November 29, 2013





Na Saleh Ally
Mbeya City ndiyo imepanda Ligi Kuu Bara msimu huu, lakini baada ya mechi 13 za mzunguko wa kwanza, utafikiri ilipanda daraja misimu mitatu iliyopita.


Kuna mambo mengi muhimu ambayo yameonekana kupitia Mbeya City na inawezekana kabisa wadau wa timu nyingine wakikubali watajifunza.

Pamoja na ugeni wake, Mbeya City imeonyesha mambo kadhaa ambayo ni nadra kufanywa na timu iliyopanda msimu kwa mara ya kwanza.

Ndani ya mechi 13 pekee, Mbeya City imefanya mapinduzi makubwa ambayo yanaweza kuwa funzo kwa timu nyingine.

Wananchi:
Mbeya City imeonyesha ni timu ya wananchi kweli kwa kuwa imefanikiwa kushika nafasi ya tatu katika timu zilizoingiza mashabiki wengi baada ya Yanga na Simba.
Katika mechi 13 ilizocheza, Mbeya City imeingiza mashabiki 43,439 na kuzipiku timu kibao ikiwemo Azam FC iliyoshika nafasi ya nne kwa kuingiza mashabiki 30,236.

Azam FC ni maarufu maradufu zaidi ya Mbeya City, lakini wingi kwa wa mashabiki wa timu hiyo, imeshika nafasi ya juu.
Unaweza kusema watu wa Mbeya walikuwa na hamu ya kushuhudia mechi za Ligi Kuu Bara. Kwao si kitu kigeni kwa kuwa walikuwa na Prisons. Hii inaonyesha kiasi gani timu zinazoungwa mkono na mashabiki zinavyokuwa na nguvu.

Mapato:
Katika suala la mapato, ni sawa na kusema kuwa ni kitu cha kushangaza kwa kuwa Mbeya City pia imeshika nafasi ya tatu baada ya Yanga na Simba.
Yanga imeongoza kwa mapato, katika mechi 13 inafuatiwa na Simba ambazo zimeingiza zaidi ya Sh bilioni kwa kila moja.
Mbeya City pia imejitutumua kwa kuwa katika mechi 13 ilizocheza Mbeya na kwenye viwanja vingine, imeingiza Sh milioni 360.7. Maana yake ndiyo timu inayopendwa zaidi sasa kwenye ligi hiyo baada ya Yanga na Simba.

Sokoine & ugenini:
Mbeya City inakubalika zaidi kwao Mbeya, hilo halina ubishi na takwimu zinaonyesha katika Sh milioni 360.7, Sh milioni 201 zimepatikana kwenye Uwanja wa Sokoine ambao ndiyo wa nyumbani.
Pia imeusaidia uwanja huo kurudisha umaarufu wake kama enzi za Tukuyu au Mecco, maana umekuwa wa pili kwa kuingiza fedha na mashabiki wengi baada ya Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Lakini bado imekuwa timu iliyofanya vizuri kwa kuingiza fedha nyingi ugenini ukiacha Simba na Yanga. Katika mechi hizo nje ya Sokoine, imeingiza Sh milioni 159.5.

Kichekesho:
Kichekesho kiko katika makato, kwamba pamoja na Mbeya City kuonyesha mapinduzi makubwa katika soka ikiwa ndiyo imeshiriki ligi nusu msimu tu na kuingiza Sh milioni 360.7, imejikuta ikiambulia fedha kiduchu sana.
Katika mechi hizo 13, Mbeya City imeambulia kama Sh milioni 83.8 tu huku ikiacha zaidi ya Sh milioni 150 zikiingia kwenye migawo mingine. Kugawa kwa timu pinzani ni sahihi, lakini makato yamekuwa mengi sana.
Inaonekana ni kama kichekesho kwa kuwa timu kama Mbeya City au hata nyingine zimejitahidi kuingiza fedha nyingi, lakini nyingi zinaangukia katika mengine ambayo hata hayana msingi.
Katika mechi mbili dhidi ya Yanga na Simba, kabla ya makato, Mbeya City iliingiza Sh milioni 223, hii inaonyesha mechi zake dhidi ya watani hao zinafuatiliwa na ziliingiza zaidi ya asilimia 75 ya fedha zilizopatikana katika mapato ya timu hiyo.
Huenda hilo likaangaliwa na kuchukuliwa hatua ili kuendelea kuzipa nguvu timu zinazoibuka na kuleta changamoto katika mpira wa Tanzania kama ilivyo kwa Mbeya City.
Lazima katika suala la makato kuwe na kipaumbele kwa timu kwanza, vitu vingine vifuatie huku vikijua kuzipa timu nguvu, hii itasaidia mapato kuendelea kupatikana kwa muda mrefu zaidi kuliko kuzikata kupindukia.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic