July 2, 2014



Na Saleh Ally
TANZANIA ndiyo tumekwama Kombe la Dunia, huenda mimi na wewe ambao tuna kati ya miaka 25 hadi 35, tutaendelea kulishangilia kwa kujichagulia nchi za wenzetu hadi hata kama Mwenyezi Mungu atatujaalia kufikisha miaka 80.


Usiseme natanguliza uchuro, lakini jiulize mipango iko wapi ambayo unaweza kuiita madhubuti kwamba itafikia siku na sisi tutakwenda kucheza michuano hiyo mikubwa ya soka duniani.

Kila baada ya miaka minne, Kombe la Dunia linafanyika, sisi ‘ayaaa’, ilibaki kidogo tuende, halafu miaka mingine minne, tunarudia hayohayo bila ya kuona haya hata chembe.

Kila kiongozi anayeingia anakuwa na mipango yake, haiendani na yule aliyemaliza muda wake, maana yake kila baada ya muda tunakuwa na mipango mipya, si endelevu. Maana yake tutasubiri bila kupata na watu wanaona poa tu!


Sikioni anachokifanya Jamal Malinzi wa TFF, unaweza kusema tutakuwa na uhakika wa kushiriki Kombe la Dunia 2018 nchini Urusi. Mwisho tutajisikia, aah ilibaki kidogo tu au kisingizio tunaonewa.

Lakini hatuna tofauti na wale ambao wanafuzu kwenda kwenye michuano hiyo, wanaonyesha ndani ya Afrika kuna matatizo makubwa na hata kama tutapata nafasi ya kushiriki kwa timu zetu tano, tutaendelea kufeli.

Afrika ina nafasi tano, usisahau Tanzania haijawahi kupata, lakini wanaopata nafasi hizo, wengi wanaonyesha bara hili lina uwezo mkubwa wa vipaji vya soka, lakini matatizo ni mawili, fedha na nidhamu.

Fedha kwa maana ya kupata kila kinachotakiwa ndiyo maana wanaofanya vizuri wakiwa na timu zao kwenye Kombe la Dunia, wanatokea barani Ulaya au kwingineko. Unaweza kujiuliza hivi, vipi Asia wenye timu nne nao walifeli kupitisha hata timu moja kwenda 16 bora?

Afrika ilipitisha mbili, Algeria na Nigeria na zote zimeng’olewa? Jibu hapa kuna mambo mawili pia, kuzidiwa uwezo kutokana na ubora wa wenzetu. Ila Nidhamu ndiyo limekuwa tatizo kubwa sana, nitaeleza.

Cameroon, waligombea posho, wakagombana kambini, mmoja wa wachezaji wao Alex Song, akamtwanga mtu ‘kipepsi’ hata hana mpira!

Ivory Coast, kumekuwa na mgogoro wa chinichini, inaonekana tayari kuna makundi kati ya wakongwe na wale chipukizi ambao alikuwa anawaamini zaidi kocha Sabri Lamouch. Mwisho wametolewa kama wengine.

Ghana, hakuna anayeweza kukataa kwamba walikuwa na kikosi bora kabisa, bahati mbaya wakaangukia katika kundi gumu dhidi ya Ujerumani, Ghana na Marekani lakini bado walionyesha kiwango.

Katikati ya mapambano, Sulley Muntari akamtwanga kiongozi, Prince Boateng akaanzisha tafrani, wote wakatimuliwa. Kikosi kizuri lakini nidhamu mbovu na hakuna tofauti na wengine.

Angalia Nigeria na Algeria, wameonyesha mfano, ndiyo maana walifanikiwa kufika hata 16 bora. Nidhamu imewavusha kwa kuwa ukisema timu bora, zile tatu zilizotoka mapema ndiyo zilipewa nafasi ya juu zaidi kuifikisha mbali Afrika.

Nigeria na Algeria ndiyo walionekana hawana nafasi kwa maana ya uwezo wa vikosi vyao, ukiangalia majina au wale wachezaji wakubwa.

Lakini wamekwenda mbali zaidi kuliko waliopewa nafasi kutokana na kuwa na uwezo na wenye majina makubwa. Hii ndiyo maana sahihi ya nguvu ya nidhamu katika mchezo wa soka.

Watanzania tunalilia kwenda Kombe la Dunia, lakini tuamini inawezekana nidhamu ya chini ya viongozi wa shirikisho, klabu zetu na wachezaji wenyewe pia inaweza ikawa inatuangusha.

Nidhamu ni udhaifu mkubwa katika mambo mengi barani Afrika, hakuna ubishi hata nyumbani Tanzania huo ndiyo udhaifu wa wengi, taasisi nyingi na mwisho tunajikamua kutupia watu lawama bila ya kujikagua.

Tusiache mifano hii ikapita tu, tujifunze kuwa inawezekana kabisa kufanikiwa kwa uwezo wa fedha na kipaji. Lakini nidhamu inaweza ikawa ni nguzo ya kubadilisha mambo na mwisho ikawezekana tukacheza Kombe la Mataifa Afrika na baadaye Kombe la Dunia.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic