April 8, 2013




Nimesikia uongozi wa Simba kuwa unataka upongezwe kutokana na masuala ya kadhaa, moja wapo ni kumuuza kiungo wake mshambuliaji, Emmanuel Okwi raia wa Uganda kwa klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia.

Uongozi huo wa Simba ambao unachukia sana kukosolewa, umeeleza mambo kadhaa uliyoyafanya kama kupandisha kipato cha Simba lakini pia ‘kumuuza’ Okwi kwa kitita cha dola 300,000 (zaidi ya Sh milioni 450).

Fedha ni nyingi na kama ingekuwa ni suala la maandishi ya kwenye makaratasi pekee yanaweza kuonekana ni fedha halisi, basi hilo lingewezekana. Lakini ukweli walichokifanya Simba ni kitu cha kushangaza.

Kama watakuwa wanahitaji pongezi, basi wanalazimika kusubiri hadi malipo ya fedha zote za mauzo yatakapoingia katika akaunti yao. La sivyo wanastahili lawama kwa kuwa watu wasio makini na wenye kukurupuka kwa kuwa biashara ya Okwi ni biashara kichaa.

Nasema biashara kichaa kwa kuwa Simba imeharakisha kumuuza Okwi kama vile ilikuwa na mipango madhubuti, inaonekana faida ya fedha imekwenda kwa mchezaji mwenyewe au na mtu mwingine yoyote ambaye huenda ‘amepozwa’.


Lakini klabu kama Simba, haijafaidika jambo lolote hadi sasa zaidi ya kuendelea kuathirika katika mambo kadhaa ya msingi, mojawapo likiwa ni kumkosa mchezaji huyo katika mechi nyingi za ligi.

Angalia Simba katika kipindi hiki inavyosota katika kila njia, haina fedha, wachezaji wake wamekuwa wakilipwa kwa mafungu na mambo si mazuri ingawa uongozi umekuwa ukijitahidi kuficha mambo kwa kuyafunika kwa kisingizio eti unasakamwa.

Leo uongozi huo unataka upongezwe kwa madudu lukuki uliyofanya, uongozi unajisifia hata katika suala la Okwi ambalo dhahiri linaonekana ni kama kichekesho kwa kuwa Simba imefanya biashara ya hisia bila ya kuingiza chochote.

Siku chache kabla ya kumuuza Okwi ‘bure’, Simba ilikuwa imengia mkataba na mchezaji huo na kumwaga zaidi ya Sh milioni 40. Halafu yenyewe ikaamua kwenda kumuacha Tunisia bila ya kupata fedha hata chembe zaidi ya ahadi. Hii ni aina gani ya biashara? 

Lakini kama haitoshi, Simba inataka isifiwe kwa kuongeza kipato cha klabu hiyo, lakini aibu za timu kuingia katika madeni makubwa yanayopelekea aibu zimekuwa zikizidi.
Basi la Simba kuzuiwa Arusha kutokana na deni la Sh milioni 15, kuna kiongozi anapinga hata bila ya haya, lakini hiyo ndiyo hali halisi. Achana na hivyo, wachezaji wa Simba kuzuiwa dakika chache katika hoteli kabla ya kwenda uwanjani kuivaa Coastal Union.

Sasa kipato kama kimekua na sasa Simba inaingiza fedha nyingi ukilinganisha na ilivyokuwa kabla ya kuingia uongozi wa sasa, kwa nini madudu kama hayo hayaishi? Lakini uongozi wala hauoni, unataka pongezi!

Uongozi unajua kama umeshindwa kuingoza timu yake katika mwenendo mzuri, ndiyo maana mambo mengi sana yamevurugika.

Benchi la ufundi, wachezaji wakongwe ni matatizo matupu na leo wako wachezaji wanaolipwa mamilioni ya fedha, hawana faida na timu.

Nasema hawana faida kwa kuwa hawachezi na sababu za msingi kuwazuia wasicheze hazipo, ukiulizwa utaambiwa fulani alimuudhi kocha! Wao ni binadamu, maudhi hayakosekani, yakitokea lakini kuna njia ya maana kuyashughulikia na kikubwa ni wao kuitumikia Simba. 

Lakini haifanyiki na uongozi kwa kuwa si imara unashindwa kulishughulikia suala hilo, mwisho inatumika short cut ambayo ni kuwafungia halafu inabaki kwa Simba kwa kuwa inaendelea kutoa mshahara wa bure wakati mchezaji hapotezi chochote.

Mwisho wa msimu mchezaji ataondoka zake na kujiunga na timu nyingine, Simba itakuwa imemaliza msimu kwa aibu. Ukiangalia, hesabu bora zingekuwa ni kufanya mazungumzo ya pamoja kwanza ili kukubaliana kuhusiana na tofauti zilizopo.

Baada ya hapo wachezaji hao wangecheza kwa moyo mmoja na kuisaidia klabu, mwisho wa msimu bado uongozi ungeweza kuwaita na kujadili upya masuala kadhaa na kujua kama inaweza kuendelea nao au la.

Lakini uongozi wa Simba, hauna ‘akili’ hiyo ambayo zaidi inalenga kuisaidia timu na pia kuwasaidia wachezaji kung’amua matatizo yao. Mwisho uongozi unalazimika kulaumu kwa kuwa unakosolewa.

Unashindwa kuwa na hoja za msingi kwa kuwa unaona umeharibu na kukubali kwamba wenyewe ni chanzo ni kama ‘dhambi’ kubwa.

Haya ni machache, yako mengi ambayo uongozi unapaswa kuangalia kwa maana ya kujifunza, kujirekebisha na ikiwezekana kukubali kukosolewa. Cha kuwapongeza kinaweza kuonekana kwa darubini kwa kuwa kinafichwa na madudu lukuki. Najua mme-miss kupongezwa, haya basi Hongera uongozi wa Simba.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic