Usiku wa kuamkia leo (Jumatano) ulikuwa
ni siku ya kudhalilika kwa wakali wa pasi Barcelona baada ya kuchapwa kwa mabao
3-0 wakiwa nyumbani Camp Nou.
Barcelona walikutana na kipigo cha mabao
hayo kutoka kwa Real Madrid ikiwa ni mechi ya pili ya nusu fainali ya Kombe la
Mfalme maarufu kama Copa de Rey.
Katika mechi ya kwanza mjini Madrid,
wageni Barcelona walikomaa na kufanikiwa kupata sare ya bao 1-1, hivyo wengi
wakategemea wakirejea nyumbani Camp Nou, wageni Madrid watakiona.
Hata hivyo, mambo hayakuwa hivyo, kwani Madrid
ndiyo walionekana ni tatizo kubwa kwa wenyeji wao huku wakikosa mabao mengi.
Lionel Messi ndiye alionekana kuwa
tatizo kubwa awali, lakini baadaye akapotezwa huku mpinzani wake mkubwa
Cristiano Ronaldo aking’ara kwa kupachika mabao mawili.
Ronaldo alipachika bao la kwanza katika
dakika ya 13 na la pili 57 kabla ya Varane kufunga la tatu kwa kichwa katika
dakika ya 68. Kabla ya Jordi Alba kuipatia Barcelona la kufutia machozi katika
dakika ya 89.
Pamoja na kupata mabao hayo matatu,
Madrid waliendelea kutawala mchezo katika dakika za mwisho huku wakionyesha
walipania kuwatia ‘njaa’ zaidi wapinzani wao hao wakubwa.
Muda mwingi, Messi alionekana kama
amekwenda likizo huku Ronaldo akiendelea kuwa tishio na kuisumbua ngome ya
Barcelona kwa kushirikiana Mesut Ozil na Di Maria.
Mourinho ambaye haishi vituko, dakika za
mwisho za mchezo huo aliamua kuondoka kwenye benchi na kuingia vyumbani hali iliyoonyesha
kumdharau Kocha Msaidizi wa Barcelona, Jordi Roura.
Madrid walitua jijini Barcelona siku ya
mechi ukiwa ni mfumo mpya na walitegemea kuondoka leo asubuhi kurejea jijini Madrid.
Timu hizo zinakutana tena Jumamosi hii
katika mechi ya La Liga itakayopigwa kwenye Uwanja wa Bernabeu jijini Madrid. Huenda
Barca wakalipa kisasi au wenyeji kuendeleza ubabe.
0 COMMENTS:
Post a Comment