November 8, 2013

BOBBY AKIWA MAZOEZINI, JANA JIJINI NAIROBI

Na Saleh Ally, Nairobi
Bado inaonekana uongozi na hata mashabiki wa Simba hawana furaha sana na mwenendo wa kikosi chao, ingawa wako wanaamini mambo yanaweza kwenda sawa.


Mashabiki na wanachama wa Simba, huenda wangefurahi kupata mkombozi wa kuwatoa hapo walipo, wengi wanaamini kocha mwingine na hasa mahiri na ikiwezekana kutoka nje ya Tanzania anaweza kuwa msaada mkubwa.
...SALEH ALLY NA BOBBY NYUMBANI KWAKE KATIKA ENEO LA HURLIGHAM JIJINI NAIROBI

Uongozi wa Simba, bado haujafungua mdomo wake rasmi kusema kwamba Kocha Abdallah kibadeni na msaidizi wake, Jamhuri Kiwhelo ‘Julio’ ambaye hahofii kutimuliwa, kwamba safari imewakuta.

Mechi ya juzi dhidi ya Ashanti United ilikuwa inasubiriwa kama jibu sahihi la nini cha kufanya lakini kabla kukaibuka taarifa za ujio wa kocha mpya, huyu ni Robert ‘Bobby’ Williamson, raia wa Scotland.

Taarifa hizo kutoka katika gazeti ambalo hutoka Jumamosi, liking’ara na picha kubwa kabisa mbele, lilieleza kuwa Mskochi huyo ndiye kocha mpya wa Simba, ikiwa ni habari kubwa na tayari ikazua hofu kwa makocha wa Simba na furaha kwa baadhi ya mashabiki, kwamba mkombozi amepatikana.

Uchunguzi wa Salehjembe ulianza kuonyesha hofu katika jambo hilo, kwani viongozi karibu wote wa Simba, walisema wazi hawakuwa wamefanya mazungumzo na Williamson kuhusiana na suala la yeye kujiunga Simba.

Vipi kuwe na taarifa kama hiyo bila hata kuwa na uhakika, kwa kuwa Nairobi si mbali hasa kama wasomaji wanataka uhakika wa jambo, Championi lilifunga safari hadi katika mji huo mkubwa zaidi nchini Kenya kwa ajili ya kuzungumza naye, ana kwa ana ili kupata uhakika zaidi.

Williamson ambaye ni mshambuliaji wa zamani wa Rangers ya Scotland ambaye Alex Ferguson pia aliwahi kuichezwa kama mshambuliaji, anaonyesha kushangazwa na jambo hilo, huku akisisitiza hapendi kuzushiwa mambo, badala yake hufurahia uhakika wa mambo.

Kocha huyo ambaye pia amewahi kuinoa Wes Brom Albion ya England kati ya mwaka 1986-88, anasema amekuwa akifanya mambo yake kwa kufuata utaratibu kwa kila kitu na sasa anaheshimu sana mkataba wake.
Kwani siku chache, Williamson ameiongoza Gor Mahia anayoinoa sasa kutwaa ubingwa wa Kenya baada ya kuukosa kwa zaidi ya miaka kumi.
Sifa yake kubwa katika ukanda wa Afrika Mashariki ilianza kupanda baada ya kubadilisha soka la Uganda na kuibebesha Kombe la Chalenji kwa miaka minne ambayo ni  2008, 2009, 2011, 2012.
Mahojiano kati ya Williamson na gazeti hili, yalifanyika jijini hapa nyumbani kwake katika eneo la Hurringum, moja ya maeneo yanayokaliwa na ‘wenye nazo’.

Salehjembe: Vipi Bobby, taarifa za wewe kuwa ni kocha mpya Simba zimeshika kasi nchini Tanzania, labda lini unatarajia kutua na umeishakubaliana nao kuhusiana na maslahi?
Bobby: Kuna mtu pia kanieleza kuhusu hilo kutoka Tanzania, lakini nakuhakikishia sijawahi kuzungumza na kiongozi au mtu yoyote wa Simba.
Salehjembe: Taarifa zinasema mmeanza mazungumzo, au ni siri kubwa?
Bobby: Sidhani kama kuna siri katika jambo kama hilo, kama Simba wangekuja, basi ningewaeleza wanonane na Gor (Mahia) kwanza. Ninaheshimu mkataba wangu na nisingependa kuchanganya mambo.
Salehjembe: Mara nyingi watu wa mpira mmekuwa mkificha mambo, utakataa leo, kesho tunasikia uko Simba.
Bobby: Kama watakuja Simba, basi labda nisubiri, ikiwa hivyo nitakueleza mara moja. Lakini nakuhakikishia, sina mazungumzo yote na Simba, ndiyo maana nasema sipendi mambo ya kuzushiwa.
Salehjembe: Kuzushiwa kivipi?
Bobby: Nimeelezwa kuwa imeripotiwa mimi ni kocha mpya Simba, ni kitu ambacho sikijui kabisa. Wewe pia umeuliza kitu hicho hicho. Mimi ni mtu mwenye ushirikiano, naweza kupatikana na ningezungumza kama ninavyofanya hapa. Sipendi kabisa mambo ya kubahatisha, mimi ni kocha wa Gor.
Salehjembe: Labda mkataba wako unaisha lini na ikitokea timu ikakuhitaji, mfano Simba au nyingine yoyote, uko tayari kuondoka?
Bobby: Mkataba unaisha mwakani, sina shida katika suala la kuondoka, mimi ni kocha lakini ningependa utaratibu ufuatwe na ndiyo maana nasisitiza uongozi wa Gor kupitia kwa mwenyekiti vizuri ukahusishwa.
Salehjembe: Tukiachana na hilo ambalo angalau sasa tuna uhakika, vipi kuhusiana na kipa Ivo Mapunda ambaye ni kati ya vijana wako.
Bobby: Mapunda ni kati ya makipa bora kabisa katika kikosi changu, anafanya kazi yake vizuri. Ni kipa wa pili lakini amefanya kazi nzuri sana kila alipopewa nafasi.
Salehjembe: Unampa nafasi gani kutokana na makipa uliowahi kuwafundisha kuanzia Uganda?
Bobby: Nafasi ya juu, kwa maana ya kiwango na nidhamu. Lakini anajituma na ukuliza mashabiki watakuambia, anaipenda kazi yake na wanampenda sana.
Salehjembe: Ulikuwa kocha wa mshambuliaji Emmanuel Okwi, lakini mambo yake yamekuwa hayaendi vizuri pamoja na wengi kuamini anaweza kucheza Ulaya. Unafikiri nini tatizo?
Bobby: Okwi ni kati ya wachezaji bora kabisa katika ukanda huu, inawezekana pia namna ya kumuongoza au kujiunga na timu ambayo hawakuendana. Lakini bado ana nafasi ingawa anatakiwa kufanya mambo yake kwa mahesabu makubwa maana muda pia usonga mbele, kwa maana ya umri.
Salehjembe: Bobby, nashukuru sana kwa ushirikiano wako?
Bobby: Karibu tena, umesema wewe ni mwandishi chipukizi wa Salehjembe, vipi naona kama umri umeenda.

Salehjembe: (kicheko), kwaheri.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic