June 16, 2014



UAMUZI wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kusimamisha uchaguzi wa Simba uliopangwa kufanyika Juni 29, mwaka huu umenishitua na bado sijaelewa vizuri!


Nilikuwa kati ya waandishi waliohudhuria kikao chake wakati akitangaza kuhusiana na uamuzi huo uliojaa kila aina ya mikanganyiko ambayo inayonyesha Simba haitakuwa tena na matumaini ya kufanya vizuri msimu ujao, nitaeleza.
Kabla ya kulizungumzia suala la kutofanya vizuri, turudi kwenye hili la kusimamisha uchaguzi na kuutaka uongozi wa Simba kuunda kamati ya maadili ni la kukurupuka na linaonyesha lina jambo ndani yake.
Angalia mambo haya, baada ya kamati ya uchaguzi kufanya kazi yake na kumuengua Michael Wambura, alikata rufaa kwenye kamati ya rufaa chini ya TFF. Kamati hiyo ikachukua uamuzi wa kumrudisha.
Lakini bado kuna wanachama waliendelea kukata rufaa wakijumuisha masuala kadhaa ambayo mengine yalipelekwa na kamati ya uchaguzi kwenye kamati ya maadili ya TFF.
Sasa TFF inalirudisha suala hilo Simba, hali ambayo ingelazimisha kufuta kwanza kwa uamuzi uliotolewa na kamati ya rufaa ya TFF. Maana jambo hilo liliishatoka kwenye mikono ya Simba na kuingia TFF, sasa limerudishwa tena kwenye klabu hiyo wakati vyombo vya shirikisho hilo viliishatoa maamuzi!
Tayari huu ni mkanganyiko mkubwa! Pili, TFF imeagiza kuwa hadi Juni 30, siku moja baada ya tarehe ya uchaguzi waliokuwa wamepanga Simba, ndiyo uundaji wa kamati hiyo ya maadili iwe imekamilika.
MALINZI

Itakayofanya kazi ya kuunda kamati hiyo ni kamati ya utendaji. Sasa hicho ndiyo kichekesho cha kuvunja mbavu na hata magoti, kama Wambura amerudishwa kugombea, maana yake bado ni mjumbe wa kamati ya utendaji.
Maana yake naye atashiriki kuunda kamati ya maadili ambayo itafanya kazi ya kujadili masuala yanayompinga yatakayowasilishwa kwenye kamati hiyo. Ingekuwa kabla ya mchakato wa uchaguzi kama ilivyofanyika kwa kamati ya uchaguzi sawa, si sasa uchaguzi umeanza na fitna kibao.
Inajulikana uongozi uliopita chini ya Ismail Aden Rage umegawanyika akiwemo Rage mwenyewe. Wengine wanaunga mkono huku, wengine kule, hivyo suala la kamati hiyo ni vurugu mpya ndani ya Simba, TFF na Malinzi wanalijua hilo.
Nikirudi kwenye hoja ya kwanza kabisa, kwamba Simba itaendelea kuteseka, kwa kuwa haitakuwa na muda tena wa maandalizi, nasherehesha na suala hilo la uundaji wa kamati ambalo mwisho wake ni Juni 30.
Halafu zitapangwa siku za kukaa kwa kamati hiyo mpya, ndani yake kutakuwa na muda wa wale watakaokata rufaa kwenye kamati ya maadili ya TFF kama hawataridhika na uamuzi wa kamati ya maadili ya Simba.
Kimahesabu, inaonekana uchaguzi wa Simba unaweza kufanyika mwishoni mwa Juni. Mwezi mmoja kabla ya ligi kuanza, itakuwa Agosti 24, sasa jiulize lini uongozi mpya utaingia madarakani na kuanza kufanya usajili, maandalizi ya timu kwa uhakika?
TFF wanalijua hilo, hata kama watasema hawahusiki wanajua namna Simba imekuwa na machungu mambo kwenda hovyo kwa ajili ya kutaka kufanya kitu Fulani. Awali, nilianza kupata hisia huenda ni kwa lengo la kumlinda mtu Fulani ndiyo maana mambo yanakwenda shaghalabaghala bila ya kujali maslahi ya Simba.
Lakini Malinzi akajibu swali la kwamba kuna taarifa anambeba Wambura kwa vile alikuwa ni kampeni meneja wake. Yeye akasema hakuwahi kutangaza hilo na watu wanamzushia.
Kwa kuwa limetoka mdomoni mwake, si vibaya kumuamini. Lakini hili la uchaguzi kusimamishwa, kusubiri kuundwa kwa kamati ya maadili katikati ya uchaguzi wa Simba ni kuiangamiza Simba. Nasisitiza TFF inalijua hilo.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic