July 17, 2013


MASATU (WA PILI KULIA WALIOSIMAMA) WAKATI AKIICHEZEA PMSSB YA INDONESIA

 Na Saleh Ally
Kati ya mabeki waliowahi kucheza soka nchini na majina yao hayapotea midomoni mwa mashabiki wa soka ni George Magere Masatu.

Masatu alikuwa na sifa nyingi sana, lakini utambulisho wake lilikuwa ni umbo lake dogo lakini uwezo mkubwa ulifunika kila kitu na kupingana na mfumo wa soka unaoagiza beki wa kati lazima awe na umbo kubwa ili kucheza vizuri.

Masatu alianza kupata jina kubwa wakati akiwa katika kikosi cha Pamba ya Mwanza kilichotikisa soka nchini, lakini baadaye akaendeleza makali yake akiwa na Simba.

Baada ya kucheza soka nchini baadaye Uarabuni, Masatu aliondoka nchini na kwenda Indonesia ambako alicheza soka kwa zaidi ya miaka mitano kabla ya kustaafu na baadaye akapata kazi katika shule ya watoto iliyo chini ya klabu maarufu ya England ya Arsenal ambako alifanya kazi kwa miaka mitatu na ushee.

Masatu anasema sasa amerejea nyumbani Tanzania baada ya kuishi Indonesia kwa zaidi ya miaka nane na atafanya nini?

“Kuna mambo mengi sana ya kufanya, lakini tunaweza kuzungumza kwanza masuala ya soka na baadaye, nitawaeleza mambo yatakavyokuwa na kipi ambacho nimepanga kukifanya,” anasema Masatu katika mahojiano yake ya kwanza na gazeti la Championi ikiwa ni siku moja tu baada ya kutua nchini.

Kuna mambo mengi sana kuhusiana na Simba, lakini umbo lake na namna alivyoweza kucheza na kuwa beki bora lakini pia kuhusiana na fainali ya Kombe la Caf, mwaka 2003 kwa kuwa Masatu alikuwa kati ya wachezaji walioelezwa kuhusika na hujuma.


Lakini Masatu anaanza kuelezea kwa ufupi kuhusiana na maisha yake wakati akiwa Simba na hadi alivyoondoka, mara ya mwisho aliingia katika mgogoro na kufikia hata kutaka kumpiga kiongozi mmoja wa Simba.

“Simba ndiyo ninayoipenda, nimecheza pale kwa moyo mmoja ingawa mpira wa Tanzania kipindi kile ulikuwa na mambo mengi sana ambayo unaweza ukashangaa hata kama ukiambiwa unaweza kukataa.

“Simba ni timu kubwa, lakini ilifikia wakati tunasafiri kwa roli lakini wachezaji walicheza bado kwa moyo na kutaka kushinda. Nakumbuka miaka michache kabla sijaondoka Simba tulisafiri na basi kwenda Lindi.

“Ilikuwa ni mechi ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Kariakoo Lindi. Tukiwa njiani basi liliharibika mara kadhaa, ulikuwa usumbufu mkubwa na ikafikia wakati likakwama sehemu na tukasukuma na kulitoa, safari ikaendelea.

“Lakini tulipofika sehemu nyingine tena, gari likaharibika na kulikuwa na hofu huenda tungechelewa hata kucheza mechi. Hivyo tukaomba msaada kwenye roli la mchanga kutoka kampuni iliyokuwa inatengeneza barabara na tukalazimika kulipa ili twende Lindi.

“Wale jamaa wakawa tayari kutoa lile roli, lakini baadaye wakasisitiza ilikuwa ni lazima kila mchezaji lazima alipe nauli ya shilingi elfu moja kwa kuwa hatukuwa mbali sana kabla ya kufika Lindi. Wakati ule hatukuwa na fedha na hakukuwa na njia ya kutuma.

“Mimi niliwaambia viongozi kuwa nina fedha na waniahidi kunirudishia na mimi nitakachofanya ni kutoa, wakakubali na nikafanya hivyo. Safari ikaendelea na tukafika Lindi ambako nakumbuka tulicheza na kuifunga Kariakoo kwa mabao 2-1.

“Wakati huo timu hiyo ilikuwa haifungiki pale Lindi, kwani hata ufunge bao vipi utaambiwa ni offside, lakini sisi tulifanya kazi ya ziada na kuwafunga na hawakuwa na ujanja kutokana na mabao yetu,” anasema Masatu.

“Pamoja na ushindi huo, bado katiika kambi ya Simba kulitokea matatizo makubwa sana, hii ilisababishwa na uamuzi wa uongozi kuwapa baadhi ya wachezaji nafasi ya kusafiri na ndege wakati wengine tulipanda lori.

“Sisi tukiwa kwenye basi na baadaye lori, kipa Mohammed Mwameja na Renatus Njohole wao walikuja na ndege hadi pale. Hii iliwaudhi wachezaji wengi sana na kusababisha zogo kubwa wakati wa kikao. Nilichofanya mimi ni kujaribu kuwapoza wachezaji nikitumia neno la riziki ya mwenzo huwezi kuizuia.

“Ajabu kiongozi mmoja, nakumbuka alikuwa anaitwa Kipukuswa, yeye aliendelea kunisakama kwa maneno. Kweli roho iliniuma sana kwa kuwa nilikuwa nimetoa fedha yangu kuhakikisha timu inafika lakini ukiachana na hivyo, bado nilijitahidi kusaidia kuwapoza wachezaji wapunguze hasira, nikamvaa.”

“Wote tulianguka chini, wakati huo sikujali tena kama kulikuwa na heshima. Maana niliona kuna tatizo pia roho iliniuma kutokana na maneno ya kashfa ambayo kiongozi huyo alikuwa anatoa mbele ya watu wote pale. Zogo kubwa likaibuka.”

BAADA ya Masatu kupanda jazba na kumvaa Kipukuswa, hali ya amani ilipotea katika kambi ya Simba. Je, nini kiliendelea? Kuna mtu alijitokeza kuwaamua au kuna mtu aliumia katika ugomvi huo? Masatu ataendelea kusimulia likiwemo suala la fainali ya Kombe la Caf mwaka 1993 ambayo yeye na wenzake walielezewa kupanga matokeo kwa kushirikiana na mdhamini wakati huyo Azim Dewji ili Simba ifungwe na kukosa kombe. Simulizi ya Masatu itaendelea keshokutwa IJUMAA, USIKOSE.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic