February 14, 2014


Na Saleh Ally
YANGA ina kila sababu ya kusema sasa inatakiwa kuwa katikati ya maandalizi ya kutosha dhidi ya mabingwa wa Afrika, Al Ahly ya Misri kwa kuwa si timu ya mzaha.


Mechi yao itakuwa Jumamosi, Machi 8, kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam na kurudiana ni jijini Cairo siku chache baadaye, hakuna haja ya kuficha mambo kwa madai ya kutaka kuwapa Yanga moyo, badala yake ukweli ni huu, haitakuwa mechi lelemama.

Wakati Yanga inakwenda kumalizia mchezo wake dhidi ya timu dhaifu ya Komorozine ya Comoro, Jangwani wataanza rasmi Ligi ya Mabingwa Afrika watakapokutana na wababe hao wa Afrika, ambao usipokuwa makini, utawadharau kwa mengi, lakini si kwamba hawafungiki.
Al Ahly wameonyesha hawafanyi utani katika suala la ushindi, angalia pamoja na kwamba Yanga inaweza isiwe timu tishio kwao kwa maana ya uzoefu au mafanikio katika michuano hiyo ya Afrika lakini wameshaanza kutuma watu kufuatilia mwenendo wa Yanga na huenda wanafanya zaidi ya hapo. Hadi sasa hatujui, lakini inawezekana wanafuatilia mambo mengine kwa kuwa kweli wanataka kuvuka na kusonga mbele.

Wakati Yanga ina takribani mwezi mzima kabla ya kuwavaa wababe hao wa Afrika, burudani katika soka zitakapokutana timu hizo ni suala la umri na uzoefu baina ya wachezaji wa Yanga na wale wa Al Ahly.
Moja ya sifa kuu ya Al Ahly ni kuwa na wachezaji wenye umri mkubwa lakini wanaoendelea kuitumikia na kufanya vizuri, kwani hakuna aliyetarajia kama wangeweza kubeba ubingwa wa Afrika wakiwa na lundo la “watu wazima”.
Idadi kubwa ya wachezaji wake nyota ni wale wanaozidi umri wa miaka 30, lakini bado wako fiti na wamekuwa wakiendelea kufanya vizuri katika anga za kimataifa na tishio katika soka la Afrika. Hesabu zinaonyesha zaidi ya wachezaji 12 wa Al Ahly wanazidi miaka 30.
Mwaka 2006, Mohamed Barakat alikuwa kati ya wachezaji wa timu ya taifa ya Misri iliyotwaa ubingwa wa Afrika kwa kuifunga Ivory Coast jijini Cairo, lakini bado ameendelea kuichezea timu yake ya Al Ahly hadi leo na sasa ana umri wa miaka 37.
Jaribu kupata picha, Barakat akiwa anachuana na David Luhende wa Yanga mwenye miaka 22 na akafanikiwa kumshinda, tofauti yao ni miaka 15. Lakini leo wanapambana na huenda Barakat akaonekana ni bora.
Kuna nyota mwingine, Mohamed Aboutrika, umri wake ni miaka 35, lakini ndiye atakuwa akipambana na Frank Domayo ambaye atakuwa akitofautiana naye kiumri kwa zaidi ya miaka 13, inaonyesha kuna jambo la kujifunza.
Kwamba wachezaji wa Al Ahly wanajitunza na kuthamini kazi yao, ndiyo maana wanaweza kudumu kwa kipindi kirefu wakiendelea kufanya vizuri huku wakiwashangaza wengi barani Afrika na duniani kote.
Wakati mwingine hata wachezaji kutoka Bara la Ulaya wameshindwa kudumu katika soka kwa muda mrefu kama ilivyo kwa wachezaji wa Misri ambao wanasifika kwa kuwa makini kwa kazi yao, na inaelezwa kutoendekeza starehe kupita kiasi hasa uzinzi na ulevi kupindukia, kunawasaidia kudumu kwa kipindi kirefu.
Kweli mwenendo wa Al Ahly si mzuri katika Ligi Kuu ya Misri, hata mechi ya mwisho imetoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Al Ittihad lakini iko katika nafasi ya pili, unaweza kusema haifanyi vibaya maana hata Yanga iko katika nafasi ya pili kwenye msimamo hapa nyumbani.
Mara ya mwisho Yanga kucheza na Al Ahly ilikuwa mwaka 2008 kwenye Uwanja huo wa Taifa jijini Dar na wachezaji waliokuwepo na kucheza wakati huo na wapo hadi sasa katika kikosi cha Yanga ni Juma Kaseja, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Athumani Idd ‘Chuji’, Mrisho Ngassa na Jerry Tegete.
Al Ahly ilishinda kwa bao 1-0 lililofungwa na mshambuliaji Mreno, Flavio aliyepata pasi ya Aboutrika. Kwa upande wa Yanga, Kaseja alikuwa langoni, Cannavaro, Ngassa na Chuji walimaliza dakika 90, Tegete aliingia kuchukua nafasi ya Boniface Ambani ambaye siku hiyo soka lilimkataa.
Kama Yanga ni watano tu waliokuwepo kipindi hicho, Al Ahly wanarudi na takribani wachezaji 10 waliokuwa katika kikosi kilichoing’oa Yanga. Maana yake ni watu wanaoelewana, wanaopanga kinachoeleweka na pamoja na umri wao, bado watatoa upinzani.
Changamoto zote ni sehemu ya Yanga kuangalia namna ya kujipanga, jamaa wana uwezo lakini Yanga ina timu nzuri na inaweza kufanya vema hasa kama watajiamini kuwang’oa inawezekana, lakini isiwe kwa maneno tu.

MSIMAMO MISRI
                                           P        Pts
Al Mokawloon                   8          16
Al Ahly                              8            16
Smouha                               7         16
Al Ittihad                            8          12
Misr Lel Makasa                  8            11

MSIMAMO TANZANIA BARA
                                               P           Pts
Azam                                    16           36
Yanga                                  16          35
Mbeya                               17         34
Simba                                17          31
Coastal                             17             22



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic