January 10, 2014



Na Saleh Ally
KUKAA nje kwa Lionel Messi kwa takribani miezi miwili sasa kumekuwa gumzo kubwa katika soka duniani.
Lakini juzi amecheza mechi yake kwanza tangu kurejea uwanjani huku karibu kila upande duniani ukiwa na hamu ya kutaka kujua kama kweli atakuwa sawa. Mechi hiyo ilikuwa ni ya Copa del Rey na Barcelona ilikuwa ikitoana jasho la Getafe na kufanikiwa kushinda kwa mabao 4-0.
Messi raia wa Argentina anaaminika ndiye mchezaji bora zaidi katika kipindi hiki ingawa kumekuwa na mjadala wa kila aina.
Kurejea kwake na mabao mawili kumezua mengi, lakini kufunga tu hakujawa sababu ya gumzo, badala yake kweli yuko fiti.
Kuonyesha kweli yuko fiti, Messi aliingia katika dakika ya 61 kuchukua nafasi ya Andres Iniesta, halafu akafanikiwa kufunga mabao hayo mawili huku akionyesha uwezo wake kama ilivyozoeleka.
Kimahesabu, Messi amecheza dakika 29 na kufanikiwa kufunga mabao mawili, hakuna ubishi sasa yuko fiti.
Lakini kivutio kingine ni kwamba, Messi amefunga mabao hayo mawili ndani dakika tatu tu. Bao moja katika dakika ya 89 na dakika za nyongeza.
Hali hiyo inaonyesha mambo mawili, kwamba yuko fiti kweli kimwili na kisaikolojia, lakini ana uwezo wa kucheza kwa kasi zaidi kila muda unavyosonga uwanjani, ndiyo maana akafunga hata kipindi ambacho mpira unakwisha.
Inaonyesha kiasi gani dunia ilikuwa inamsubiri Messi kwa hamu kubwa kwa kuwa vichwa vya habari vya kila aina vyenye ufundi wa aina yake vilitundikwa kwenye magazeti na runinga mbalimbali.
Inakadiriwa zaidi ya vichwa vya habari 200 viliandikwa kutoka katika vyombo mbalimbali vya habari kama runinga na magazeti katika mabara ya Ulaya, Amerika Kaskazini na Kusini. Huenda kesho vikaongezeka kupitia magazeti ya Tanzania na kwingineko Afrika na Asia.
Hata magazeti yenye mtazamo au upinzani na Catalonia anakotokea Messi kama lile la Marca ambalo liko jijini Madrid lilikubali kuweka kichwa kikubwa cha habari: “Messi amerudi”, halafu likaongeza: “Alihitaji chini ya nusu saa kuonyesha yuko fiti.”
Upande wa eneo la Catalonia ndiyo usiseme, vichwa vya habari hadi vilivyoonekana kukiuka maadili ya uandishi vilitupiwa kwenye magazeti kadhaa.
Lakini mengi yalieleza kurejea kwa “Masta” au “Mfalme”, huku vyombo hivyo vikisifia namba alivyoonyesha uwezo mkubwa pia kufunga mabao mawili ndani ya dakika tatu na moja akiwa ‘amewakokota’ mabeki wawili kabla ya kufunga kiufundi.
Ajabu zaidi ni vichwa vya habari lukuki kutoka barani Amerika Kusini ambako mchezo maarufu zaidi ni ule wa mpira wa kikapu.
Lakini gumzo lilikuwa ni mabao mawili ya Messi ndani ya dakika tatu na sekunde 31, huku wachambuzi wakisisitiza ni mchezaji wa kipekee na hakuna wa kumfananisha naye.
Runinga maarufu ya michezo ya ESPN na ile kubwa namba moja duniani kwa habari ya CNN, zilitenga muda maarufu kuelezea kurejea kwa Messi na alichokifanya katika mechi hiyo ya Copa del Rey.
Kwao Argentina hasa katika mji aliozaliwa wa Rosario mambo yalikuwa tofauti, wengi waliisubiri mechi hiyo kama vile ni ya Kombe la Dunia, lakini walitaka kuhakikisha kama kweli Messi amerudi na anaweza kufanya makubwa.
Kila bao lake lilishangiliwa kwa nguvu na kelele zilisikika sehemu kadhaa za mji huo, Gazeti la The Buenos Aires Herald liliandika: “Kasi ya ajabu”, halafu likasema ni ahueni kwa Kocha Gerardo Martino katika mechi ya kesho Jumamosi dhidi ya wakali Atlético Madrid. Gazeti la Argentine Daily Olé likaandika kichwa: “Muuaji kazini”.
Messi aliumia Novemba 10, mwaka jana na tokea hapo ilionekana La Liga imedorora kwa kuwa Cristiano Ronaldo hakuwa na mpinzani wa kumtoa jasho na hata Diego Costa wa Atletico Madrid alipofanya vizuri alionekana si saizi yake.
Messi amekuwa na sifa ya kutoumia mara kwa mara, huenda ndiyo maana imekuwa gumzo kutokana na kuumia kwake. Hata hivyo bado ana muda wa kuthibitisha kama kweli yuko sawa na mechi ya kesho dhidi ya Atletico Madrid inaweza kutoa majibu.
Kwa sasa Messi na Ronaldo ndiyo wachezaji wanaotupiwa macho na kutegewa masikio zaidi mwingine yoyote kwa sasa.
Kurejea kwake, hivi karibuni kutaanza kurudishwa kwenye ushindani dhidi yake na Ronaldo anayepewa nafasi zaidi ya kutwaa tuzo ya Ballon d'Or.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic