Na Saleh
Ally
WAYNE
Rooney amekuwa mchezaji wa sita wa Manchester United kufikisha mechi 300 za
Ligi Kuu England, akiwa na timu hiyo.
Lakini
rekodi hiyo si gumzo sana kama ile ya mkataba wake mpya ambayo unakwenda hadi
2019, kwani amesaini mkataba wa miaka mitano na nusu na atakuwa akilipwa pauni
300,000 (zaidi ya Sh milioni 750) kwa wiki.
Kwa
Ulaya, mjadala mkubwa umekuwa ni sababu zipi Manchester United imekubali kulipa
fedha nyingi kiasi hicho kwa ajili ya Rooney, maarufu kama Wazza wakati hakuwa
na kiwango kizuri msimu uliopita hadi ikaelezwa alikuwa na mpango wa kwenda
Chelsea.
Kiwango
hicho cha juu kabisa duniani ni gumzo, lakini inaonekana Manchester walikuwa na
kila sababu ya kufanya hivyo kwa kuwa hawapo katika hali nzuri na usingekuwa
wakati mzuri kumpoteza Rooney.
Dalili
zinaonyesha wako katika wakati mgumu na huenda miezi minne ijayo watakuwa
katika foleni wakisubiri ratiba ya michuano ya Europa League badala ya Ligi ya
Mabingwa Ulaya. Kumpoteza Rooney ni sawa na kupotea njia mara mbili.
Lakini
ndani ya mkataba huo, inaonyesha Manchester United itaendelea kubaki na haki za
mauzo ya picha ya Rooney, kitu ambacho kitaisaidia kuingiza mamilioni ya pauni
na kuisaidia kuweza kumlipa Rooney kiwango hicho bila ya kutetereka.
Kwa
kifupi, pamoja na kiwango, lakini Manchester katika wakati mgumu kama huu,
ilikuwa inahitaji jina la mtu kama Rooney kuendelea kuonyesha iko imara, ina
uwezo kifedha na ina wachezaji nyota na wenye majina makubwa.
Yote
hayo yatabaki kuwa kati ya Rooney na Manchester United, lakini malipo ya juu
kama hayo ya Rooney au yale ya Cristiano Ronaldo na Real Madrid au manunuzi ya
Gareth Bale ya pauni milioni 86 kutoka Tottenham kwenda Real Madrid,
yanaonyesha soka ni biashara kubwa sana hapa duniani.
Mshahara
wa pauni 300,000 kwa wiki, nani atalipwa? Hata awe profesa wa chuo kikuu
maarufu kuliko vyote duniani, haitawezekana, lakini Rooney anapata kwa wiki.
Fedha
anazolipwa kwa wiki, huenda zina nafasi ya kutatua matatizo makubwa zaidi ya
Yanga na Simba kwa muda mrefu na wakayasahau milele.
Mfano
sasa zimekuwa katika mchanganuo wa mambo mengi sana, kwamba klabu zina mipango
ya kisasa na zinataka kubadilika. Yanga na Simba ndizo timu kongwe zinazotia
aibu kuliko zote kwa kipindi kirefu.
Hazina
hata uwanja wa mazoezi, zinafanya mazoezi kwa kukodi. Hazina tofauti na wakazi
wengi wa Dar es Salaam ambao maisha yao ni kupanga. Angalau wao wanaweza kusema
ugumu wa maisha, lakini Yanga, Simba zina uwezo wa kuingiza fedha na kucheza
viwanja angalau vya mazoezi.
Gharama
zinaonyesha hivi, uwanja hasa wa nyasi bandia unaweza usizidi Sh milioni 150.
Maana yake Yanga na Simba zinahitaji angalau Sh milioni 300 tu kwa zote mbili,
kumaliza milele matatizo ya kutokuwa na viwanja hata vya mazoezi tu.
Mshahara
wa wiki wa Rooney unaweza kuwajengea uwanja wa mazoezi Yanga na ndugu zao
Simba. Lakini jiulize, kwa nini fedha za kwenye soka ifikie upande mmoja fedha
ya wiki inaweza kutatua matatizo ya milele kwa upande mwingine?
Ukweli
ni kwamba wapo wanaouchukulia mchezo wa soka ni biashara kubwa ambayo si ya
kuifanyia mzaha, ndiyo maana kuna wachezaji wanaoweza kulipwa fedha za kufuru
kama Rooney na Ronaldo au wanaweza kununuliwa kwa vitita vikubwa kama Bale.
Hapa
nyumbani, hakuna wanaoona hivyo na kama wapo ni wachache na wamekuwa
wakikatishwa tamaa na wengi ambao ni wagumu kuelewa na bado wanaamini Yanga na
Simba ni kwa ajili ya kuburudisha mioyo tu pale zinaposhinda.
Hakuna
atakayekataa kama Yanga na Simba zinafanya biashara ya soka, lakini haziko
makini. Ndiyo maana mambo yamekuwa ya kubahatisha zaidi.
Kutokuwa
na uwanja hata wa mazoezi ni sehemu ya kuonyesha kiasi gani timu hizo haziko
makini au si zilizopania kupata mafanikio kiutendaji na badala yake kushinda
pekee ndiyo kunabaki kuwa mafanikio A na Z.
Hakuna
kiongozi wa Man United anayeweza kutoa hata senti yake mfukoni kumlipa Rooney.
Fedha zote zinatokea kwenye mfereji wa mipango ambao unatokana na umakini wa
klabu hizo. Kweli huko ni England, sawa. Lakini hapa basi Yanga na Simba
zifikie hata robo ya hapo!
Angalau
kupitia njia ileile ya kuuza jezi, kuyashawishi makampuni makubwa kuidhamini,
kusajili timu bora inayofanya vizuri ili kuvuta watu wengi uwanjani. Pia
kusaini mikataba ya uhakika ya haki za runinga. Basi, fedha za kuwalipa
wachezaji, kujenga viwanja na maendeleo mengine, haziwezi kuwa vikwazo.
Viongozi
wa Yanga, Simba zenye utajiri wa watu wanaosubiri kununua au kulipia chochote
kutoka katika klabu hizo lakini hawakipati, wasishangilie fedha za Rooney kama
gumzo la vijiwe vya kahawa. Badala yake ziwaumize na waanze kutafakari angalau
kwa tundu dogo tu, walitumie kama njia ya kutokea walipokwama miaka nenda rudi.
0 COMMENTS:
Post a Comment