April 22, 2013



Klabu ya Simba ni kati ya zile zilizopoteza kabisa mwelekeo msimu huu, shahidi wa kwanza katika hili utakuwa ni uongozi wa klabu hiyo.
Nasisitiza hili, kwamba uongozi wa Simba unapokosolewa hujenga makusudi hisia za kuonewa au kuhujumiwa, lakini hali halisi iko hivi, uongozi huo unajihujumu wenyewe kwa kuwa umejaza watu wengi wanaoangalia maslahi yao wenyewe.

Mwenyekiti wake, Ismail Aden Rage anajua kama amepoteza mwelekeo, lakini amekuwa akilalama kuhujumiwa na kwa kuwa ni muoga wa kujibu hoja zinazoelekezwa kwake, ndiyo maana anajenga mazingira ya vitisho na uzio wa kutaka asielezwe, labda si Metodo, sitaacha kumueleza ukweli na vitisho si kitu cha kunirudisha nyuma. 


Simba imepoteza mwelekeo katika kila kitu, ukianzia kwa uongozi hakuna ushirikiano wala kuaminiana. Ukirudi katika kikosi chenyewe ndiye kabisa, amani na upendo vimetoweka na kila mmoja anakwenda njia yake.

Marubani ambao ni Rage na viongozi wenzake wameishapoteza mwelekeo, hawawezi tena kukirudisha ‘chombo’ katika nia yake sahihi, ndiyo maana hakuna upendo na amani ndani ya timu na klabu kwa ujumla.

Mwanasimba yupi anaweza kusema anafuraha katika kipindi hiki, anzia mashabiki, wachezaji hata benchi lote la ufundi.

Simba imeamua jambo moja, kwamba badala ya kuwatumia wachezaji wakongwe ambao wanadai wana matatizo, wamewachukua vijana na kuwapandisha, wameamua kuwaamini ili wapambane. Ni jambo zuri sana.

Lakini bado tatizo linaendelea kubaki palepale kutokana na uongozi kutokuwa makini na kufanya mambo mengi kwa mfumo wa kubabaisha na wanapokosolewa au kukumbushwa wanalia eti wanahujumiwa, upuuzi!

Vijana ambao Simba wameamua kuwaamini nao wamekuwa wakilia kuhusiana na maslahi yao, kwangu naona ni kitu cha ajabu sana kusikia vijana hao wanadai mishahara yao ya miezi kadhaa na hawajalipwa.

Nashangaa zaidi kusikia hata mikataba waliyotaka kuwasainisha waliwaomba ‘wawakope’, kwamba walitoa ahadi ya fedha watakayowapa, halafu baada ya hapo watawalipa siku nyingine baada ya kusaini! Si kitu kizuri.

Pia si sahihi kuwaona vijana hao kama wana shida sana, au ni wale wanaoibembeleza Simba kwa kuwa hawana pa kwenda. Hadi leo wanacheza bila ya kuwa na mikataba na timu hiyo. 

Kuna macho ya wengi, wanaiona kazi yao. Siku kijana ataamua kuondoka na kufuata suala la maslahi, halafu uongozi uanze kutangaza ni msaliti kama ilivyokuwa kwa Kelvin Yondani ambaye alitafutiwa uadui wakati tatizo kubwa lilikuwa kwa uongozi wa Simba.

Vijana kweli wanachipukia, lakini wanapaswa kupewa motisha, kulipwa mishahara mizuri nikiwa na maana wapewe mikataba bora ambayo itawafanya wajitolee zaidi na si kupewa maneno na ahadi nyingi na yule anayefunguka na kuhoji anaonekana mbaya.

Morali haipatikani sehemu yenye njaa, wote tunalijua hili. Sasa si sahihi fedha zinaoingia ndani ya Simba kupitia vyanzo kama wadhamini, fedha za milangoni na malipo ya pango la majengo ya Simba, kuingia kwenye mifuko ya wachache ambao wanajidai eti wanaipenda zaidi klabu hiyo, halafu wanaotoka jasho zaidi ndiyo wanaumia.

Kuwachukulia vijana kama watoto wa shule ni kosa, ndiyo maana mnawapa nafasi ya ya kupambana na timu nyingine mkiamini wanaweza kufanya vizuri. Basi walipeni vizuri ili waifanye kazi yenu katika kiwango cha juu.

Nawakumbusha vijana hao si ‘maroboti’, wana akili zao timamu na wana malengo yao ndiyo maana wamefikia walipo. Tambueni wanajua wakifanyacho hivyo fanyeni nao kazi kwa kufuata utaratibu mkiamini wanajitambua.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic