November 20, 2013




Na Saleh Ally
UNAWEZA kuona kama ni miujiza lakini hali halisi inaonyesha kuwa, mambo mengi yanayotokea ndani ya Simba yanaashiria timu hiyo imekuwa haina uhakika wa mambo inayoyafanya kwa kipindi chote cha misimu miwili.


Baada ya kwisha kwa msimu uliopita, Simba ndiyo ilikuwa timu iliyofanya usajili wa wachezaji wengi chipukizi, ilisajili wachezaji zaidi ya kumi ikiwa ni pamoja na kuwapa mikataba wachezaji wake chipukizi waliokuwa wakiitumikia bila mikataba.
 
LIEWIG

Lakini hilo halikuwa kubwa sana zaidi ya namna timu hiyo inavyotimua makocha na sasa imeweka rekodi mpya ya kufanya kazi na makocha wanne katika kipindi cha misimu miwili.
Simba imemtangaza kocha mpya, Zdravko Logarusic, raia wa Croatia, ambaye sasa anachukua nafasi ya Abdallah Kibadeni aliyeifundisha Simba kwa nusu msimu tu.

Kabla ya Kibadeni, Simba ilifundishwa na Patrick Liewig, raia wa Ufaransa, ambaye alichukua nafasi ya Milovan Cirkovic.

Sasa Simba imemtangaza kocha mpya, Zdravko Logarusic, raia wa Croatia, ambaye anakamilisha idadi ya makocha wanne katika kipindi cha misimu miwili.
MILOVAN AKISAINI SIMBA MBELE YA RAGE (KULIA)

Maana yake kila kocha amefundisha nusu msimu, kwa Logarusic ambaye alikuwa akiinoa Gor Mahia ya Kenya, kikubwa ni kumuombea aumalize msimu.
Rekodi nyingine ya Simba ni kwamba, katika misimu miwili, imefundishwa na makocha kutoka katika nchi nne tofauti.
Milovan kutokea Serbia, Liewig wa Ufaransa, Kibadeni ambaye ni mzalendo na Logarusic anayekuja ambaye anatokea Croatia.
Hakuna kocha ambaye angedumu milele katika kikosi cha Simba, lakini inaonekana hata uongozi wa klabu, hasa ule wa juu, ulikuwa tatizo kubwa.
Mfano, angalia kila ulipofika wakati wa kocha kuondoka, sababu zilionyesha kuwa na walakini. Hakuna ubishi, misimu miwili timu kufundishwa na makocha wanne tofauti inachanganya na inaonyesha kuna tatizo.

Milovan:
Msimu mmoja kabla alikuwa ameipa Simba ubingwa na kuiongoza kutoa kipigo cha aibu kwa Yanga cha mabao 5-0.
Lakini uongozi wa Simba ukamuondoa na kusema alikuwa mvivu, anashirikiana na wachezaji na timu yake ilikuwa nafasi ya pili katika msimamo. Ikashindwa kumlipa fedha yake hadi Rahma Al Kharusi ‘Malkia wa Nyuki’ alipojitokeza na kumlipa.

Liewig:
Mfaransa huyu alichukua nafasi ya Milovan, akafunga safari na Simba hadi Oman kwa kambi ya wiki mbili, aliporejea sera yake ikawa vijana zaidi na Simba ikaambulia kushika nafasi ya tatu nyuma ya Azam FC na mabingwa Yanga.
Uongozi wa Simba ukasema ataendelea kubaki, kosa ni alipofunga safari kwenda mapumzikoni kwao Ufaransa, akatumiwa salamu na barua ya kufutwa kazi.
Kwa kuwa alikuwa anadai alirejea, akalipwa nusu hadi ameondoka nchini baada ya kurudi mara ya pili, Liewig bado anadai dola 8,500 hadi leo.

Kibadeni:
Aliiongoza Kagera Sugar kushika nafasi ya nne nyuma ya Simba, ikaonekana anaweza na kupewa nafasi ya Liewig.
Naye ameifundisha Simba kwa nusu msimu tu, alianza mwanzoni mwa msimu huu, mwisho wa mzunguko wa kwanza, kikosi chake kimeshika nafasi ya nne nyumba ya Mbeya City, Azam FC na vinara, Yanga.

Logarusic:
Sasa ni zamu ya Logarusic, Kocha Bora Kenya msimu wa 2011/12, akiwa na Gor Mahia ya Kenya. Aliiwezesha kushika nafasi ya pili mara mbili, msimu huu alifundisha nusu msimu kabla ya nafasi yake kuchukuliwa na Bobby Williamson ambaye awali ilielezwa ndiye kocha mpya Simba kabla Championi halijakosoa na kuweka mambo sawa kwamba kocha huyo hakuwa na mpango wa kujiunga na Msimbazi.
Huenda kwa wachezaji waliokuwa Simba kwa misimu yote miwili, wanapaswa kuwa makini maana wanalazimika kutumia mifumo mingi kutoka kwa makocha wanne tofauti wenye asili ya nchi nne, si kitu rahisi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic