya kupatikana na hatia ya kuzungumza maneno ya uchochezi.

 

Kamati na Maadili ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ilitangaza kumfungia Mwakalebela kwa miaka mitano na faini ya jumla ya Sh milioni tano kutokana na makosa mawili.

 

Kwanza ni uchochezi kwa mashabiki wa Klabu ya Yanga dhidi ya vyombo vinavyosimamia akidai vinaihujumu Yanga, alivyoitwa katika kamati hiyo ya maadili alishindwa kuthibitisha.

 

Kosa la pili ni kusema alikuwa na mkataba baina ya Bernard Morrison na Simba na aliuonyesha mbele ya waandishi wa habari lakini Kamati ya Maadili imeeleza kwamba alishindwa kuuonyesha kwao mkataba huo na kuthibitisha kile alichokizungumza mbele ya waandishi wa habari.

 

Adhabu alizopewa Mwakalebela zimeelezwa kwa mujibu wa vifungu vya 73 (4) cha Kanuni ya Maadili na 6 (1) (b) na 6 (1) (c) cha Kanuni ya Maadili pia.

 

Wakati Mwakalebela akiwa ameanza kutumikia adhabu hiyo, kumeibuka hoja kadha wa kadha kuhusiana na adhabu hiyo na wako wamekuwa wakiishambulia TFF katika hili.

 

Inawezekana ni kutuelewa mambo na hili limekuwa likiendelea kwa kuwa TFF ina kamati ambazo ni huru na zina uwezo hata wa kumfungia kiongozi wa shirikisho hilo. Wanaoamua si wafanyakazi wa TFF badala yake wadau mbalimbali wanaokuwa wameteuliwa kuendesha kamati hizo.

 

Mwakalebela angeweza kuthibitisha alihojiwa maana yake kusingekuwa na udhia huo. Kilichotokea imeonekana hana huo mkataba wa Morrison kama alivyosema na kashindwa kuthibitisha kwamba TFF na Bodi ya Ligi Tanzania (TPLB), zinaihujumu Yanga na adhabu ikafuatia.

 

Nianze na kusema bila ya ubishi, kama ilivyoeleza kamati ya maadili, kama Mwakalebela alishindwa kuthibitisha aliyoyasema, anastahili adhabu kabisa.

 

Lazima kuwe na weledi katika uzungumzaji, viongozi wapunguze mihemko katika mambo ya msingi na wanapaswa kuwa na staha kuepusha kusababisha athari na chuki ndani ya mchezo wa soka.

 

Viongozi wengi hasa wa klabu hizi kubwa, wana tabia wanakosea halafu baada ya hapo wanatafuta kisingizio kwa kuwaangushia mpira TFF au wadau wengine na silaha yao imekuwa mashabiki, hili limekuwa kawaida.

 

Pili, pamoja na kuwaadhibu, bado ninasisitiza kwamba adhabu ziwe zile ambazo zinawafanya watu wajifunze na kurejea kufanya yaliyo sahihi. Adhabu ya miaka mitano inakuwa ni sawa na kumfungia mtu kifungo cha maisha. Miaka mitano ni mingi sana na adhabu inakuwa ni kama ya kukomoana.

 

Hata adhabu ya fedha, nayo ni kubwa sana. Bado inawezekana ikawa chini ya hapo na bado ikawa fundisho kwa mhusika lakini isiwe kama ndiyo itakuwa adhabu ya mwisho kutolewa. Hivyo kuna kila sababu ya kuzipitia hizo kanuni mbili na nyingine za Kamati ya Maadili maana zinakuwa zinaumiza na kukomoa badala ya kuumiza na kubadilisha.

 

Mwisho ni mashabiki hasa wale baadhi ambao wameingia na mihemko bila ya kuingia ndani ya mistari ya usahihi kuangalia kipi sahihi ambacho kinaweza kufanyika.

 

Kuandamana ili iweje? Mwakalebela kashindwa kuthibitisha kwenye kamati, kuandamama ili iweje wakati Mwakalebela kapatikana na hatia. Acheni hoja dhaifu eti alizungumza kwa niaba ya klabu, sote tunajua kanuni inambana muhusika au aliyezungumza bila ya kujali ni kwa niaba ya klabu au yeye mwenyewe na washkaji zake.

 

Hivyo kuwe na namna ya kuheshimu mamlaka na kuepuka kujiona wakubwa sana wakati sivyo. Ukishakuwa na kundi lako, basi unaona hakuna kama nyie na mnaweza kusema lolote, si sahihi hata kidogo.

 

Nyongeza, si kila jambo likiwatokea Yanga lazima wafananishe na Simba au ikumbushiwe Simba. Alichokosea, alichoadhibiwa vinaweza kuwa mjadala bora ambao ukatoa funzo badala ya kuingiza yasiyohusika.

 

Adhabu hizi ni msumeno, zinakata huku na kule. Lakini lazima tukubali kuzipitia na mwisho kufikia ule mwafaka unaokuwa ni kuadhibu kwa ajili ya kurekebisha na kutengeneza ubora sahihi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic