August 9, 2014



Na Saleh Ally
GARETH Bale ndiye mchezaji ghali kuliko wote duniani katika kipindi hiki baada ya uhamisho wake wa pauni milioni 86 kutoka Tottenham Hotspur kwenda Real Madrid kuweka rekodi mpya.
Pamoja na kuwa ghali, mwenye fedha za kutosha, tokea kuanza kwa maandalizi ya msimu Bale amewashangaza wengi baada ya kuwahi mazoezini kuliko wachezaji wote.

Achana na kuwahi mazoezini, zaidi ya mara 15, wachezaji wa Madrid wameondoka mazoezini na kumuacha yeye akijifua pekee.
Pia wamemkuta akiwa mazoezini ameanza kujifua zaidi ya mara 10, hali inayoonyesha Braza amepania vilivyo kung’ara na kuisaidia Madrid msimu uhao hata kuliko alivyofanya msimu uliopita.
Mazoezi ambayo amekuwa akifanya Bale yakiwemo yake ya kukimbia kasi yameonyesha kiasi gani wachezaji wanaweza kuwa na hamu au tamaa ya kufanya vizuri hata baada ya kufanikiwa.
Wachezaji wengi wa Kiafrika, wakiwemo wa hapa nyumbani Tanzania, mara baada ya mafanikio kidogo tu, basi wanajiingiza kwenye starehe au wanavmba vichwa.
Bale ndiye ghali, ameonyesha kweli ana uwezo lakini bado ndiye amekuwa wa kwanza kufika mazoezini, anawahi na kuanza kabla ya wenzake, lakini anaendelea na mazoezini baada ya kumaliza na wenzake.
Tamaa ya maendeleo haiwezi kupatikana usingizini na hilo linaweza kuthibitishwa na vitendo vya Bale ambaye anajiandaa na msimu mpya wa La Liga huku akiwa amepania kufanya vizuri zaidi ya msimu uliopita.
Kung’ara:
Kabla ya hapo, rekodi iliyokuwa juu ni ile ya Cristiano Ronaldo kutoka Man United na kutua Real Madrid kwa pauni milioni 80.
Baada ya Bale kutua Madrid, mengi yalizungumzwa na uchambuzi kwamba ilikuwa ni vigumu kwake kufanya vizuri au angefunikwa kabisa na Ronaldo.
Wachezaji kadhaa nyota hasa wale wakongwe nchini England walimshauri kubaki Spurs. Lakini raia huyo wa Wales, alizidi kuwa jasiri akahakikisha anafikia alichokuwa nakitaka, kuichezea Real Madrid na kutimiza ndoto yake.
Msimu uliopita, Bale amefanya mengi makubwa ambayo yamethibitisha kuwa yeye ni bora, lakini ni mchezaji anayejiamini na kutaka kufanya na kutimiza anachoona ni sahihi.
Alifanikiwa kucheza mechi 24 za La Liga na kufunga mabao 15, huku akitoa pasi 12 zilizozaa mabao, hilo lilikuwa jibu kwa wote walioamini nyota huyo mwenye miaka 25 alikuwa  hana nafasi ya kung’ara Hispania kwa madai aina yake ya uchezaji haiendani na ile ya La Liga.
Bale ameng’ara, amefanya mambo mawili makubwa ambayo ni furaha ya juu ya viongozi, wanachama na mashabiki wa Real Madrid. Kuifunga Barcelona na kubeba makombe kwani alikuwa mchango mkubwa hadi Madrid ilipobeba ubingwa wa Ulaya kwa mara ya kumi.
Msimu mmoja tayari ana makombe mawili, Copa de Rey na Ligi ya Mabingwa, lakini jamaa bado hajaridhika, anataka tena.
Mechi 10:
Katika mechi 10 za mwisho msimu uliopita, Bale alicheza dakika 876, alikosa dakika 24 tu baada ya kucheza dakika 86 wakati Madrid ikiitandika Sociedad kwa mabao 4-0, yeye akipachika moja.
Mechi nyingine ambayo alicheza 70 ilikuwa ni Madrid ilipoitwanga Almeria kwa mabao 4-0, Bale akafunga moja. Katika mechi hizo kumi amefunga jumla ya mabao sita.
Katika mechi hizo kumi, pamoja na kufunga mabao sita, Bale amekuwa nyota wa mchezo mara tatu, wakati Madrid ilipoichapa Malaga 1-0, halafu dhidi ya Rayo Vallecano waliyoshinda 5-0 pia walipoitandika Barcelona 2-1.
Bale ameweka rekodi ya juu zaidi katika mechi dhidi ya Rayo Vallecano ambayo Madrid ilishinda kwa mabao 5-0, yeye akafunga mawili, akawa nyota wa mchezo lakini akapata alama 10 za ubora wa mechi. Kama ungekuwa ni mtihani, alipata mia kwa mia.
Inawezekana Bale anataka bado kuonyesha ubora wake, lakini anajua bila ya mazoezi ya kutosha hataweza kufanya vizuri wala kuuonyesha ubora huo. Funzo kwa wale wanaojiandaa na Ligi Kuu Bara pia, kwamba kipaji au uwezo pekee bila mazoezi ya kutosha, haitoshi.

Mechi 24
Mabao 15
Asisti 12
Kilo 74
Urefu mita 1.83



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic