Kipa mpya wa Yanga, Juma Kaseja,
ameonyesha nidhamu ya hali ya juu kwa kufika katika siku ya kwanza ya mazoezi
ya timu hiyo, lakini akapigwa ‘stop’ kuanza kazi katika timu hiyo.
Nassoro Matuzya, ambaye ni Daktari Mkuu
wa Yanga, amesema Kaseja hataweza kuanza kazi rasmi wiki hii kutokana na tatizo
la maumivu ya kifundo cha mguu wake wa kulia.
Matuzya amesema kipa huyo aliyesajiliwa
katika kipindi hiki cha dirisha dogo tayari ameshaanza matibabu ya tatizo hilo
wiki moja iliyopita ambapo sasa yuko katika wiki ya pili ya tiba hiyo na
kuongeza kuwa sasa ataanza rasmi kazi yake hiyo mapema wiki ijayo.
“Tumefurahi kuona amefika katika siku ya
kwanza ile jana (juzi), lakini hataweza kuanza kazi, tumemzuia kutokana na haya
maumivu yake ya kifundo cha mguu ingawa ameshaanza tiba wiki moja iliyopita,”
alisema Matuzya huku akiongeza kwa kusema:
“Wiki hii yupo katika wiki ya pili ya
tiba hiyo ambayo inatakiwa aifanye kwa wiki mbili, nafikiri kwa hali
nilivyoiona ataweza kuanza kazi rasmi wiki ijayo, kama kila kitu kitakuwa sawa
kama hali inavyokwenda sasa.”
Kaseja alipata maumivu hayo wakati
akifanya mazoezi yake binafsi katika kujiweka sawa kabla ya kuanza kuitumikia
timu hiyo.
Kabla ya kujiunga na Yanga Kaseja
alikuwa nje kwa nusu msimu baada ya kumaliza mkataba wake na timu yake ya muda
mrefu, Simba.
0 COMMENTS:
Post a Comment