June 16, 2014


Na Saleh Ally
ENGLAND haikuwa imepoteza mechi yake ya kwanza ya Kombe la Dunia tokea mwaka 1986, lakini usiku wa kuamkia jana, haikuwa na ujanja dhidi ya Italia ‘Azzurri’.
England imelala kwa mabao 2-1 na sasa iko kwenye dakika za kifo, kwani mechi yao inayofuata dhidi ya Uruguay, iwapo kati ya timu hizo moja itapoteza, basi safari ya nyumbani imewadia.
Wakati England imepoteza mechi hiyo kuna mengi yataibuka lakini chanzo, kivutio cha mchezo huo alikuwa ni kiungo wa Italia Andrea Pirlo mwenye umri wa miaka 35.


Kiungo huyo wa mabingwa wa Italia, Juventus ndiye alikuwa kila kitu aliyeichanganya England alivyotaka yeye, akaipeleka mechi hiyo iende alivyopanga yeye.
Kuna mambo mengi Waitaliano walifanya lakini la kwanza, kila walipopata mipira, kabla ya kwenda mbele ilikabidhiwa kwa fundi huyo ili aanze kupanga anataka waende vipi na alifanya hivyo.
Kila walipohisi kuna presha kubwa ya kushambuliwa, basi ikitokea wamepokonya mpira kutoka kwa wachezaji wa England, Pirlo alikabidhiwa mpira naye anaanza kazi ya kupanga mipango ambayo ilikuwa ina madhara kwa England.
Kitakwimu, England ilimiliki mpira kwa 25% na Italia 75%, kazi kubwa ikifanywa na Pirlo ambaye alikuwa mchezaji aliyegusa mpira mara nyingi zaidi yaw engine wote katika mechi hiyo.
Ingawa mwisho wa mechi, Mario Balotelli aliyefunga bao la pili na la ushindi kwa Italia alitangazwa kuwa mchezaji nyota wa mechi, Pirlo alikuwa zaidi ya nyota.
Mashabiki wa Italia, muda mwingi waliimba “olés, oles”, huku Pirlo akiendelea kuupoza mpira na kupanga mechi nzima iende anavyotaka yeye.
Kabla ya mechi hiyo, mmoja wa memba wa benchi la ufundi, Gary Neville alianzisha zoezi la kumdhibiti babu huyo na kuliita “Operation Stop Pirlo”, Neville anaijua kazi yake. Lakini mwisho amefeli.
Juhudi za kumtumia Jordan Henderson, hazikuzaa matunda, mkongwe Steven Gerrard alijitahidi, lakini kazi ilikuwa ngumu na hata alipopewa jukumu hilo Danny Welbeck, ili amvuruge, bado kazi haikuwa lahisi.
Pamoja na kampeni, Pirlo alipiga pasi 69 katika kipindi cha kwanza na zikafika kwa 96%  ambayo ni ya juu kuliko ya wachezaji wote.
Pia ndiye alikuwa stesheni na anayewaagiza Marco Verratti na Daniele de Rossi, wafanye nini, maagizo yake hayakuwa kwa maneno, badala yake basin a vitendo, kazi ikafanyika.
Awali Kocha wao, Cesare Prandelli aliamua waanze na mfumo wa 4-3-2-1, haukufanya kazi vizuri, wakaingia kwneye 4-1-4-1 na hapo ndipo England ilipofia.
Prandelli amembadika Pirlo jina la “mchezaji wa wote”. Akimaanisha kocha yoyote anaweza kumtumia kwa kuwa anaweza kucheza aina yoyote ya mfumo wa soka.
Yeye ameimuingiza kwenye mfumo wa rejeta, hiki ni kifaa ambacho hutumika kupoza injini inayofanya kazi. Ndiyo maana gari zinawekewa maji, kupitia rejeta.
Kila Italia walipokuwa wanashambuliwa sana, mpira unapelekwa kwa Pirlo ili kupoza mambo kwa kuwa katika historia yake ya soka, hajawahi ‘kupaniki’.
Pirlo amekuwa akisema hivi: “Kupaniki ni kujimaliza zaidi, mchezo wa soka unatoa zaidi nafasi ya kurekebisha makosa na ukipaniki, unaiua nafasi hiyo, ndiyo maana napenda kutulia zaid.”
Pirlo bado ana uwezo wa kuendelea kutoa somo kwa vijana katika mechi zijazo za Kombe la Dunia. Ukubwa dawa, lakini kazi yake haina mwingine.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic