June 30, 2014



Na Saleh Ally
ASIYEPENDA kusikiliza maoni ya watu, akaamini anajua kuliko mtu yeyote, mara nyingi huishia kufeli, kuna mifano ya watu wengi sana.


Lakini katika kusikiliza, si lazima kila unaloambiwa ulifanyie kazi, kwa kuwa kuna maoni ambayo yanaweza kuwa si sahihi, ukisikiliza kila uliloambiwa na kuliamini, pia unaweza kufeli.

Ndiyo maana Wanasimba wakamuamini Evans Elieza Aveva na kumpa urais kwa kuwa wanajua ana uwezo wa kuikwamua klabu yao kutoka kwenye matatizo, migogoro, kashfa kibao za uuzaji wachezaji bila ya kupata fedha na mengine mengi.

Pamoja na malumbano kwa zaidi ya mwezi kuhusiana na uchaguzi mkuu, hatimaye wanachama wa Simba, jana waliamua kumpa Aveva dhamana ya kuiongoza klabu yao hiyo ambayo inahitaji mabadiliko ili kurudi kwenye maendeleo na sifa yake kwa kuwa Simba ni klabu maarufu barani Afrika na yenye mafanikio katika nyanja za kimataifa kwa hapa nyumbani.

Simba imekuwa kwenye utulivu kwa miaka mingi, kabla ya uongozi wa ‘uncle’ Ismail Aden Rage, haujaingia madarakani ambao katika miaka minne ni mwaka mmoja tu ulikuwa una mafanikio, baada ya hapo ni migogoro, uadui na matatizo lukuki.

Matatizo yaliyoondoa umoja ndiyo yaliyoifanya Simba kupoteza sifa yake ya sharubu imara na badala yake karibu kila timu, zikiwemo hata Mbeya City iliyopanda daraja, zikaanza kuisumbua, kuifunga na hata ukipenda unaweza kusema waliionea Simba.

Simba haikuwa Simba tena, ndiyo maana wakati Wanasimba wanakupa kura, wengi wao watakuwa wanataka mengi lakini mawili furaha ya moyo, yaani kuwa na timu inayoshinda na maendeleo ya klabu, vitakuwa ni vitu vya kwanza kabisa.

Vipande:
Simba imevunjika vipande, kipindi cha Rage kilikuwa cha hovyo, watu hawakuwa na upendo, hawakuelewana na mwisho kila mmoja akaishi kwa kuangalia maslahi yake na si yale ya Simba tena.

Ndiyo maana uliona Simba ilivyoyumba, kwa kuwa kila mmoja aliigeuza chukua chako mapema, hivyo una kazi ya kuzuia hilo na badala yake kila mmoja afanye kwa maslahi ya klabu.

Siri:
Inawezekana watakaosoma makala haya, wataelewa lakini siri itabaki kuwa ya kwako kwamba siku zote msemakweli, anachukiwa.

Wala usisimame, songa mbele kama utakuwa unafanya mambo kwa ajili ya maslahi ya klabu. Pia ningekushauri hata kama utakuwa unajua mambo mengi ya klabu hiyo kuliko mimi, usikubali kupendwa sana.

Nimeona viongozi wengi wanaoingia madarakani wamekuwa wakipenda sana kuonekana watu wazuri wanaotaka kumfurahisha kila mtu, ni kosa kubwa.

Kama kuna mtu au kundi la watu linaharibu, basi waeleze ukweli kwa nia na njia nzuri na mwisho lengo liwe umoja na kusaidia kuijenga Simba.

Umoja:
Kama nilivyoeleza awali, Simba ya sasa iko katika vipande. Moja ya kazi kubwa ni kuunganisha makundi makubwa ambayo chuki zao ni zile za kibinadamu na zinaiumiza Simba.

Najua hauwezi ukafanya mambo yote kwa wakati mmoja, lakini umoja ni kati ya mambo ya mwanzo kabisa kuanza kuyafanya kwa kuwa bila ya kuwa pamoja hakuna kitu kimoja kinaweza kuwa cha umoja na kushika namba moja.

Binadamu wana kawaida ya kusahau, huenda wako waliokuwa na hasira kwa kuwa walitaka kugombea wakaondolewa, wengine wana hasira kwa kugombea na kushindwa. Lakini wote hao ni Simba na wana uwezo wa kuisaidia klabu yao.

Hivyo Aveva, una kazi kubwa ya kuwaunganisha Wanasimba hata kama itakuwa ni taratibu huku ukiendelea kufanya mambo mengine ya mafanikio.

Simba ni kubwa, kwa hali iliyokuwa imefikia, haiwezi kubadilika ndani ya siku mbili na kila kitu kikaenda tofauti. Lazima muda wa kutosha unatakiwa.

Lakini hakuna mabadiliko yatakayopatikana kwa siku moja bila ya kuanza taratibu. Hivyo ni vizuri kuanza taratibu kuwaunganisha Wanasimba kwa ajili ya kujenga Simba moja imara kuliko ‘visimba’ vingi visivyokuwa na ushirikiano na mwisho ni kuiua tu nguvu ya klabu hiyo.

Najua utakuwa na kazi kubwa sana, karibu usaidie kuendeleza soka na kama kawaida, ukipatia tutakumwagia sifa za kutosha, lakini siku ukikosea, basi ukweli ndiyo ada.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic