July 24, 2021


 WAKATI umewadia na muda umebaki

mchache sana kabla ya watani wa jadi

kuvaana kwenye Uwanja wa Lake

Tanganyika mjini Kigoma.


Historia inakwenda kuandikwa kwa uwanja

huo kuwakutanisha watani wa jadi Yanga na

Simba katika mechi muhimu ya fainali ya

Kombe la Shirikisho.


Fainali ambayo imo katika rekodi ya

kuwakutanisha watani wa jadi kucheza


mechi mbili ndani ya mwezi mmoja na hapo

hakuna mechi ya kirafiki.


Mwezi huu wa Julai, tayari Yanga

wamemfunga Simba kwa bao 1-0 katika

mechi ya Ligi Kuu Bara ambayo iliihakikishia

Yanga kusimama katika nafasi ya pili ya ligi

hiyo lakini ikaizuia Simba kuchukua ubingwa

mapema, mikononi mwa watani wake

Yanga.


Hii ni mechi ya pili, mechi ambayo Yanga

wanalitaka Kombe la shirikisho, wanataka

kumvua Simba ubingwa na kuthibitisha

ushindi wao katika mechi iliyopita wala

haukuwa wa kubahatisha.


Kwa upande wa Simba, wanataka kutetea

ubingwa wao, wanataka kulipa kisasi na

tatu kuonyesha Yanga waliwaotea katika

mchezo ule ambao wengi hawakutarajia

kuona Simba wanapoteza.


Wakati hayo yanakwenda kutokea na

matokeo tukisubiri dakika 90 za mchezo

huo, niwakumbushe waamuzi kwamba

mwamuzi wa mchezo uliopita Emmanuel

Mwanembwa alileta shida kubwa ambayo

imeacha malalamiko.


Shida hiyo ilikuwa wazi na ilionekana ni

kama mwamuzi alipanga kumaliza mchezo


huo bila ya kutoa penalti au kutoa kadi

nyekundu hata kama ilitakiwa.


Tuliona rafu kadhaa ambazo wakati

mwingine tungeweza kusema zilistahili kadi

nyekundu kabisa. Lakini mwamuzi hakutoa

hata kadi ya njano ikionekana wazi alipania

kuubalansi mchezo.


Kulikuwa na penalti, kila mmoja aliona lakini

mwamuzi hakutoa pigo la penalti na hii ni

ile sehemu ya kuonyesha kwamba

kunakuwa na mwenendo au mwelekeo wa

kisiasa unaotokana na ukubwa wa mechi ya

Yanga na Simba, waamuzi hawapaswi

kuingia huku.


Kama ni kadi, basi mtu ale kadi na kama ni

penalti basi mara moja itolewe kwa mujibu

wa sheria 17 za mchezo wa soka. Lakini

haikuwa hivyo ndio maana nimeamua

kumkumbusha mwamuzi Ahmed Arajiga na

wenzake kwamba mechi wanayokwenda

kuchezesha ni dhamana kubwa na ndio

inabeba thamani yote ya michuano ya

Kombe la Shirikisho ambayo Azam Media

wamewekeza mamilioni ya fedha. Wengine

wamewekeza kwenye timu na zimetoa ajira

kwa wachezaji maelfu.


Waamuzi walioteuliwa kwa ajili ya kucheza

mchezo huo ni pamoja na Ahmed Arajiga

(Manyara) ambaye atasaidiwa na Ferdnand

Chacha (Mwanza) na Mohammed Mkono


(Tanga) wakati mwamuzi wa akiba atakuwa

ni Elly Sasii wa Dar es Salaam.


Si jambo zuri mtu kufanya uzembe tena kwa

zile siasa za kuhofia au kutaka

kuwafurahisha baadhi. Au kutaka

kutoonekana haukuwa mkatili au

haukuboronga na hapa unakuwa

umezikanyaga sheria 17 za mchezo wa soka

na mwisho lawama kama ilivyo ada

zinaangushiwa kwa Shirikisho la Soka

Tanzania (TFF), jambo ambalo si sahihi.


Waamuzi wawe imara na wakumbuke kama

watafuata weledi wa kazi yao na uamuzi

wao uwanjani ukawa ni ule ambao ni sahihi.


Basi hakuna kitakachoweza kuwaangusha

au kuwafanya waonekane walikosea hata

kama itakuwa ni baada ya miaka 100 ijayo.


Ukweli haupingiki, ukweli haushindwi milele

na vizuri kufanya sahihi na kuacha kuwe na

malumbano na kadhalika, lakini mwisho

hakuna anayeweza kukushinda.


Bila shaka, hii imekuwa ni tabia kwa muda

mrefu kwamba waamuzi wanaingia

uwanjani kuchezesha mechi ya watani

wakiwa wanataka kuhakikisha inaisha bila

kadi nyekundu au kutoa penalti. Wako

waamuzi hufurahia hata mechi iishe kwa


sare kwa kisingizio cha kupunguza

“makelele”.


Suala la “makele” si kazi yao, nani

atachukizwa au nani ataumizwa kwa

kupoteza au yupi atafurahi kwa kushinda,

waamuzi waitoe kabisa hiyo badala yake

waende kuchezesha mpira tu na suala la

matokeo, litokane na mchezo

utakavyokuwa.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic