March 31, 2014


Soka inaweza kusaidia mapambano dhidi ya mauaji ya tembo
Tanzania imekuwa katika kampeni kubwa ya kupambana na mauji ya wanyama aina ya tembo ambao kadiri siku zinavyosonga mbele imekuwa ikionekana kuwa watatoweka.

Tembo wanauawa kwa kuwa kuna watu wanaingiza mamilioni ye fedha kutokana na kuuza pembe zao, hii inaonyesha kiasi gani watu wanaweza kuwa wanyama kwa ajili ya kujali maslahi yao na si ya taifa au uhai wa wanyama hao.

Ubinafsi ni sehemu ya sifa ya binadamu wengi, nianze kwa kusisitiza hivi; kama kuna mtu anashiriki katika hilo basi aamini anachofanya si sahihi na hana sababu ya kuendelea, ambaye alikaribia kuingia kwenye mkumbo huo, aachane nao kwani dili ziko kibao ambazo si lazima kuua.
Unaweza kushangaa vipi leo Metodo imehamia huku, lakini lengo ni kuweka msisitizo kuhusiana na wanyama hao ambao ni urithi wa taifa letu na wanamhusu kila mmoja.
Nchi nyingine hazina tembo, usijali ziko Afrika au Ulaya. Lakini Tanzania tumepata bahati hiyo kutoka kwa Mwenyezi Mungu, hivyo ni lazima tupambane kuhakikisha tunalinda uhai wao kutoka kwa majangili ambayo ni miongoni mwetu kama jamii.
Lakini kingine ambacho kimenivutia ni namna ambavyo wanaopiga kampeni ya kupambana kuielezea jamii ubaya wa kinachofanyika na kuwataka wananchi kuungana na serikali kupambana na watu hao.
Wanatumia njia mbalimbali kama za matangazo na mambo mengi, lakini michezo imesahaulika na imekuwa ni kawaida kwenye kampeni mbalimbali muhimu.
Michezo ina nguvu hata kuliko wanasiasa wengi, hivyo inaweza kupewa nafasi ya kuzitangaza kampeni za kupambana na ujangili na ikiwezekana wanamichezo mbalimbali wakiwemo wa soka wakapewa nafasi ya kuziongoza kampeni hizo kwa jamii.
Soka imetumika sehemu mbalimbali kurudisha amani kwenye jamii, mfano Rwanda ambako baada ya mauaji ya kimbari mwaka 1994. Soka ni sehemu ya njia iliyotumika kurudisha uelewano na upendo miongoni mwa Wanyarwanda bila ya kujali mmoja ni Mtutsi, Mtwa au Mhutu.
Si Rwanda pekee, nchi nyingi duniani wameutumia mchezo wa soka kama sehemu ya kuwakutanisha na kufanya mambo muhimu kwa ajili ya jamii.
Angalia Afrika Kusini iliyopata mafanikio katika kupambana na maambukizi ya virusi vya ukimwi kupitia mchezo wa soka. Hali ilikuwa mbaya, lakini kupitia soka, nafuu ikawa kubwa.
Jaribu kuwauliza watu wengi kuhusiana na mshambuliaji wa Yanga au kiungo wa Simba anaitwaje. Lakini fanya hivyo kama unataka kujua mbunge wa jimbo fulani, itakuwa kazi kukutamkia.
Hiyo ni sehemu ya kuonyesha michezo inapewa nafasi kubwa na jamii ya Watanzania na nguvu yake iko juu. Hivyo wananchi wanaweza kupata somo la kuwarejesha na kuwakumbusha umuhimu wa kuwalinda tembo hao.
Lakini inawezekana kuwashawishi majangili hao, kwa kuwa ninaamini lazima watakuwa ni sehemu ya wanamichezo au wapenda soka, kwamba hata wapenda michezo wenzao wanapinga. Inawezekana ikawa vigumu kuamini lakini ukweli unabadilisha wengi, labda wale viburi ambao watakataa makusudi.

Sitaki kuingilia kampeni hizo ambazo zinaonyesha kuwa kweli Tanzania na nchi nyingine jirani zimenuia kweli kupambana nao ujangili huo. Lakini lazima muamini, kama ni kufikisha ujumbe kwenye jamii, soka ina nguvu.
Inawezekana hamkuwa mmefikiria nilichowakumbusha leo, lakini bado hamjachelewa na pia ujumbe kwa wengine; msisahau kuwa michezo hasa soka ina nguvu na sauti yake ni ya juu zaidi kuliko ile ya wanasiasa. Hivyo itumieni.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic