December 16, 2013




WATANZANIA tunasifiwa kwa uungwana, lakini sifa yetu nyingine inayosababisha mambo mengi tunayofanya yakwame ni woga, kitu kibaya sana.


Ukimuuliza mtu kwa nini ni muoga, hakika ufafanuzi unakuwa hauna nguvu za kukufanya kuamini kwamba mtu fulani alitakiwa kuwa muoga katika muda fulani, ujinga tu.
Wiki moja iliyopita, timu ya Zanzibar iliyoshiriki michuano ya Kombe la Chalenji nchini Kenya ilikuwa katika tafrani kubwa baada ya wachezaji wake kuzuiwa hotelini jijini Nairobi.

Wachezaji hao walizuiwa kwa kuwa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), lilishindwa kulipa gharama za hoteli.
Kutokana na hali hiyo, mmiliki wa hoteli hiyo akaamua kuwashikilia wachezaji, makocha na viongozi wa Zanzibar Heroes hadi hapo atakapopewa fedha zake.
Awali ilielezwa kwamba wachezaji hao walikuwa wakipewa ruhusa ya kwenda kuangalia mechi za michuano ya Chalenji iliyokuwa ikiendelea baada ya wao kutolewa.

Lakini baadaye, mmiliki wa hoteli akaingia hofu na kuamua kuwazuia kabisa hata kutoka nje na sasa wakawa kama wanyama au mifugo.
Mwisho tatizo hilo limemalizika kwa Cecafa kulipa bili ya hoteli iliyokuwa inadaiwa na Serikali ya Zanzibar kushughulikia suala la usafiri na timu hiyo imerejea nyumbani.

Kinachonishangaza ndiyo kile ambacho  nimeanza kukizungumzia, woga au inawezekana ni tabia ya kupuuzia tu mambo kutoka kwa viongozi wetu kuanzia wale wa Chama cha Soka Zanzibar (ZFA) na hata Serikali ya Zanzibar.
Kama ni tamko, basi ni ili mradi tu mtu amesema, hakuna anayeonyesha kiasi gani tumekasirishwa na uhuni huo wa Cecafa ambayo inaongozwa na Mtanzania, Leodeger Tenga.
Taarifa zinasema wakati matukio ya wachezaji na makocha wa Zanzibar Heroes kunyanyaswa namna ile yakitokea, Tenga hakuwa nchini Kenya na alifika siku ya fainali, siku ambayo hata Sudan waliocheza fainali na Kenya pia walizuiwa hotelini.
Hii si mara ya kwanza kwa baraza hilo kufanya mambo ya kipuuzi kama hayo ambayo hayapaswi kupewa nafasi kwa jamii na hasa katika masuala yanayohusisha utaifa.
Kuidhalilisha Zanzibar Heroes ni kuidhalilisha Zanzibar, lakini ni kuonyesha dharau kwa taifa la Tanzania pia. Sasa mbona mmekaa kimya na mnaona ni kama tukio la kufurahisha?
Cecafa wataacha lini mambo yao ya kubabaisha kila wakati kama hayo kama viongozi husika mnakuwa waoga kukemea na ikiwezekana hata kuhakikisha mnasisitiza Cecafa waombe radhi na ikiwezekana waahidi kwamba itakuwa mwanzo na mwisho?
Msimamo kwa lengo la kusimamia haki ni jambo zuri, uimara wa viongozi pia ni vizuri ukaonekana wakati kama huu taifa linapodhalilishwa tena na kikundi tu cha watu fulani.
Wachezaji wa timu ya taifa ambao ni askari wa taifa, wanawekwa rehani kama mifugo halafu linaonekana ni jambo la kawaida! Au mlitaka azuiwe mwanasiasa mmoja ili uwe wakati mzuri wa kupiga kelele na kujipatia ujiko?
Huu ndiyo wakati wa kuzima ubabaishaji wa Cecafa ili waachane na kuyafanya mataifa yetu kuanzia timu za taifa na ikiwezekana klabu zetu kuwa biashara yao kwa ajili ya kuwaingizia vipato.
Zanzibar au Tanzania kwa jumla ina uwezo wa kuikemea Cecafa, ikiwezekana kuipa onyo ili kuachana na ubabaishaji kama uliotokea ambao umewadhalilisha askari hao waliokuwa wanapigania nchi. Nawakumbusha, viongozi wao, pia ni tatizo katika maendeleo ya nchi.
FIN.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic