August 7, 2013




Saleh Ally, Colmar 
KIWA unatembea katika mitaa mbalimbali ya miji ya Ufaransa, kuna mambo mengi ambayo unaweza kujifunza kama utakuwa unataka kuchunguza.
Kwa kuwa nimefika katika nchi zaidi ya tano za bara la Ulaya, Ufaransa inaonekana ndiyo nchi yenye Waafrika au watu wengi zaidi wenye asili ya bara la Afrika ambao wanaishi katika nchi hiyo.

Wako wale ambao wazazi wao walihamia tokea kitambo, wengine wamehamia kutoka katika nchi zao hivi karibuni lakini kwa kifupi huenda ikawa ndiyo nchi ambayo ubaguzi wa rangi kwa Waafrika ukawa si katika kiwango cha juu kama utalinganisha na Hispania, Italia, Ujerumani na kwingineko.

Huenda England pia ikawa inaikaribia Ufaransa, lakini katika miji miwili ya Colmar na Strasbourg nchini Ufaransa niliyoitembelea, hali hiyo inajionyesha wazi na huenda hakuna mtu anayeonyesha kunishangaa sana kama mgeni pale ninapokuwa ninakatiza mitaa kwa mwendo wa mdundo.

Hali hiyo ya mitaani, ndiyo jibu sahihi katika Ligi Kuu ya Ufaransa maarufu kama Ligue 1 ndiyo ligi kubwa duniani ya soka ambayo wachezaji wengi wenye asili ya Afrika wameweza kufanya vizuri na baadaye kuibuka na kuwa maarufu.

Haina maana ni Waafrika pekee ambao wanajulikana, wako wengi wakiwemo Wafaransa wenyewe wasio na asili ya pembeni, lakini hali halisi ni kwamba hakuna ligi nyingine maarufu duniani ambayo wachezaji wenye asili ya Afrika wamepata umaarufu mkubwa kama ligi hii.

Kama ukifanya hesabu za haraka kwa sasa, katika timu kubwa tatu za Ufaransa kama Olympique de Marseille, AS Monaco na PSG utagundua kuna zaidi ya wachezaji 35 katika vikosi vyote kuanzia za vijana hadi kikosi kikubwa.

Lakini kama ni vikosi vikubwa, basi ni zaidi ya wachezaji 15 kwa jumla ya timu zote hizo, kitu ambacho si rahisi kutokea katika ligi kama zile za England au Premiership, La Liga ya Hispania na Serie A ya Italia.

Wachezaji lukuki wenye mafanikio au majina makubwa kutoka Afrika au wenye asili ya Afrika wamepitia Ufaransa kabla ya kwenda kwenye ligi nyingine na kupata umaarufu mkubwa.

Achana na wale wenye asili ya Ulaya kama Michel Platin, Éric Cantona, Didier Deschamps, Christophe Dugarry, Fabien Barthez, Emmanuel Petit, Laurent Blanc Mikel Arteta na wengine wengi. Lakini angalia hawa wafuatao ambao asili yao ni Afrika na wamekuza soka lao nchini humo.

Zinedine Zidane,  Basile Boli, , Nicholas Anelka,  Marcel Desailly, Jean Djorkaeff, Jean Tigana, Abeid Pele, Didier Drogba, Lilian Thuram, Thierry Henry, Youri Djorkaeff, Patrice Evra, Hatem Ben Arfa na wengine kibao ambao unaweza kutumia muda wako kidogo tu kuwakumbuka.

Wengine ni George Weah alitokea moja kwa moja Cameroon ambako alikuwa anacheza soka baada ya kuchukuliwa kutoka kwao Liberia. Akapaa hadi Ufaransa kwa nguvu za Arsene Wenger, baadaye akaja kuwa mchezaji bora wa dunia.

Lakini angalia pamoja na kupita Tanzania, Afrika Kusini na Uswis, jina la Shabani Nonda lilipaa zaidi na kupata soko kubwa baada ya kuanza kucheza katika timu za Ligi Kuu ya Ufaransa.

Wako wengi wengine ambao walifanya vizuri hapa kama Mnigeria Victor Ikpeba aliyekuwa lulu akitokea Monaco, lakini Emmanuel Adebayor kutoka Togo pia akatengeneza jina kutoka hapa na sasa ni kati ya wachezaji maarufu kabisa kutoka Afrika.

Ligi ya Ufaransa ni ya ushindani mkubwa kutokana na vipaji vingi, ndiyo maana timu nyingi tajiri kutoka katika ligi za England, Italia na Hispania huona ni rahisi zaidi kupata wachezaji hapa na kuwatumia.

Inakuwa ni nadra mchezaji nyota wa England kuja kucheza hapa baada ya kufanya vizuri huko au Hispania, labda kama atakuwa anakaribia kustaafu ingawa PSG na Monaco zikiwa chini ya mabilionea wa Kiarabu zinaanza ‘kupindua kabati’ kwa kugeuza mambo kwani sasa ziwanunua wachezaji maarufu kutoka katika ligi hizo kubwa duniani na si kuuza pekee kama ilivyokuwa awali.

Beki wa SRC Colmar inayoshiriki ligi daraja la pili Ufaransa, Jean Verger, anasema hajawahi kusikia mchezaji analalamika kwa kubaguliwa kwa kuwa Ufaransa ndiyo nchi ya Ulaya inayoongoza kwa kuwa na mchanganyiko wa jamii nyingi zaidi.

“Nimeanza kucheza soka nikiwa na miaka tisa, sasa nina miaka thelathini na nimekuwa najiandaa kustaafu ndiyo maana nasomea ukocha. Lakini Ufaransa ndiyo nchi yenye watu wote duniani na wanaishi sawa.

“Ukisema umbague mweusi kutoka Afrika, kuna wengi tu ambao si weusi ambao wanatokea Afrika. Watu kutoka Tunisia, Morocco na Algeria. Utaona hadi kuna sehemu zinajulikana kuwa ni maeneo kwa ajili yao tu.

“Lakini hata imani za kidini, hapa watu wana nafasi kubwa ukilinganisha na sehemu nyingine. Ufaransa ni nchi huru ya kila mmoja. Lakini serikali ya hapa ni wakali sana kwa anayevunja sheria kwa kuwa wanataka watu waishi pamoja kwa amani,” anasema Verger.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic