May 14, 2013




Karibu kila kukicha kumekuwa na vita kubwa inayohusiana na makato ya mapato katika viwanja vya soka katika mechi za Ligi Kuu ya Tanzania Bara.

Malalamiko hayo yanatokana na namna timu ambavyo zimekuwa zikikatwa fedha huku wadau wengine wakifaidika wakati hawatoi fedha nyingi kujiandaa na mchezo kama inavyokuwa kwa timu.

 Vita hiyo imekuwa ikipamba moto ingawa naweza kusema wadau kadhaa kuanzia katika vyombo vya habari hadi ndani ya klabu zenyewe wamekuwa ni waoga kupambana zaidi.

Hawasimami na kuzisaidia klabu, inawezekana ni uoga wa nafsi au kuamini hawana haja ya kupiga kelele kwa kuwa hawafaidiki. Lakini ndani ya klabu hizo, kukaa kimya kwa viongozi, huenda wanaona hawana sababu ya kuhangaika kwa kuwa wanapata ‘kitu’ kupitia mlango wa nyuma.

Kelele za wachache ambao tuliamini tunaweza kusaidia, zilichangia kusaidia serikali kuamka na kutangaza kupunguza makato kadhaa kama yale ya uwanja ambayo mengi yalikuwa yanajirudia na kuwafaidisha wengine.


Mimi naanzisha vita nyingine, lengo ni kusaidia kupatikana kwa mabadiliko angalau kama yale yaliyotokana na kupunguzwa kwa makato.
Ukiangalia makato ya kila mchezo wa Ligi Kuu Bara, utaona kuna makato yanayokwenda kwenye Mfuko wa Maendeleo ya Soka au Football Development Fund (FDF).

FDF inahusika na maendeleo ya soka, lakini bado sijawahi kusikia kwa mwaka wameingiza shilingi ngapi na zimetumika namna gani zaidi ya kupata ufafanuzi kidogo kutoka TFF kwamba fedha hizo zinatumiwa na timu za vijana.

Nimeelezwa kutoka TFF kwamba fedha hizo wala hazitoshi kwa na shirikisho hilo limekuwa likilazimika kufanya juhudi kutafuta kwingine ili kuzisaidia timu hizo. Kweli hilo linawezekana, nakubaliana nao.

Lakini hofu yangu ni moja, TFF inachukua fedha hizo na mimi narudi kwenye hoja yangu ya kwanza ya mapato nilioyoianzisha. Kwamba inachukua fedha zaidi ya mara moja, yaani inachukua asilimia kadhaa za mapato kama shirikisho na baadaye kupitia FDF.

Lakini kitu cha ajabu, sijawahi kusikia fedha za FDF zikitajwa kwamba zilitumika hivi au vile, au zilisaidia kiasi gani. Imekuwa kimya tu na fedha hizo za makato kwenda FDF zimekuwa kama vile mto unaoingia baharini.

Lazima tukubaliane, fedha hizo ni za umma. TFF wanapaswa kuwa wazi na kutueleza zinatumikaje, zimekupungua kiasi gani na wanahitaji nyongeza ya kiasi gani huenda ikawasaidia hata wadhamini kujua kama wanahitaji nini.
Haiwezekani fedha zinazotokana na makato ya mapato ya klabu tuambiwe zimeingia kuendeleza soka, lakini hatujui zinaendeleza soka vipi zaidi ya kusikia juujuu tu, eti hutumika katika timu za vijana.

Mara kadhaa, nilitafuta kutaka kujua anaouendesha mfuko huo, nilidhani serikali. Lakini kama ni TFF, ukimya wao kutouzungumzia mfuko huo hata siku moja Napata hisia za ufujaji na kuna kila sababu ya wao kuwa wazi na kutueleza.
Fedha hizo zinakatwa hadharani, kwenye taarifa zake kwa vyombo vya habari TFF inaelezea makato hayo. Ndiyo maana naona nna haki ya kuhoji, matumizi yake ni vipi lakini angalau msimu huu waliingiza kiasi fani katika mfuko huo.

Mara kadhaa nimesikia TFF ikisema wana upungufu katika fedha kwa ajili ya kuzihudumia timu za vijana. Huwa ni Sh ngapi na fedha za FDF huchangia kwa kiasi gani?
Klabu na viongozi wake zimekaa kimya, hazitaki kuhoji wala hazina haja ya kujua kama ilivyo kawaida yao, lakini ninaamini wako wenye kiu ya kutaka kujua kama ilivyo kwangu. Hivyo TFF lazima ijue fedha hizo ni za umma na wadau wana haki ya kujua, basi watueleze.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic