February 10, 2014


 Na Saleh Ally
MWENDO wa kocha Jose Mourinho ulianza taratibu sana huku ikionekana kama vile ’amebugi’ kwa vile Ligi Kuu England ni ngumu zaidi, tofauti na wakati alipokuwepo.


Kadiri siku zinavyosonga mbele, kikosi chake kimekuwa kikiimarika na hakuna ubishi ndani ya mwezi mmoja tu, kimeishachukua nafasi inayoonyesha kuwa wana nafasi ya kubeba ubingwa wa England msimu huu.

Mourinho anaonekana ana nafasi ya kutwaa ubingwa kutokana na namna kikosi chake kinavyozidi kuonekana tishio lakini sifa nyingine ni ukubwa wa kikosi.

Chelsea na Manchester City ndizo timu zisizoweza kuyumbishwa na majeruhi kwa kuwa zina rundo la wachezaji mahiri na wengi kwenye  safu zote, yaani beki, kiungo na ushambuliaji.

Mfano, Arsenal au Liverpool, ikitokea wachezaji wawili tu wa kikosi cha kwanza wameumia, basi tatizo litakuwa kubwa maradufu kuliko inavyoweza kuwa kwa timu hizo mbili.

Hesabu za Mourinho kutoka Ureno zimekuwa tofauti na makocha wengi, amekuwa akijitahidi kujenga uwezo mkubwa wa kipumzi hata kabla ya kuanza mashindano.
Mfano, alikuwa akisajili kikosi kikubwa, hali iliyowashangaza wengi kwa kuwa waliona ni kama matumizi mabaya ya fedha.

Lakini faida yake inaanza kuonekana katika hatua za mwisho.
Mourinho kama ameingia katika mbio za kuwania ubingwa, hakuna ubishi atakuwa msumbufu kwa kuwa pamoja na uwezo mkubwa kimbinu, ana kikosi kipana na anaweza kubadilisha nusu yake kikafanya vizuri.
Upande wa kikosi, mfano kwa mabeki na viungo wakabaji kuna nyota kama John Terry, Garry Cahill, Branislav Ivanovic, Ashley Cole, Cesar Azpilicueta, David Luiz, Ramirez, Mikel Obi, Nemanja Matic na wengine, anakuwa na uhakika hata wa mechi kumi mfululizo. Kiungo ndiyo amejaza watu lukuki kama akina Eden Hazard, Oscar, Willian na Frank Lampard.

Lakini angalia washambuliaji, Mohammed Salah, Samuel Eto’o, Demba Ba, Fernando Torres, Andre Schurrle na baadhi ya chipukizi.
Ratiba ya mechi za mwisho kwa Chelsea ni dhidi ya West Brom, Man City (Kombe la FA), Everton, Galatasaray (Ligi ya Mabingwa), Fulham halafu Tottenham. Kwa kikosi chake hakutakuwa na usumbufu mkubwa.

Kwa mfumo Mourinho amekuwa kimya lakini ameibukia katika kipindi mbio zinaenda ukingoni, wakati wanashtuka kuwa ni hatari, tayari amepanga jeshi lake vizuri na ameshakuwa msumbufu.
Tayari Mourinho na kikosi cha Chelsea wanaonekana ni washindani hatari na wenye nafasi ya kutwaa ubingwa. Lakini mambo mengi Mourinho aliyafanya akionekana kama anakosea au ameshindwa na ugumu wa Premiership msimu huu, lakini sasa mambo ni tofauti kabisa.
Man City ya Manuel Pellegrini hawana tofauti kubwa na Chelsea, angalau wana kikosi chenye wachezaji wengi wenye uwezo na wanaweza kutoa msaada hadi mwisho wa ligi.

Arsenal si dhaifu, lakini haina kikosi kipana chenye wachezaji wengi wazoefu, pia angalia ratiba yao, ni hatari na vigumu kwao kupambana nayo hadi mwisho. Na kama Arsenal watafeli, hali kadhalika Liverpool, basi ubingwa utakwenda kwa timu kati ya Chelsea au Man City ambazo zinavaa jezi za bluu.

Angalia ratiba inavyoiangusha Arsenal na kuitupa kwenye wakati mgumu sana; keshokutwa Jumatano, inakutana na Manchester United, kweli itakuwa nyumbani Emirates lakini kumbuka inatokea katika majeruhi ya kupigwa mabao 5-1 na ndiyo gumzo sasa katika soka England na duniani kote.

Mara tu baada ya mechi hiyo, Arsenal haitakuwa na muda wa kutosha kupumzika kwa kuwa siku tano baadaye inakutana na Liverpool katika mechi ya Kombe la FA, hii ni mechi kubwa.
Siku tatu baada ya mechi hiyo, Arsenal watacheza tena Emirates dhidi ya mabingwa wa Ulaya, Bayern Munich ambayo ndiyo inaaminika kuwa na kikosi bora zaidi barani humo kwa kipindi hiki.

Arsenal watamaliza Februari kwa kucheza na Sunderland tarehe 22, baada ya hapo Machi Mosi ndiyo watakuwa wanarejea dimbani kuwavaa wabishi Stoke City. Machi 8 wanaivaa Swansea na mwezi huohuo tena wanacheza na Bayern Munich mechi ya pili, safari hii wakiwa Ujerumani.

Achana na ugumu wa mechi hizo ngumu na mfululizo, Arsenal katika mwezi huohuo wana mechi nyingine ngumu Machi 16 dhidi ya Tottenham na Machi 22 dhidi ya Chelsea. Halafu watafunga mwezi na mechi dhidi ya Man City.

Ratiba hii si rahisi kwa Wenger, maana yake inatoa nafasi kwa Chelsea na Manchester City kuwa na nafasi na kutwaa ubingwa.

 Liverpool wenyewe nao mambo siyo rahisi sana kwani itacheza na Fulham, Arsenal, Swansea, Man United na Cardiff katika mechi zinazofuata.

City ya Pellegrini, nayo haina ratiba ngumu ya kutisha mwishoni ambayo itacheza na Sunderland, Chelsea, Barcelona (Ligi ya Mabingwa), Stoke, Sunderland, Aston Villa, Barcelona tena, halafu Hull City.

Mpira una mambo mengi sana yanayoshangaza, yasiyoaminika na yanayoshtukiza, ndiyo maana hakuna anayeweza kujiamini.
Ingawa timu zenye rangi ya bluu zinapewa nafasi kubwa kutokana na hali halisi, lakini mambo yanaweza kugeuka ikitokea upande mmoja ukazubaa au kulala.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic