March 6, 2013


Na Saleh Ally
NILIKUTANA na shabiki mmoja wa soka, hakutaka kunieleza anashabikia timu ipi ya soka hapa nyumbani zaidi ya kusema yeye ni Arsenal damu pamoja na kwamba kikosi cha Arsene Wenger kimekuwa hakieleweki, leo raha, siku mbili zinazofuata ni karaha tu.

Pamoja na kuzungumza naye mambo yote, muungwana huyo mpenda soka aliniuliza kama sina hofu na bastola inayomilikiwa na Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage ambaye nimekuwa nikimkosoa mara kadhaa kuhusiana na uongozi wake.


Nilipomuuliza amejuaje kama Rage anamiliki kifaa hicho, akanikumbusha ile kesi ya ubunge baada ya Rage kupanda na ‘cha moto’ jukwaani, hali iliyosababisha matatizo kwa Chama cha Mapinduzi (CCM). Kweli nikakumbuka.
Lakini kwa kuwa si mtu wa siasa, nikamueleza tuachane nayo na kumsisitizia: “Bastola yake haituhusu, wala haiwezi kunipa hofu ya kusema ninachoona ni bora kwa soka ya Tanzania, ukweli ndiyo kila kitu.”

Leo nimerudi tena, naendelea na nilichokianza miezi kibao iliyopita kuhusiana uendeshaji wa Rage, najua wengi wamekuwa wakiniona mkorofi, lakini naamini kama ni gari, limeshakata breki kwa kuwa nina kila sababu ya kufanya hivyo.
Rage ameshindwa kuongoza, inaonekana wazi leo. inawezekana hata mliokuwa mkiniona ninamsakama tu labda kwa sababu zangu binafsi, mnaanza kuelewa. Naamini mtanielewa zaidi kadiri siku zinavyosonga, kikubwa tuombe uzima.

Nani asiyejua Simba ilikuwa katika mwendo mzuri sana? Lakini kila kitu kinakwenda mrama na aibu ndiyo imekuwa zawadi ya Simba kila jua linapochomoza.
Ushirikiano:

Chini ya uongozi wa Rage, hakuna ushirikiano ndani ya klabu hiyo kuanzia kwa viongozi na wachezaji, wachezaji wenyewe kwa wenyewe na hata makocha na vijana. Hakika mambo si mazuri, hali inayoashiria moja kwa moja kuwa mambo yamekushinda na inaonekana hutayaweza tena.

Simba haigombanii chochote bora tena, kila kukicha inawania nafuu, haina tena uhakika wa kuchukua ubingwa ambao kiaina imewaachia Yanga na Azam FC. Nafasi ya pili, huenda ikawa tatizo pia kama mwenendo ndiyo huo.

Yanga walikumbana na ‘aibu’ ya kuwa wa tatu, uongozi wako unaitengeneza msimu huu kwa Simba. Hatari zaidi, Simba inaweza ikadondokea hata nafasi ya nne kwa kuwa klabu ina kikosi kisichokuwa na ushirikiano, maana yake hakina sifa ya kuitwa timu na matatizo yote siku ya mwisho yatakuwa ya uongozi wa juu.

Msimu uliopita, safi kwenu na mlistahili pongezi. Msimu huu mmeboronga, ingawa Rage unanishangaza, maana bado unaona unastahili pongezi!

Siasa:
Inaonekana wazi Rage umebanwa, kuna mambo mengi yanatokea ndani ya klabu hiyo bila wewe kujua. Shughuli za kisiasa zinakubana. Wakati Simba ikiwa inaendelea kuyumba, mzee wangu wewe ulionekana ukigombea bendera na kijana mbichi wa Chadema. Katika hilo huna makosa, lakini jiulize ulikuwa ni wakati wa kuiacha Simba?

Kocha:
Hivi karibuni ulisikika ukimuangushia mzigo kocha Milovan Cirkovic ambaye mlimtimua, mkashindwa kumlipa hadi msaada wa Malkia wa Nyuki ndiyo ukaokoa jahazi. Pamoja na kusema Mserbia huyo ni tatizo, leo Simba ina Mfaransa, mambo ndiyo mabaya zaidi.

Katika hali ya kawaida, haingii akilini kama kweli Simba ilifanya kitu cha msingi mbele ya uongozi wa Rage. Katika hili wanachama na mashabiki wa Simba wameonyesha kuchukizwa, ndiyo, wana haki kwa kuwa wanachotaka ni matokeo mazuri.

Kama Milovan aliondoka, alikuwa na matatizo, basi aliyekuja alitakiwa kuleta matokeo mazuri kuliko yeye. Sasa Simba inadidimia kuelekea nafasi ya nne, kitu ambacho mwisho wa ligi kinaweza kusababisha aibu kubwa kama mwenendo ndiyo huo.

Kujiuzulu:
Nani kasema ni dhambi? Nani kasema kufanya hivyo ni aibu kubwa? Sasa vipi Rage mbona hautaki kuiokoa Simba kama unaipenda kweli? Kuwa muungwana, jiuzulu. Mambo mengi yanaonekana kukwama kwa kuwa wewe na uongozi wako, mmeshindwa.
Utapinga vipi hamjashindwa? Timu haifanyi vizuri, madeni lukuki kupindukia na wachezaji hawajalipwa fedha zao za usajili, wanacheleweshewa mishahara. Angalia hivi karibuni, basi la Simba lilizuiliwa na mwenye hoteli, kisa madeni. Hizo zote ni aibu!
Kukimbia:
Sema hautaki kunisikia tu mzee wangu, hivi karibuni ulifanya kitu kibaya sana. Ulionyesha wazi ulivyo mjanja kutetea maisha yako kuliko kuungana na vijana wako na kama ni kuzama baharini, basi mzame pamoja.
Unajulikana kuwa unaipenda Simba, wewe unaipenda Simba ipi? Labda kama ipo nyingine, maana siku inafungwa na Libolo, wewe ukaikimbia na kuondoka zako. Tena vibaya zaidi ukawakimbia hadi wageni mawaziri na wabunge uliokuwa umewaalika. Hakika wewe una roho ngumu...eeh!

Najua Kiswahili kina maneno mengi sana, kila mmoja ana ujuzi wa kuyapanga kivyake mdomoni, wewe ni mwanasiasa, lazima utakuwa fundi. Lakini mambo mengi yanakubana, yanaonyesha umefeli, sasa umefika wakati maneno yako hayafanyi kazi tena. Chukua uamuzi wa busara.

Ahadi:
Nilishakuchambulia ahadi kibao ulizowahi kuahidi ambazo hujatekeleza, moja ni ile ya uwanja ambayo uliwaonyesha Wanasimba mchoro. Hadi leo imekuwa ni ahadi isiyotekelezeka na wewe umekuwa mkali kweli kuhusiana na hilo.

Unajua mengi uliyoahidi ambayo hayajatekelezeka, ushauri wangu ni huo. Simba ‘unaipenda’ , ninaamini hata yenyewe inakupenda. Lakini kupendana kunaisha, ni sehemu ya maisha. Unaweza kubaki kama mmoja wa wazee wa klabu na kuendelea kushauri, pumzika ‘mwayego’ Rage.

Ninaamini wanaosema ninakushambulia au kama unafikiri hivyo basi unakosea sana. Huenda kwa mara nyingine nimekukumbusha kwa upole sana. Unaonyesha umeshindwa, nafsi yako itakueleza ukweli. Basi unaweza kuonyesha unaipenda Simba kwa kuwapa nafasi wengine, kung’ang’ania hakutakusaidia lolote, badala yake utaendelea kuiumiza Simba ‘yako’.

SOURCE: CHAMPIONI NEWSPAPER

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic