December 16, 2013

MKE WA MZEE SMALL, MAARUFU KAMA MAMA SAID



IJUMAA, Mzee Small alizungumzia namna alivyozushiwa kifo na kufurahishwa kwake na Watanzania walivyoonyesha kumjali baada ya kusikia taarifa hizo.

Lakini akasisitiza bado anaumwa, upande mmoja wa mwili wake umepooza na analazimika kutembea kwa kujivuta huku akitumia fimbo. Je, maisha yake yakoje? Endelea.


MZEE Small anasema maisha kwake ni magumu sana kwa kuwa wakati fulani alikuwa akiendesha maisha yake kwa kuuza maji kupitia visima vyake.


Sasa mambo yamekuwa magumu na hasa kutokana na gharama kubwa za matibabu ambazo amekuwa akitoa.

“Kama ulivyoona leo, ninakwenda kufanya mazoezi mara mbili kwa siku na kila ninapokwenda lazima bodaboda ije kunichukua na kunirudisha.

“Si kitu kidogo kwangu kwa kuwa sina sehemu inayoweza kuniingizia kipato kwa uhakika ili niweze kujihudumia katika kiwango kizuri na kwa asilimia mia.

“Ila ninasisitiza, sitaki kutangaza kwamba ninaomba msaada. Ninajua wako wenye mapenzi na mimi na wakijisikia kufanya hivyo basi nitafurahi.

“Naogopa kusema nisaidieni maana watu wana majukumu na matatizo yao, lakini kwa anayeona anaweza kufanya hivyo, nitajisikia faraja.

“Wakati mwingine hata mtu kama akitokea kunitembelea kama mlivyofanya nyie nafurahi.nasikia faraja sana,” anasema Mzee Small.

Hata hivyo, Mzee Small anasisitiza pamoja na shida zote anazopata, mkewe ni kama dereva wa kila kitu naye anamchukulia tena kama ndugu na si mkewe tu pekee.

Pamoja na hivyo, Mzee Small ambaye ni gwiji wa uigizaji nchini anaonyesha kuingia hofu na mkewe, kwamba anaweza kuchukuliwa na mtu fulani, halafu bila ya kusita anapiga mkwara mzito, tena hadharani.

“Mimi katika hili nitakuwa mkweli tu bila ya woga, kama nitasikia kuna mtu anataka kufanya ujanja na kumchukua mke wangu, sitachelewa, nakuambia namroga aokote makopo.

“Huyu mke wangu amekuwa akifanya kila kitu kwa ajili ya kuhakikisha napona. Sasa mimi namuona si mke tu, huyu ni kama ndugu yangu.

“Unajua anapambana, anafanya kila juhudi kuona nina nafuu na mambo yangu yanarejea katika hali nzuri. Sasa kama anatokea mtu anataka kumchukua unadhani nitafanya nini, maana nguvu za kupambana naye sina.

“Kilichobaki ni kumroga tu, hata ikiwezekana aokote makopo kama nitaweza kweli kufanya hivyo,” anasema Mzee Small, kawaida yake vituko haviishi (anaangua kicheko).

Pamoja na mkwara huo kuhusiana na mkewe, Mzee Small anasema amekuwa akishangazwa na baadhi ya ndugu zake kumtupia lawama mkewe.

“Wakati mwingine kuna baadhi ya ndugu zangu wamekuwa hawaelewi, wanamtumia mke wangu lawama nyingi sana,  wanahisi ananipotosha,” anasema.

“Si sahihi, maana hata baada ya kuzushiwa kifo, kuna ndugu walisema mke wangu ndiyo kasababisha, eti amekuwa akinipeleka sana kwenye vyombo vya habari, nasema si kweli.

“Wakati watu wanaanza kupiga simu, wote tulikuwa chumbani tumelala, hakuna aliyejua kati yetu. Nakumbuka mlikuwa wa kwanza kutaka kujua, mara tu baada ya kuzungumza nanyi, basi hatukulala tena, maana simu ziliendelea kutoka kwa watu mbalimbali ambao walitaka kupata uhakika.”

Kuhusiana na suala la matibabu, pamoja na mazoezi, Mzee Small amekuwa akihangaika kila aina ya tiba ilimradi apate kupona tu.

“Kuna kipindi nilipata mganga wa kienyeji kutokea Kigoma, alitaka nimuandalie sehemu ya kulala ili aje hapa anitibu. Nilifanya hivyo, lakini alipofika Dar, ilikuwa ni vituko na havina mfano wake, hadi nikakasirika.”

MZEE SMALL anasema mganga wa kienyeji aliyehamia kwake alizua vituko ambavyo havikuwa na mfano. Ni vituko vipi, mwisho wake ilikuwaje na alichukua uamuzi gani? ENDELEA KUFUATILIA KESHOKUTWA JUMATANO.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic