June 30, 2014



KWA mara nyingine, Yanga imeingia kuwa moja ya klabu inayochagiza katika masuala ya msisimko wa soka nchini kwa kuamua kuajiri watu watatu kutoka nchini Brazil kwa ajili ya kuitumikia.
Yanga imemuajiri kocha wa zamani wa timu ya taifa, Taifa Stars, Marcio Maximo ambaye pia amechagua msaidizi wake Leonaldo Neiva.

Pamoja na makocha hao wawili, Yanga wamejiri kiungo mchezaji anayeitwa Andrey Coutinho ambaye atakuwa na kazi ya kurudisha kiungo cha Jangwani.
Yanga imewahi  kuajiri makocha wawili kutoka Ulaya, pia wachezaji wawili kutoka Ulaya wote wakiwa makipa kwa nyakati tofauti wakaichezea timu hiyo.

Ilikuwa ni sehemu ya kuonyesha kuwa timu ya Tanzania inaweza kuajiri wachezaji kutoka nchi tofauti ingawa huko nyuma, Malindi ya Zanzibar iliwahi kuajiri mchezaji pia kutoka Brazil.

Safari hii Yanga, imerudi tena na kuweka rekodi nyingine ya kuajiri raia watatu wa Brazil ambao wanakuja kufanya kazi kuhakikisha kikosi chake kinakuwa bora zaidi.
Jambo la wageni hao limefanywa kitaalamu, kwanza Yanga wameanza kumnasa Maximo ambaye uwezo wa kazi yake ulionekana wakati akiinoa Taifa Stars. Halafu yeye akapewa kazi ya kutafuta msaidizi pamoja na kiungo.

Yanga haitalaumiwa kwa kuwa Maximo ambaye amepewa kazi ya kuinoa Yanga kwa mafanikio ndiye ameachiwa apendekeze wa kufanya nao kazi kutoka nchini kwao Brazil. Kila kitu kimekwenda kitaalamu.

Vizuri kuupongeza uongozi wa Yanga kwa hatua uliopiga ambayo itakuwa ni changamoto au funzo kwa aina yoyote ile. Mfano Wabrazil hao wakifanya vema kutakuwa na somo, lakini wakifeli, bado kutakuwa na jambo la kujifunza kwa wadau wa soka nchini.
Pamoja na hivyo, kuna kila sababu ya kuamini Coutinho kama mchezaji hawezi kuwa malaika katika kikosi cha Yanga kwa kuonekana ujio wake kama kila kitu kimemalizika.
Wala kusiwe na wanaoamini, huenda Coutinho atakuwa na uwezo wa Ramirez wa Chelsea au Neymar wa Brazil kwa kuwa tu wote ni wachezaji kutoka Brazil, hiyo haiwezi kuwa sawa.
Matarajio ni kuona Coutinho anatoa mchango wake katika kikosi cha Yanga kama ambavyo mchezaji yoyote ‘profesheno’ anatakiwa kuifanya kazi yake anapotoka nchini kwao na kwenda kucheza nchi nyingine.

Bila shaka atakuwa anajua kwamba ana deni kutoka kwa uongozi na wanachama wa Yanga ambao wanatarajia kuona makubwa kutoka kwake. Lakini makubwa hayo yasiwe ya kipimo cha umalaika, watu kuamini huenda hakosei au akicheza katika kikosi Yanga haiwezi kufungwa.

Bado wachezai walio Yanga wanapaswa kumchukulia mchezaji huyo kama changamoto, lakini suala la kugombea naye namba linabaki palepale na lazima washindane naye na kushirikiana naye pia ili kuifanya ofisi yao ambayo ni Yanga inapata mafanikio.

Kumvika umalaika, itakuwa ni tatizo na huenda itawaingiza Yanga kwenye presha kubwa, mfano kama vile kuamini akiwepo yeye, basi wao hawawezi kufungwa au lazima watafanya vizuri.

Coutinho atakuwa na uwezo wa kufanya vizuri zaidi kama atapata naye atatoa ushirikiano ili kujenga kikosi imara cha Yanga ambacho kinataka kufanya vizuri katika michuano ya nyumbani na ugenini.
Hakuna ubishi lazima Mbrazil huyo atapata shida mwanzoni, kuna suala la mazingira ambayo lazima yako tofauti nay ale ya Brazil, hivyo atahitaji muda nab ado watu wanapaswa kulikubali hilo.

Lakini kama itagundulika hana lolote, basi bado Yanga wana haki ya kukataa kuuziwa Ubrazil na badala yake watake mchapakazi. Mara moja uongozi unaweza kuchukua hatua na kumrejesha kwao.

Hivyo kumuunga mkono ni jambo bora sana kwa maana ya kumsaidia afanye kazi yake vizuri. Lakini pia kuwa wazi kama wakiona ameshindwa kazi, basi litakuwa jambo zuri ili kuonyesha kwamba wako ‘siriaz’ na wasingependa kuona utani kwenye maendeleo ya klabu na timu yao.
Tusubirini tuone.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic