November 4, 2013


Na Saleh Ally
Kuna mambo mengi sana yanatokea ndani ya Klabu ya Simba, ukijaribu kuyazungumza, basi wahusika wanatafuta ‘huruma’ kwa kusema wanasakamwa huku wakitolea mifano laini kwamba mbona wengine wameachwa!

Kitu kizuri ni hivi; ni mara chache kuwakuta wakisema kilichozungumzwa ni uongo, badala yake husisitiza aliyewakosoa ametumika au amesahau kuwakosoa wengine. Wanakuwa si wanaochambua hoja husika, badala yake wanaivisha masikio iliyopo ili kujali ambayo hayahusiki wakati husika.

Moja ya vitu vya ajabu kabisa vinavyotokea Simba katika kipindi hiki ni ile tabia ya benchi la ufundi kwamba mchezaji hata akishindwa kucheza vizuri katika mechi moja tu, anaingia kwenye lawama kubwa na kushushwa katika kikosi cha kwanza. Hii ni ajabu.
Mimi si kocha, lakini kweli inawezekana vipi mchezaji anaposhindwa kucheza mechi moja tu anashushwa kikosi B na hakuna msamaha hali ambayo inajenga hali ya visasi vya wazi?
Kocha Mkuu, Abdallah Kibadeni na msaidizi wake, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’, ndiyo makocha wazalendo ambao tuliamini wangeweza kuwa mfano, lakini mambo yamekuwa tofauti, lawama na tofauti ndiyo yamekuwa mazungumzo yao.

Simba haiwezi kupoteza mchezo bila ya kuwa na mchawi anayeangushiwa mzigo. Kila mechi utasikia hujuma, mchezaji anashushwa timu B lakini ukiangalia kiuchezaji, Simba inahaha katika mechi kadhaa kutokana na kukosa wachezaji wazoefu.
Hii inazua hofu huenda wachezaji wakongwe wanaonekana ni kama sumu katika kikosi cha Simba, jiulize nini hasa tatizo? 

Inawezekana kuna tatizo la woga kwamba kama kuna kitu kinakosewa wanaweza kuhoji, hivyo kusababisha waonekane ni adui.

Wachezaji walioadhibiwa ni Henry Joseph, Abdulhalim Humud, Ramadhani Chombo ‘Redondo’ na Haruna Chanongo ambaye ni chipukizi pekee.

Kila mmoja ameshushwa timu B ambayo sasa inataka kuonekana kama ni gereza la waovu wa timu ya kwanza, kwani anayeharibu anashushwa huko. Kawaida jukumu la timu hiyo ni kujenga na kuwapeleka juu na si kupokea rundo la wachezaji kutoka timu kubwa, eti kisa wamecheza chini ya kiwango kwa dakika 45 tu!
Walio timu B wanaweza kujengewa hisia kwamba, waliko wenyewe ni ‘gereza’ la wakosaji wa timu ya kwanza, lakini wanaoshushwa pia wanaingiwa na hofu na kuona wanadhalilishwa huku benchi la ufundi la Simba likiwasahau kabisa kwa kuwa adhabu yenyewe haina fomula.
Anayekosea hupewa nafasi ya kujirekebisha, hilo halijafanyika. Lakini kabla ya kufanya hivyo, jambo la msingi ni kuzungumza na mkosaji na kikubwa ni walimu kuangalia maslahi ya timu kwanza na si wao binafsi.
Simaanishi Simba ichukue kocha Mzungu, lakini nakukumbusha wakati fulani marehemu Patrick Mutesa Mafisango alilewa na kumtukana matusi ya nguoni Kocha Milovan Cirkovic siku chache kabla Simba haijaondoka kwenda nje ya nchi kucheza mechi muhimu ya Ligi ya Mabingwa.
Milovan, raia wa Serbia, akasema amemsamehe na kumuunganisha kwenye kikosi, akacheza na kuwa msaada mkubwa. Safari ya pili, baadhi ya viongozi wa Simba walishinikiza Haruna Moshi ‘Boban’ apewe adhabu eti alimdharau kiongozi mmoja.
Milovan akasisitiza kiongozi aliyezozana na mchezaji hakuwa wa kuchaguliwa, hivyo akataka kuwe na tofauti na umakini katika utoaji adhabu. Hasira za watoa misaada hao zikachangia Milovan kuondolewa kwa madai anashirikiana na wachezaji watukutu.
Kadhalika, baada ya kuondoka kwa kipa Juma Kaseja, utaona mambo yanavyowabana wakongwe wengine ambao sasa wameingizwa tayari kwenye mlango wa kutokea, kilichobaki ni kuufungua tu.

Henry:
Kosa lake lilikuwa ni kwenda kupumzika, lakini baada ya kuwasiliana na Julio. Kibadeni akakasirika na kumuondoa katika kambi, leo ni zaidi ya mechi ya tatu Simba imecheza, hajarudishwa.
Taarifa zinaeleza atarudi kucheza mechi ‘siriaz’ kwenye mzunguko wa pili. Jiulize Simba ilimsajili wa nini? Maana yake anaendelea kula mshahara na hatakuwa katika mpira wa ushindani kwa muda mrefu, tatizo ni hilo.

Angalia namna benchi la ufundi la Simba lilivyoshughulikia suala hilo, tafakari utaona kilichopo.

Redondo:
Ramadhani Chombo ‘Redondo’ ni kati ya wachezaji wenye uwezo mkubwa kisoka, tumekuwa tukielezwa ameshushwa kutokana na matatizo yake mengi, lakini kumbuka kipindi cha Patrick Phiri na Milovan Cirkovic alicheza tena vizuri tu.

Msimu huu tangu umeanza eti yupo kikosi cha pili tu kwa kuwa alikosea, lakini jiulize kwa kikosi cha Simba kilichopo sasa, kweli hahitajiki?

Ataendelea kubaki kikosi cha pili hadi lini na mwisho wake utakuwa upi na kweli benchi la ufundi halimhitaji? Ukweli ni kwamba anaendelea kudidimia na miaka inasonga.

Humud:
Mkongwe mwingine, huyu alikumbana na rungu la kuteremshwa katika timu ya pili eti kwa kuwa alicheza vibaya dhidi ya Yanga. Alipotolewa, vijana walioingia wakafanikiwa kuongeza nguvu na Simba ikasawazisha.

Tangu wakati huo, akabaki kikosi cha pili, hakuna maelezo zaidi lakini ukweli ni dakika 45 tu ndizo zimemuondoa kikosini. Jiulize akirudi atacheza vizuri au ndiyo kummaliza kabisa?

Chanongo:
Hapa kuna hatari zaidi, Chanongo alionyesha uwezo mkubwa msimu uliopita akitokea timu B hadi timu ya wakubwa na sasa ni tegemeo. Lakini amerudishwa kikosi cha pili na kesi yake ndiyo ileile ya Humud.

Huyu si mkongwe, lakini unapomrudisha kikosi B kwa kucheza chini ya kiwango ndani ya dakika 45 katika mechi moja tu, unamfanya aendelee kuporomoka.


Angalia umri wa Chanongo, uzoefu wake katika soka na ukubwa wa mechi ya Simba na Yanga. Lakini hebu angalia kama kweli kuna waliotuma shutuma kwake kwamba amehujumu, vipi hadi leo hawajatoa ushahidi? Ukimya wao unamaanisha hawana uhakika, hapa kuna mambo mawili tu yanaweza kufanyika, wamuachie aendelee na kazi au wawasilishe ushahidi ashughulikiwe.

2 COMMENTS:

  1. Wewe ni mchawi wa Simba!! Mbona huisemi vibaya YANGA. Makala zako zimejaa majungu na lengo ni kutaka kudhoofisha SIMBA!!!!

    ReplyDelete
    Replies
    1. wewe ulie comment, nadhani hujitambui,..sidhani kama ww ni mpenzi au mshabiki wa samba,sidhani kama yanga inahusika hapa issue ni simba ,..kiukweli hata mie namuunga mkono mwandishi wa makala hii, jullio,kibaden na mashabiki wababaishaji kama ww ndo mnao iharibu simba kwa kuwa hamtaki kuuona ukweli mkasoma alama za nyakati.

      Delete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic