October 7, 2013





Na Saleh Ally
Mshambuliaji nyota wa Simba, Amissi Tambwe amesema ameanza kuingia hofu kutokana na mabeki kumpania lakini mbaya zaidi ni kumshambulia kwa kumpiga ngumi kila wanapopata nafasi ya kufanya hivyo.


Tambwe raia wa Burundi, ameliambia Championi Jumatatu kwamba amekuwa akishambuliwa kila mara na mabeki wa timu mbalimbali kwa kupigwa ngumi za kichwani, tumboni na mabeki wa Ruvu JKT walitia fora zaidi.

“Karibu kila mechi nilicheza nimekuwa nikikumbana na hali hiyo, lazima nipigwe ngumi mbili au tatu, matusi ndiyo usiseme, tena masimango ya ajabu. Wale wanajeshi (Ruvu Shooting) wa jana (juzi), walinipiga ngumi nyingi zaidi, zinazidi tatu na mmoja alinipa ngumi ya jicho, nikapata maumivu makali sana.

“Baada ya mechi nililazimika kwenda kwa daktari naye akanifanyia uchunguzi na kusema sikuumia sana, ila kulikuwa na uvimbe kidogo ambao leo umezidi kupungua,” alisema mshambuliaji huyo aliyepiga mabao nane katika mechi sita.

Tambwe alipoulizwa kama anahitaji ulinzi, alisema: “Ulinzi maalum si sahihi, lakini sheria zifuatwe na waamuzi wanaweza kuliona hilo kwa kuwa wako zaidi ya mmoja uwanjani. Soka si mchezo wa kuumizana kwa makusudi.

“Kila mtu atumie mbinu kumpita au kumzuia mwenzake lakini kimichezo, kupigana ngumi na wakati mwingine mateke kwa makusudi si kitu chema.
“Angalia, mara kadhaa wachezaji wanawatukana kabisa waamuzi, lakini wanawaacha, huenda wanahofia. Nafikiri hata wachezaji tunapaswa kuangalia Fair Play, si sahihi kutoa lugha chafu kwa waamuzi.

“Kama akija mwamuzi kutoka nje akapata nafasi ya kuchezesha ligi, basi ninaamini kutakuwa na kadi nyingi sana kwa kuwa wachezaji wengi hawaheshimu waamuzi na wanacheza kwa uadui, soka ni kazi, soka ni furaha.”

Tambwe amekuwa gumzo kutokana na uwezo wake wa kupachika mabao, wakati ligi ina mechi saba kwa kila timu, yeye ameishapachika mabao nane kimiani.
SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic