August 7, 2013



Na Saleh Ally, Strasbourg
SAFARI ya kwanza nilishindwa kufika katika mji wa Strasbourg nchini Ufaransa, nilibanwa na kumaliza shughuli zangu katika miji kadhaa ya Ujerumani. Lakini safari hii niliona ingekuwa muhimu kufanya hivyo kwa ajili ya kujifunza lakini kuwafikishia wasomaji wanachohitaji.
 http://media.irishcentral.com/images/20111101040416arsene_wenger.jpg
Niliamua kusafiri nikitokea mji wa Freiburg nchini Ujerumani na baada ya saa moja na nusu tu nilikuwa nimeishavuka na kuingia nchini Ufaransa katika mji wa Colmar, hapo nilipata chakula cha usiku na kuendelea na safari yangu na nilitaka kufika Strasbourg.

Kwa wanasiasa, huenda wangedhani niliamua kuingia kwenye rekodi ya watu waliowahi kufika katika jengo maarufu zaidi la Bunge la Ulaya ambalo liko katika mji huu wa nane kwa ukubwa nchini Ufaransa na uko Mashariki mwa nchi hii, si mbali kutoka Ujerumani.

Kama mwanamichezo nimevutiwa kufika Strasbourg kwa kuwa ndiyo mji aliozaliwa Kocha Mkuu wa Arsenal, Arsene Wenger, ambaye pamoja na baadhi ya mashabiki wengi kumbeza, lakini ni maarufu huenda kuliko mwanamichezo yeyote wa Ufaransa katika eneo lote la nchi hiyo linalopakana na Ujerumani.

Bunge la Ulaya ni maarufu zaidi, lakini inaonekana baada ya hapo, wengi wanamzungumzia Wenger, kwani hata wafanyakazi wa bunge hilo, mara kadhaa walikumbushia kwamba mji huo anatokea Wenger ambaye kwa sasa ndiye kocha maarufu zaidi kutoka Ufaransa.

Ukiachana na kwamba ndiye kocha mwenye mafanikio zaidi kuliko wote waliowahi kuifundisha Arsenal kwa maana ya kutoa vikombe 11 ambavyo ni vingi zaidi, lakini Wenger ni kocha msomi ambaye nje ya soka, amekuwa na mambo mengi ya ziada kama vile elimu ya uchumi.

Kitaaluma, alihitimu ‘masters’ ya uchumi katika Chuo cha Stanford, California, nchini Marekani na ana uwezo wa kuzungumza lugha kadhaa zikiwemo Kifaransa, Kijerumani, Kiingereza na Kijapani.

Mji wa Strasbourg una Wafaransa wengi wanaozungumza Kijerumani na ndiyo mji unaoongoza kwa kutoa wachapakazi kwa kuwa utamaduni wao umechanganyika na ule wa Kijerumani. Kawaida Wafaransa wengi wanajulikana kwa kupeleka mambo yao taratibu kwa madaha, kwa kifupi wana sifa ya uvivu na maneno mengi, lakini wanaoishi katika mji huu ni majembe.

Asilimia kubwa ya watu wanaoishi katika mji huu wanajivunia Wenger, mfano katika hoteli mbalimbali, sehemu za usafiri wa jamii, lakini hata kwenye viwanja vidogo vya soka, wanaona ni jambo zuri kusema ndiko Wenger alikozaliwa Oktoba 22, 1949.

Ingawa baada ya kukua, Wenger alihamia katika mji mdogo wa Duttlenheim na kuanza kucheza katika timu ya FC Duttlenheim iliyokuwa inafundishwa na baba yake, baadaye alirejea tena katika mji huu na kujiunga na kikosi cha Mutzig na baadaye Mulhouse.

Kuonyesha hapa ndipo ‘home’, Wenger alirejea na kujiunga na ASPV Strasbourg ambayo aliichezea kuanzia mwaka 1975-78 na kuhamia kwa wapinzani wao wa RC Strasbourg alikocheza mechi 11 tu na baada ya hapo akastaafu soka na kuingia katika ukocha baada ya kuwa amehitimu diploma ya ukocha.

Mashabiki wengi wa soka katika mji huu wanamuita Wenger kwa jina la Le Professeur, yaani Profesa na asili ya watu wengi wa hapa ni wasomi, wanapenda ‘kubukua’ na mara nyingi ni watu wa vazi la suti na wanajulikana kwa maringo ingawa bado sifa ya uchapakazi inawalinda.

Alikozaliwa Wenger leo si kijiji tena, badala yake kuna majengo mazuri tofauti na ilivyokuwa mwanzo lakini bado asilimia kubwa ya familia yake ni watumishi wa kanisa kwa kuwa hata yeye akiwa mdogo amewahi kuwa kati ya watumishi wa kanisa.



Kwa timu zinazoshiriki Ligi Kuu England, mashabiki wengi wa mji huu wanaiunga zaidi mkono Arsenal kwa sababu mbili kuu, kwanza kabisa ni kwa sababu ya Wenger na anapewa heshima kama mtu aliyefanya kazi ya ziada kutoka katika familia ya kimasikini, baadaye kuwa msomi na anayeutangaza mji huu kimataifa.

Pili, wachezaji wengi kutoka Ufaransa kama Patrick Vieira, Thierry Henry, Robert Pires, Emmanuel Petit, Silvan Wiltord na wengine wameitangaza sana Ufaransa kisoka na kikubwa wengi wao walikuwa katika kikosi cha Ufaransa kilichotwaa ubingwa wa Kombe la Dunia mwaka 1998, hivyo Arsenal hapa ni kama nyumbani.

Katika hali ya kawaida unaweza kudhani umaarufu wa Wenger ni kitu kidogo sana, lakini hali halisi inaonyesha kocha huyo ana umaarufu mkubwa sana kwa kuwa mji wa Strasbourg ni kati ya miji mikongwe kabisa duniani na una bandari maarufu na ya pili kwa ukubwa katika zile zilizo katika mto maarufu Ulaya uitwao Rhines.

Miaka kadhaa iliyopita Strasbourg ulitangazwa kuwa moja ya urithi wa dunia katika miji bora, ingawa ni wa tisa kwa ukubwa nchini Ufaransa lakini ulishika nafasi ya tatu kwa ubora wa mpangilio katika nchi hii na wa 18 duniani.

Strasbourg ni mji wenye mambo mengi sana ya kumbukumbu na una mpagilio wa majumba mengi sana ya kizamani ambayo yanabaki kuwa kama kumbukumbu ikiwemo moja ya sehemu ambayo Wajerumani waliporwa na Wafaransa baada ya vita ya pili ya dunia.

Mmoja wa wahudumu katika hoteli niliyofikia aliniambia, kuna idadi kubwa kubwa ya vijana wamekuwa na ndoto ya kuwa makocha bora badala ya wachezaji bora kwa sababu ya kocha huyo. Lakini hata walioshindwa kufanya vizuri katika soka la kulipwa, husema wanaweza kuwa makocha wazuri kwa kuwa hata Wenger hakuwahi kunga’ra wakati akicheza.

Pamoja na mambo mengi ya kila aina katika mji huo, Wenger anaendelea kubaki namba mbili katika wanaozungumzwa au maarufu zaidi baada ya bunge la Ulaya ambalo kila wiki au mwezi, linawakutanisha watu maarufu wa Ulaya au duniani kote.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic