November 4, 2013


Naanza na kukumbushia ile ishu ya mashabiki wa Yanga kung’oa viti katika mechi dhidi ya Coastal Union ikiwa ni baada ya mwamuzi Martin Saanya kutoa penalti na nahodha Jerry Santo akaukwamisha mpira wavuni.


Bao la Santo, raia wa Kenya, lilisababisha matokeo yawe 1-1, wakati mashabiki wa Yanga na asilimia 95 ya waliokuwa uwanjani, walikuwa wanaamini matokeo ni ushindi wa bao moja kwa mabingwa, Yanga.

Vurugu zikazuka, viti vikang’olewa na Jeshi la Polisi Tanzania likalazimika kutumia nguvu za ziada kuhakikisha hali ya usalama inarejea uwanjani hapo, hali hiyo imejirudia tena Simba ilipocheza na Kagera Sugar.

Mechi imemalizika kwa sare ya bao 1-1, Kagera wakisawazisha katika dakika za nyongeza, mfungaji wa bao akiwa ni Salum Kanoni. Bao lilitokana na mshambuliaji wa Kagera kuangushwa ndani ya eneo la hatari.

Baada ya hapo, mashabiki wa Simba wakakurupuka na kuanza kufanya vurugu kubwa iliyosababisha baadhi yao kuumia na kukimbizwa katika hospitali ya Temeke kwa ajili ya kupata matibabu.

Achana na hivyo, hiki ndicho kinachoshangaza zaidi na ninaweza angalau kulifananisha tukio hilo na lile la mashabiki wa Yanga katika mechi dhidi ya Coastal, viti vikang’olewa na safari hii vingi kwa kuwa tumeelezwa ni zaidi ya 50.
Hiki ni kitu kibaya zaidi ambacho kinapaswa kukemewa bila ya woga na waliofanya wanapaswa kutafakari mambo mengi sana ya msingi ili angalau wajutie upuuzi walioufanya.

Uwanja wanaouharibu ndiyo pekee bora katika viwanja nchini, lakini inakuwaje wachukue uamuzi wa kipuuzi kama huo kwa kuwa eti mwamuzi ameharibu na kuwavuruga wao? Viti na mwamuzi vinahusiana vipi?

Viti havihusiki na mpira unaochezwa, havihusiani kabisa na kipenga kinachopulizwa na mwamuzi. Sasa kwa nini mwenye hasira akimbilie kung’oa viti huku akijua wazi uharibifu wake ni hasara kwa taifa letu na si mwamuzi au TFF kama ambao ndiyo wamemuudhi?

Labda mnakuwa wasahaulifu na wakati mwingine hamhitaji kujikumbusha masuala ya msingi kabla ya kuchukua uamuzi kama ambao mmekuwa mkifanya kwa kuwa mnatumia nafasi ya wingi wa watu ili kujificha na kuepuka kukamatwa.

Lakini ukweli ninawakumbusha kuwa, pamoja na ukongwe wa klabu zenu ambazo zimeanzishwa katika miaka ya 1930, hadi sasa hakuna iliyothubutu kuweka hata nusu ya kiti cha plastiki ikasema ni maandalizi ya kujenga uwanja.

Tunajua Yanga na Simba wote wameshatuonyesha ramani ya viwanja vyao na hakuna hata kimoja ambacho kimeanza kujengwa, badala yake ni kwamba, ujenzi huo unaonekana kubaki kwenye makaratasi.
Kama klabu zenu ambazo mnaamini ni kubwa na lazima zishinde kila mechi hazina hata harufu ya kumiliki viwanja, vipi mfikie kubomoa viwanja ambavyo vimejengwa kwa nguvu ya wananchi wote wa Tanzania?

Tanzania imepata msaada kuujenga uwanja wake, lakini nusu fedha zimetolewa na serikali, inakuwaje mfanye uharibifu kwa sababu ambayo haihusiani na uwanja? Au ndiyo tabia za kipuuzi za kuiga mambo ya Ulaya, eti kwa kuwa mashabiki wakikasirika wanavunja viti, basi Wabongo nao lazima muige! Huo ni utumwa wa mawazo.

Tunakwenda mbele kwa kutaka kupambana ili kufanya tuende na dunia ya sasa katika suala la maendeleo. Lakini mnaturudisha nyuma au mnataka tuwe na viwanja ambavyo watu wakiingia kushuhudia mechi wanakaa kwenye mikeka?

Badilikeni, hasira za dakika mbili hazina sababu ya kusababisha uharibifu na kingine mjenge tabia ya kuziachia mamlaka husika kushughulikia matatizo yanayotokea, ndiyo maana kuna waamuzi wanafungiwa na kadhalika.

Tunahitaji kwenda mbele, ukarabati wa Uwanja wa Taifa kila kukicha hautatusaidia kwenda mbele. Badala yake tunatakiwa kuwa watu tunaofikiri wakati mwingine kabla ya kutenda, vizuri kutafakari faida na hasara. Jiulize kama kuna usahihi wa kuvuka barabara ukiwa umefumba macho!

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic