February 26, 2014



Na Saleh Ally
AL AHLY ndiyo habari ya mjini na tayari wako jijini Dar es Salaam baada ya kuwasili leo alfajiri kwa ndege ya Shirika la Ndege la Misri au Egypt Air wakitokea kwao Cairo.

Mabingwa hao wa Afrika wako jijini Dar es Salaam, kuwavaa mabingwa wa Tanzania, Yanga, katika mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa kabla ya kurudiana wiki moja baadaye jijini Cairo.

Yanga haijawahi kuifunga Al Ahly tangu zilipoanza kukutana, ushindi dhidi ya Waarabu hao wa Afrika Kaskazini huwa ni sare. Katika mechi itakayopigwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, watakachotaka Yanga ni kusonga mbele.
Kusonga mbele kwa Yanga lazima kusiwe na miujiza, badala yake ni kuhakikisha wanavunja rekodi kwa kuifunga Ahly katika mechi ya kwanza hiyo Jumamosi kabla ya kupanga itapambana vipi jijini Cairo.

Kuwang’oa vigogo hao si kazi ndogo, lakini katika soka hakuna linaloshindikana na kama Yanga wakijipanga vilivyo, basi watakuwa na uwezo wa kuwaondoa, lakini ni lazima washinde mechi ya Dar es Salaam.

Ahly ni bahari, kuishinda kunahitajika mipango mingi na lazima iwe kuanzia nje, yaani kabla ya mechi na wakati wa mechi. Moja ya mbinu zao ni kugomea, kupoozesha mchezo, kupoteza muda hasa wakianza kufunga na kushambulia kwa kushtukiza.

Wao pamoja na kwamba watakuwa ugenini, lakini wana mifumo mingi ambayo wataifanya kuhakikisha wanashinda au kupata sare ya ugenini ili kujiweka katika nafasi nzuri.
Wanapokuwa ugenini, mara nyingi wakifungwa ni sare na wanapokwenda kwao, basi wanahakikisha wanashinda. Mifumo ni mingi kuhakikisha wanapata sare hiyo na utaona wanapocheza kuwa ni watu waliojipanga na wanajua wanachokifanya.
Vurugu:
Yanga wanapaswa kuwa makini na mambo mengi, kuanzia nje ya uwanja ni namna ambavyo Waarabu hao wanakuwa na vituko, wanaotaka kuonyesha kwamba wanaonewa, hawajaridhika na wanatumia muda mwingi kusababisha hali ya mabishano.
Utaona watataka kukataa basi, watasisitiza hawataki hoteli, hawamtaki mtu fulani waliyepewa, wanaweza kubeba maji yao, ikiwezekana hata chakula na wakati wa kupikiwa lazima awepo mtu wao.
Wanachotaka kufanya ni kuona nguvu nyingi ya wenyeji wao inawalenga wao, Waingereza wanasema attention. Yaani mnaelekeza akili yote kwao, kumbe wao wameshafanya maandalizi ya kutosha.
Wanaamini kunapokuwa hakuna utulivu, ni rahisi wao kupanga au kung’amua ni nini cha kufanya. Hivyo Yanga lazima wawe watulivu kama walivyofanya Simba mwaka 2003, Zamalek ilitua Dar es Salaam ikakutana na kipigo cha bao 1-0, mfungaji akiwa Emmanuel Gabriel ‘Batigol’.

Dawa:
Tabia za timu nyingi za Kiarabu ni ujanja nje ya uwanja, kingine ambacho kinatumika ni moja ya dawa ambayo hupunguza nguvu ya mtu kama akiivuta na lazima Yanga wawe makini hata wakiwa nyumbani.
Mwaka 2009, wakati Taifa Stars inafuzu kwenda kucheza Chan nchini Ivory Coast, iliitoa Sudan, wakati huo kukiwa hakuna Sudan Kusini.
Wakati wa mechi ya Dar es Salaam, Wasudani walijaribu kufanya mchezo huo, wakashitukiwa. Wakiwa kwao Khartoum, pia walifanya hivyo kwa kupulizia dawa kwenye lifti wakati wachezaji wa Stars wakishuka kwenda kwenye mechi. Watu wakashituka, wachezaji wakatumia ngazi kushuka chini.
Uwanjani:
Waarabu hao wameshinda makombe zaidi ya 10, kama utachukua ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Kombe la Washindi na Kombe la Shirikisho. Hakuna ubishi wana mbinu zote.
Lazima Yanga wawe makini kwa kila hatua, wanaposhambulia na wanaposhambuliwa kwa kuwa Ahly wanajua wanafanya nini kila wanapokuwa na mpira au hawana.

Kupoza:
Wana tabia ya kupoza mpira, hasa wanapokuwa wakicheza ugenini. Halafu wanafanya mashambulizi ya kushitukiza, wakikufunga, wanarudi nyuma.

Faulo:
Wana sehemu zao wanazotaka kufanyiwa madhambi, wanalazimisha kuguswa hasa wanapokuwa nje ya 18. Wakipata faulo eneo hilo, hasa kwenye kona ya msitari wa 18, wana watu maalum kwa ajili ya kazi hiyo, hivyo lazima Yanga wawe makini.

Aboutrika:
Mohammed Aboutrika amestaafu akiwa na miaka 34, ingawa umri wake ulikuwa umekwenda, lakini ukweli ni ahueni kwa Yanga.
Ufundi wake ulikuwa wa juu, mechi mbili za fainali za Ligi ya Mabingwa dhidi ya Orlando Pirates, zote mbili alifunga. Alianza kufunga bao nchini Afrika Kusini wakati walipopata sare ya 1-1. Waliporejea Cairo, wakashinda kwa mabao 2-0, yeye akiwa ametupia la kwanza.

Ameamua kustaafu, lakini kuna wengine kama Gedo na Emad Motaeb anayevaa jezi namba 9, bado wanatakiwa kuchungwa sana.

Zote hizo ni mbinu za ushindi, lakini ukifuatilia zinaendana na umakini wa nini cha kufanya. Kama wawakilishi hao wa Tanzania wakiweza kushinda Dar es Salaam, kitu ambacho kinawezekana kama wakiwa makini kweli basi lazima wajipange nje na ndani ya uwanja, maana Waarabu hao wako makini sana.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic