March 1, 2014


MIMI nianze na kusema kuwa lazima tukubali kuwa wenzetu Waarabu wamekamilika katika suala la mpira, ukianzia maandalizi na hata mipango, wako makini kweli kama ukiwalinganisha na sisi.

Mwaka 1985, ilibaki kidogo sana tuweke rekodi ya kuwatoa Al Ahly katika michuano ya kimataifa, lakini tukafeli kidogo sana kwa uzembe wa viongozi wetu.
Mjini Mwanza tuliwafunga mabao 2-1, mimi nikianza kufunga la kwanza, halafu nikatoa pasi na nahodha wangu, Mtemi Ramadhani akafunga bao la pili lililowamaliza. Baada ya mechi hiyo wachezaji tukaomba kuweka kambi jijini Mwanza, lakini haikuwa hivyo.
Viongozi wakasisitiza turudi Dar es Salaam, lakini wiki nzima, kambi haikuwekwa na ilikuwa vigumu kuwaona. Hata siku tulipofika Cairo, Misri tukalazimika kufanya mazoezi usiku na kesho yake tukafungwa mabao 2-0, tena kwa taabu sana. Wao wakasonga mbele.
Kwa wachezaji wa kipindi kile, kweli tulikuwa tunajituma sana na tuliona sifa kupata mafanikio, lakini hatukupenda hata kidogo kuwaangusha mashabiki wetu, kitu ambacho wachezaji wa Yanga wanapaswa kufanya Jumamosi (leo).
Nimesikia kuna ahadi wamepewa, hilo ni jambo zuri lakini wasipokuwa makini itakuwa ni kazi bure ndiyo maana ninasisitiza kuwa lazima wawafikirie mashabiki watakaojitokeza kwa wingi uwanjani siku hiyo kwamba hataki kushinda na wakijituma wana uwezo wa kushinda.
Sisi tulitolewa kwa uzembe wa viongozi wetu, wao viongozi wao wanajitahidi ikiwa ni pamoja na kuwapa kambi nzuri, maandalizi mazuri pamoja na ahadi. Hivyo wana kila sababu ya kufanya vizuri.
Lakini kitu cha muhimu lazima wasisahau kwamba jamaa wamekamilika kama nilivyosema awali, watuelie na waonyeshe wako nyumbani. Maana wachezaji wa siku hivi wakiona uwanja umejaa, wanachanganyikiwa, wanakuwa waoga.
Waachane na uoga, wawajali mashabiki na huu ndiyo wakati mzuri kwa wachezaji wa Yanga kusema sasa inatosha, wawafunge Al Ahly na inawezekana kabisa.
Kama wakisema hivyo, huu ndiyo utakuwa wakati sahihi wa dunia kuijua Yanga, maana kuitoa Al Ahly ambao ni mabingwa wa Afrika, timu bora bara hili. Dunia nzima itapata habari hizo, ninasisitiza, hilo linawezekana.
Inawezekana sisi wadau, au waandishi wa habari na vyombo vyao kwa ujumla wakaamua kuisifia na kuipamba vilivyo Yanga kwa lengo la kuipa moyo, lakini wenye uamuzi wa mwisho ni wachezaji wenyewe.
Nidhamu ya mchezo ni jambo la muhimu sana na wachezaji wetu wengi hawana, limekuwa ni tatizo lao kubwa sana. Wale Al Ahly wana nidhamu ya juu sana ya mchezo, wanajua nini cha kufanya kwa ajili kila wanayekwenda kupambana naye.
Mimi wakati nacheza, nilikuwa naucheza mchezo kabla ya kuingia uwanjani. Nikifumba macho hivi naona nitafanya hivi na vile, mipango ni mapema na nikiingia uwanjani nihamu ni ya juu. Kingine Yanga waangalie wasifungwe bao la mapema, maana watateseka sana maana Ahly wakiipata nafasi hiyo, basi wanajua wafanye nini.
Mogela ni mshambuliaji wa zamani hatari wa Simba na baadaye Yanga. Ndiye alikuwa mmoja wa wachezaji wawili wa Tanzania kutikisa nyavu za Al Ahly mwaka 1985 wakati Simba ikiifunga timu hiyo mabao 2-1 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic