August 12, 2013



 Na Saleh Ally, aliyekuwa Zurich, USWISS
 Kila mmoja anaweza kuwa na ndoto zake, zangu ni nyingi na sijui kama nitatimiza zote lakini kufanya mahojiano ndani ya makao makuu ya Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) lilikuwa ni jambo kubwa na muhimu kwangu.

Hivi karibuni, nilisafiri hadi jijini Zurich, Uswis na lengo lilikuwa ni kufikia ndoto hiyo. Nilitamani kujua Fifa wanafanya vipi shughuli zao hadi kufikia kufanya mambo makubwa ikiwa ni pamoja na kutoa misaada kwa wanachama wake.
 
...AKITAZAMA MAKOMBE MBALIMBA YA DUNIA KAMA KOMBE LA DUNIA LA WANAWAKE, VIJANA, KOMBE LA MABARA, KOMBE LA DUNIA LA KLABU NA MENGINEYO YALIYO CHINI YA FIFA
Mfano, kila mwaka hutoa zaidi ya dola 250,000 (Sh milioni 405) kwa Tanzania ambao ni wanachama. Swali ni je, Fifa wanaingiza vipi fedha wakati hawana ligi wanayoisimamia moja kwa moja? Kumbuka kwamba, Fifa pia ni moja ya mashirika au taasisi tajiri kabisa duniani.
 
...AKIWA NA KOMBE LA DUNIA
Maswali yalikuwa mengi, lakini ilikuwa shida na ngumu kupata mwaliko hadi siku ilipotimia. Waalikwa wa siku hiyo walikuwa hawa; waamuzi kutoka Sweden, makocha kutoka Japan, wakala kutoka Tanzania (Damas Ndumbaro) na waandishi wawili, Amber Lee (ESPN-Marekani) na Saleh Ally (Salehjembe.com-Tanzania).

Sikutegemea kumuona Ndumbaro pale Fifa, wakati naingia alikuwa anatoka, nililazimika kumshawishi ili niweze kumhoji na hivyo ikabidi anisubiri wakati nikiingia katika chumba cha mahojiano na baadaye kutembezwa katika sehemu mbalimbali za jengo hilo.

...AKIWA NA WAAMUZI WA FIFA KUTOKA SWEDEN PAMOJA NA OFISA WA FIFA

Hata hivyo, ombi langu moja la kutaka kuzungumza na Rais Sepp Blatter liliondolewa, hivyo aliyekuwa anaisimamia ziara yangu alitaka kujua kilichonipa ujasiri wa kutaka kumuona Blatter, nikampa majibu, mwisho akasisitiza anaamini siku itafika itakuwa hivyo, yaani nitamuona, lakini wakati huo alikuwa amebanwa na alikuwa nje ya ofisi.

Kweli Blatter ni mkubwa, lakini hata Salehjembe ni  blog kubwa ya michezo, hata kama kuna kasoro kwa kuwa linaongozwa na binadamu, hivyo haki ya kumuona na kumhoji bado haipotei.

Nakubali haikuwa bahati au vinginevyo, lakini nafurahi Salehjembe.com kuwa blog ya kwanza Tanzania kufika Zurich kumsaka Blatter, hata kama hakupatikana, lakini mahojiano yakafanyika ndani ya mjengo huo.

Katika mahojiano ingawa maswali mengi yalikuwa hayajibiki kutokana na msemaji niliyepewa kusema hakuwa na mamlaka ya kujibu, alikubali kwamba kwanza Fifa haiungi mkono migogoro lakini haisaidii vyama vya soka kupambana na serikali za nchi zao.

“Hatuungi mkono migogoro, soka linachezwa kwenye amani. Lakini tunasisitiza mambo yaende kwenye msitari kwa kufuata utaratibu. Lakini pia tunakataa serikali kutumia mabavu kuviingilia vyama, Tanzania kuna matatizo lakini tunaona hayajafikia katika kiwango kikubwa.

“Tunaamini siku itafika jibu litapatikana na mambo yanakwenda vizuri, hivyo lazima kuwe na subira na kama kuna makundi, basi yawe kwa ajili ya uchaguzi na baada ya hapo watu waungane,” anasema.

“Pamoja na hivyo, mimi nikaangalia zaidi kuhusiana na Fifa, kwamba inatoa wapi fedha za kuweza kusaidia nchi lukuki, tena mamilioni ya fedha.

“Fifa inategemea mapato yake katika haki ya mambo kadhaa, lakini matangazo ya TV ndiyo yanaingiza fedha nyingi sana na hasa katika michuano ya Kombe la Dunia.



“Kati ya mwaka 2007 na 2010, kulikuwa na mafanikio na mabadiliko makubwa katika kipato chetu, tulifanikiwa kuingiza hadi dola bilioni 4.189 (Sh trilioni 6.8) ukilinganisha na miaka minne ya nyuma tuliyokuwa tumeingiza dola bilioni 2.634 (Sh trilioni 4.3).

 
“Wakati wa Kombe la Dunia la Afrika Kusini ndiyo kulikuwa na mabadiliko makubwa zaidi ya kipato kwa Fifa. Tuliingiza dola bilioni 2.408. Kati ya hizo dola bilioni 1.072 zilitokana na mapato ya haki za matangazo.

“Pamoja na kwamba tunaingiza fedha nyingi kutoka kwa wadhamini lakini Kombe la Dunia pekee liliingiza takribani asilimia 87 ya mapato yote.

“Haya yalikuwa mapinduzi makubwa ya kiuchumi, haraka baada ya hapo, timu yetu ya wachumi ikaongezwa nguvu, imekuwa kubwa zaidi kwa lengo la kufanya uchunguzi wa kutanua soko.

“Tunataka kuingiza fedha nyingi zaidi kwa kuwa tuna matumizi makubwa. Hivyo tuna wataalamu wa uchumi kutoka makampuni makubwa kabisa duniani, wengine ni maprofesa na ndiyo wanaoendelea kutufanyia uchunguzi,” anasema.

Hapo nikaanza kugundua ‘akili’ ya haraka ya Fifa na tofauti yake na ile ya TFF ambayo ina mtu mmoja tu wa masoko, tena ambaye hasikiki hata chembe na haijulikani kama anafanya kazi ya kutafuta masoko au la.

Kweli TFF inafanya kazi ya mpira, lakini najiuliza ina juhudi zipi kuwavuta wadhamini lukuki ili kupata mafanikio zaidi, hasa kwa kuwa kama wakijitokeza na kutoa fedha ndiyo maendeleo yenyewe? TFF inapata misaada kutoka Fifa kwa kuwa shirikisho hilo la kimataifa limeajiri ‘wakali’ wa masuala ya uchumi ili kupata faida.

Hapa nyumbani ni tofauti, inawezekana soko halipewi umakini mkubwa, hili si suala la leo, maana mgogoro kati ya Yanga na Azam TV usiwe kisingizio, lakini TFF lazima ikubali, lazima kuwe na juhudi za makusudi za kutafuta masoko.

Hakika haiwezi kuingiza mabilioni kama ya Fifa, lakini inaweza kupata fedha zaidi na kujenga mafanikio ambayo yataiwezesha kusaidia ipasavyo vyama vya wilaya na mikoa.

Fifa inapeleka mamilioni ya fedha katika nchi nyingi ikiwemo Tanzania, hata TFF ikiwa na mipango, siku moja itapeleka fedha wilayani na mikoani na mwisho mafanikio yatapatikana kwa kuwa fedha inasaidia mabadiliko.

Hakutakuwa na maendeleo kama TFF itakuwa ni ya Dar es Salaam tu. Angalia Fifa inajua Ulaya na Marekani ndiyo Dar es Salaam na wanajiendeleza wenyewe. Lakini Afrika ndiyo mikoani, inapeleka misaada na mambo yanakwenda.

Mfano katika fedha hizo inazoingiza, nyingi pia zinatumika Afrika, Amerika Kusini na Asia na moja ya miradi yake mikubwa ni ule wa kujenga viwanja wa Goal Project. Tayari Tanzania Bara na Zanzibar zimeshafaidika.

Sasa kuona fedha tu za Fifa zinatua nchini kama mvua na hakuna anayejifunza kutoka katika shirikisho letu, mimi naona si sahihi. Inawezekana nikawa nimejifunza mengi kutokana na maswali yangu, lakini hili lilinigusa zaidi, ninaamini TFF wanaweza kujitanua zaidi.

Soka ni utajiri, hasa ikipata watu makini wanaolenga maendeleo. Haitakuwa rahisi, lakini waliokabidhiwa dhamana lazima wakubali kuumia na kuchoka kwa ajili ya kuleta maendeleo, nasi tuwaamini na kuwapa nafasi.

TFF inaweza kusaidia kukua kwa soka kwa kujali vijana na kusaidia soka vijijini, wilayani na mikoani lakini hata kama programu zitakuwa vipi, lazima kuwe na fedha ambazo zitapatikana kwa kuwa na watu wabunifu na makini wa kuzitafuta.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic